NA MARYAM SALUM, PEMBA@@@@
‘……kidogo kidogo ndio mwendo……’.
Ni msemo wa kiswahili unao maanisha kufanya mambo hatua kwa hatua, subira
na umakini ndiyo njia bora na salama ya
kufanikisha malengo.
Msemo huu unaenda
sambamba na safari ya Mkunga kutoka kazi ya Ualimu, hadi ulingo
wa kisiasa kuwa Makamo Mwenyekiti ngome ya Wanawake Taifa wa ACT.
TUMJUE MKUNGA.
Mkunga Hamad Sadala (65)
ni mwanandoa, mchakarikaji, mwenye kujiami asiyekubali kuyumbishwa kwani
anajitambua na anajikubali popote.
Alizaliwa mwaka 1961
katika Kijiji cha Uvumbi shehia ya Chanjaani Chake Chake, ni mtoto wa tano (5) na
wa mwisho katika familia ya mzee Hamad Sadala.
Anasema kuwa mnamo mwaka
1966 hadi 1967 wazazi wake walimsomesha
elimu ya awali darasa la kwanza skuli ya
Shamiani hadi mwaka 1978 kumaliza kidato cha tatu skulini hapo.
Anafahamisha kuwa mwaka
1979 aliendelea na elimu yake ya kidato
cha nne katika skuli ya Fidel Castro, na baada ya kumaliza tu darasa lake la
kumi na mbili, aliajiriwa kuwa mwalimu mwaka 1980.
“Kumaliza tu elimu
yangu ya Kidato cha nne, sikukaa niliajiriwa rasmi ualimu, kipindi hicho kazi
inamtafuta mtu na sio mtu kutafuta kazi,” anaeleza.
Alifanya kazi yake ya
kusomesha kutoka mwaka huo katika skuli mbalimbali, ikiwemo Mwanakwerekwe C, Michakaeni,
Vitongoji, Wawi, na Mdungu.
Mwaka 2018, alistaafu
kwa hiari katika skuli ya Vitongoji, na sasa amejikita zaidi kwenye masuala ya siasa,
katika nafasi mbali mbali za kichama.
Kwa sasa ni mwanasiasa,
hasa tokaa alipostaafu kazi yake, na ni mwanachama halali wa Chama cha ACT
Wazalendo, na amekuwa kiongozi kwenye ngazi ya tawi, Jimbo,Mkoa na Taifa.
Anasema sasa
kwenye chama ni Makamo Mwenyekiti wa gome ya Wanawake Taifa, pia ni mjumbe wa
halmashauri kuu Taifa kupitia Chama chake hicho.
Mkunga anaelezea nafasi
mbali mbali ambazo aligombea kama mwanamke, tokea mwaka 2020 amesimama kidete
kugombea nafasi ya Ubunge kwa bahati mbaya hakupita.
Mwaka 2025 anasema
hakukata tamaa bali alijitokeza kugombea nafasi ya Ubunge Viti maalumu pia hakufanikiwa.
“Sababu zakutofanikiwa zipo nyingi, ambazo
hata yeye hakuwa tayari kuzitaja, ingawa wanawake wenzake walikwa wanamkubali,”anaeleza.
Anafahamisha kwenye siasa
kumekuwa na changamoto nyingi, ikiwemo kuitwa majina mabaya kutukanwa, hivyo
ustahamilivu ndio msingi wake mkuu.
Aneleza licha ya
changamoto anazopitia katika kusaka uongozi Jimboni, bado anaendelea kuwa na
subira, akiamini ipo siku itatiki tu, kwani kama ipo ipo tu.
Kwa upande wa Wanawake
wenzake ushirikiano ulikuwa mkubwa na ulimpa matumaini yakufanikiwa Jimboni,
lakini kutokana na sababu zisizoepukika zilimfanya yeye kutofanikiwa.
Anafahamisha kuwa upande
wa kijamii anaishi vizuri, kwani anapokwenda sana kushauriwa na kila mtu na huo
ndio utu na ili kufika mbali kunahitajika hayo.
“Katika jamii iliyonizunguka
nathubutu kusema inanipenda sana, kwasababu hata mimi nawapenda iwe mkubwa,
mdogo na hata awe chama chingine.
Anaeleza mtu yoyote
anapoamua kuingia kwenye siasa ni vyema kuangalia ubinadamu kwanza, kwani kabla
ulikuwa unaishi na jamii na utahitaji kurudi kwa watu baadae.
Kumbe anaona wala siasa
si chaka la ubaguzi, fitna bali ni njia ya kujichanganya na watu zaidi na
kukufanya kujulikana ndani, nje na hata kwenye mataifa ya mbali.
Anaeleza mwanamke kama kiongozi
kwenye chama chake, atahakikisha anaendelea kuishi na jamii kwa mashirikiano,
kwa hali na mali bila kujali nafasi yake, ili aweze kufikia malengo yake.
Mkunga, kukata tamaa
kwake ni mwiko kwani moja ya ndoto zake ni kuwa kiongozi wakuchaguliwa na
wananchi kwenye Jimbo lake, ili aweze kusaidia jamii katika kutatua changamoto
zinazoikabili jamii.
