NA ZUHURA JABIR, ZNAIBAR “Usafi ni nusu ya afya." Haya sio msemo wa utani, bali ni ukweli unaogusa maisha ya kila siku ya wananchi. Mazingira safi yanamaanisha afya bora, heshima ya makazi na maendeleo ya jamii, lakini pale ambapo mifumo ya usimamizi haieleweki, wananchi hubeba mzigo ambao haukupaswa. Majadiliano yaliyowakutanisha masheha, wahamasishaji wa jamii na wataalamu wa Baraza la Manispaa Mjini, yameonesha wazi kuwa changamoto za usafi wa mazingira bado zinahitaji mshikamano. Methali isemayo, "Kidole kimoja hakivunji chawa," inaakisi hali halisi ya mapambano dhidi ya uchafu wa mazingira. MGONGANO WA MAMLAKA KATIKA UKUSANYAJI WA TAKA Moja ya hoja zilizojitokeza kwa uzito mkubwa ni mgongano wa mamlaka katika ukusanyaji wa taka ndani ya shehia ya Mchangani. Kwa mujibu wa sheha Nassir Mohammed Ali, wananchi wanakabiliwa na hali ya kuchanganyikiwa, kutokana na taasisi mbili, Baraza la Manispaa Mjini na Mamlaka ya Mji Mkongwe, kufanya kazi katika ene...