NA ZUHURA JABIRI, ZANZIBAR ZANZIBAR, ni kisiwa kinachojivunia amani, mshikamano wa kijamii na historia ndefu ya kuishi pamoja. Ingawa nyuma ya taswira hii ya utulivu, kuna sura nyingine isiyoonekana mara nyingi sura ya watu wenye ulemavu, wanaoendelea kusubiri usawa wa kweli . Kwa mujibu wa takwimu rasmi, Zanzibar ina watu 167,308 wenye ulemavu, sawa na asilimia 11.4 ya wananchi wake milioni 1.89. Hata hivyo, katika meza ya maamuzi, katika ajira rasmi, na hata katika huduma za msingi, kundi hilo, bado lipo pembeni. Ijapokuwa sheria ya Watu Wenye Ulemavu ya nambari 8 ya mwaka 2022, inahakikisha haki sawa katika elimu, ajira, afya na ushiriki wa kisiasa. Lakini kati ya maandishi ya sheria na maisha ya kila siku, kuna pengo kubwa pengo linalowaacha watu wenye ulemavu wakionekana, lakini hawasikiki. “Nimejitolea maisha yangu kupambana na ubaguzi dhidi ya watu wenye ulemavu na kuhakikisha hatusahauliki,” anasema Salma Saadat, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake W...