Nje ya siasa, Mkunga ni
mwanaharakati wa elimu, na ndio maana aliwahi kumsaidia kijana ambae aliacha masomo,
baada yakufanya mitihani yake ya darasa la saba kutokana na hali ya maisha yao
kuwa duni.
“Kama mwanamke mwenye nafasi kwenye Chama
changu, sikuwa tayari kuona maisha ya kijana huyo yanafifia, nilihakikisha
napambana, ili kumsaidia kijana huyo, aweze kurudi masomoni,’’anasema.
Kwa vile Mkunga ni
mpenda maendeleo, hupenda kujishusha kwenye jamii na mwenye kuthamini taifa
akiamui kuwa, vijana na wanawake ndio nguvu ya nchi pahala popote pale.
Eneo jingine, ilikutana
na kijana huyo Ali Faki Mohamed, hamsahau Mkunga, akisema anamfananisha na mzazi,
wake baada ya kumpania hadi kufikia kidato cha pili mwaka huu.
Ndio maana Mkunga anawashauri
viongozi wengine wanaposhuhudia changamoto kama hizo, wala wasisubiri kila kitu
serikali, wachukue hatua maana ndio uzalendo unaoimbwa kila siku.
Baba mzazi wa kijana huyo Faki Mohamed Faki,
anasema kuwa Mkunga anajua maana ya maendeleo, na ndio maana baada ya kusikia changamoto
yam toto wangu, alichukua juhudi za haraka.
Anasema amekuwa akijitoa
kwenye jamii yake, na kuhakikisha vijana wanasoma na kufikia ndoto zao, tena bila
ya kujali chama wala aina ya familia.
“Mtoto wangu kama sio
mwalimu Mkunga na uwanaharakati wake, basi angali potoka kwani alikuwa tayari
kashajiingiza kwenye vikundi viovu, leo nashukuru yulo darasani,’’anasema.
Asha Hamad Khamis
mkaazi wa Vitongoji anasema mwanasiasa huyo na kiongozi ni mtu wa watu, anapenda
watu, anapendwa na jamii, yupo bega kwa bega, popote kwenye shughuli za
kimaendeleo yuko mbele.
“Kwakweli simalizi
kumuelezea kutokana na mambo mengi anayotusaidia iwe harusi iwe msiba, harakati
za elimu na hata kupigia miradi ya maendeleo,’’anasimulia.
Mwanachama wa ACT
Wazalendo Vitongoji Hadia Juma Faki, anasema Mkunga amekuwa mfano kwa wanawake
wote wa ndani ya chama na wale wingine wa nje.
“Nikimzungumzia siasa
yupo vizuri, anajiamini, anapenda ushauri, anajishusha, anapenda kushauriwa na
kila mtu, sio mtu wa kuyumbishwa,’’anaeleza.
Mpaji Abass Yussuf anafahamisha
kuwa Mkunga mcheshi, nimpenda kujichanganya na watu hachagui, ingawa kwenye
kutetea hoja huweka mbali utani.
TAMWA
Kaimu Mratibu wa Chama
cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA Zanzibar, ofisi ya Pemba Amina
Ahmed Mohamed, anasema wapo wanawake kadhaa, waliowapa elimu ya kugombea,
akiwemo Mkunga.
Anasema wamekuwa na
miradi kila baada ya muda, ukiwemo wa wanawake na uongozi SWIL, ambao uliwatoa
wanawake wingi na sasa ni viongozi akiwemo Mkunga.
‘’Kwa mfano Waziri wa
Habari, Mwakilishi wa Jimbo la Konde, huyo Mkunga, alikua mkuu wa Mkoa wa
kaskazini Pemba ni kundi la wanawale waliopitia mikononi mwa TAMWA kwa baadhi
ya wakati,’’anasema.
Anakikiri kuwa mafunzo
hayo, sio tu kujifunza wao namna ya kugombea, lakini kujiamini, kujitetea,
kutoa hoja na kufanyakazi kwa bidii.
Amina anasema TAMWA wakati
mwingine huwa na miradi hata ya kuwawezesha waandishi wa habari, ili kuwaibua
wanawake waliofanikiwa kama Mkunga na wingine, kwa lengo kuwaonesha jamii uwezo
wao.
KATIBA
Katiba ya Zanzibar ya mwaka1984
inatambua na kulinda usawa wa kijinsia katika uongozi kwa kuhakikisha wanawake,
kama sehemu ya jamii, wanashiriki katika vyombo vya maamuzi.
Kwenye kifungu chake
cha 21, kinasiistiza, ‘kila mzanzibari anayo haki ya kushiriki katika shughuli
za utawala wa nchi, ama moja kwa moja au kupitia wawakilishi waliochanguliwa,’
Hata kifungu cha 12,
cha katiba hiyo kinabainisha kuwa, ‘haki ya usawa mbele ya sheria na
wanayohaki bila ya ubaguzi wowote kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria’.
Mkunga Hamad Sadala (65) ni
mtoto wa watano kwenye familia ya Hamad Sadala kwa sasa ndie makamo mwenyekiti
ngome ya wanawake taifa kwenye chama cha ACT-Wazalendo na bado ana nia ya kujitupa
jimboni mwaka 2030.
Mwisho



Comments
Post a Comment