Skip to main content

Vikausha damu vya mjamzito hivi hapa, umo mchele, udongo, mkaa, chaki Uwezekano wa kuzaliwa watoto wenye udumavu, utapiamlo ni mkubwa

 

NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@

‘’KILA ninapobeba mimba nimezoea kula mchele kwa wingi naweza kusamehe pilau au biriani,’’ ndio maneno ya mwanzao ya Bahati Mohamed Ali (sio jina lake halisi).

Nilimfuma akiwa barazani kwake, mjini Ole wilaya ya Chake chake, pembeni yake akiwa na kibakuli cha mwazi, kwa umbali utaona amejaza chakula aina ya pepe, kumbe ni mchele wa Mbeya.

Hujichotea kidogo kidogo na kuushindilia mdomoni mwake, huku akiendela kupiga storia na wenzake, bila ya kujali kuwa ujauzito alionayo na mchele huo hauna mwisho mwema.

Kawaida yake akiwa mjamzito, kila anapoamka asubuhi anaroweka mchele upatao robo kilo hivi…na baada ya kumaliza kupika, yeye huchukua mchele wake kutafuna (kula).

Wakati mwenza wake na watoto wao, wanakula chakula cha mchana, Bahati yeye hukaa pembeni na kibakuli chake cha mchele akiendelea kubahatisha afya yake.

‘’Mimba nyengine hupenda sana kutafuna mchele wa Mbea na nyengine hupenda mchele wa mapembe, kwa kweli huwa nina hamu (kileo), kwani ikiwa nitakosa sipati hata usingizi,’’anasema Bahati.

Siku zote akiwa mjamzito, faradhi yake ya chakula cha mchana huipunguza kwa ajili ya kula mchele mbichi, uliolainika kwa maji, na kisha siku hiyo kwake kuihesabu imeshapita.

Anakiri kuwa, wanapofika kituo cha Afya, moja ya jambo wanalosisitizwa wasilitumie ni mchele, udongo, chaki wakielezwa kuwa vinakausha damu yake na mtoto.

‘’Mimi najua kuwa unapokula vitu kama hivi ikiwa na mimba havikuathiri lakini nikienda kliniki kupima damu imepungua, kumbe itakuwa ni huu mchele,’’ anasema.

Kumbe sio tu Bahati pekee, anayebahatisha afya akiwa na ujauzito, bali ni wanawake wengi wenye tabia hiyo, huku wakidhani kuwa hakuna madhara yeyote yanayoweza kuwapata.

Mama mmoja mkaazi wa Bopwe Wete ambae hakutaka jina lake litajwe anasema, yeye anapokuwa mjamzito hupenda sana kula udongo na hupata tabu sana ikiwa ataukosa.

‘’Huwa unauzwa kwenye baadhi ya maduka, kwa hiyo unaponimalizikia nanunua mwingine, mpaka najifungua na ndio akili yangu inakaa sawa,’’ anahadithia.

‘’Siku moja nilienda sehemu ambayo naficha udongo wangu lakini sikuukuta kwa iyo akili yangu ikawa haipo sawa na ni usiku wa 4:30, nilimtoa mume wangu akaununue na alikwenda, huwa kama nimechanganyikwa vile,’’ anasimulia.

Anaeleza kuwa, mume wake alikuwa na kawaida ya kumkataza kula udongo na ndio maana siku hiyo akamtoa usiku akaununue, kwani alihisi kuwa aliutupa yeye.

Maryam Khamis mkaazi wa Micheweni yeye anasema, mimba ya mtoto wake wa pili, aliwahi kuingiwa na hamu (kileo) ya kula mawe ya jasi na alikuwa hawezi kulala kama hajatafuna.

‘’Kwa kweli mimba ni kitu chingine kwa sababu, mimi ilinijia hiyo karibu na kujifungua na baada ya kujifungua moyo wangu ulitulia, mpaka leo hii,’’anaeleza.

Anasema, wajawazito wanapokwenda kliniki wanaaswa wasitumie vitu hivyo, ingawa mimba zinawapelekesha kiasi kwamba, hawataki kuufanyia kazi ushauri wa daktari.

Aisha Omar Salum ambae ni Mkunga na Muuguzi wa kituo cha Afya Maziwang’ombe anasema, hali hiyo huwatokea baadhi ya wajawazito, kutokana na upungufu mkubwa wa madini ya chuma na zinki.

Hivyo ubongo unawapelekesha kutafuta vile vitu ambavyo ataweza kupata madini hayo, jambo ambalo sio sahihi, kwani kuna vyakula kama vya mazao ya baharini ambavyo akitumia anapata madini hayo.

“Huwa sio yeye bali ni ubongo unamuamrisha kula kitu Fulani, na hiyo inatokana kwenye mwili wake kumekosekana kitu, ndio maana inampelekea kutamani,”anasema.

Mkunga huyo anasema, mjamzito kutumia vitu visivyo vyakula sio sahihi kwa sababu, anaweza kupata madhara yeye na mtoto wake, ikwemo upungufu wa damu.

Mjamzito anapokuwa na upungufu wa damu, hata mtoto wake pia hukumba, kwa sababu wakati ule kila kitu anategemea, kutoka kwa mama yake.

“Kutokana na hali hiyo mtoto hakui vizuri kimwili na kiakili na hatimae, anaweza kuzaliwa akiwa na udumavu na kukosa ufahamu,” anaelelza.

Daktari huyo anafafanua kuwa, mjamzito anaetumia vitu hivyo, anaweza kuzaa, mtoto ambae atakuwa na uhaba wa damu, ambapo huhitajika kuingiziwa damu papo hapo, jambo ambalo sio zuri.

Dk. Rahila Salim Omar ambae ni Mratibu wa kliniki za huduma na tiba kwa wanaoishi na VVU Pemba anasema, vyakula visivyo vyakula kama udongo, mkaa, chaki, mchele na mengine yanayofanana nayo, si vyema kula kwa mama mjamzito.

Kwani vitu hivyo vinasababisha madhara kwa mama na mtoto, ikiwa ni pamoja na upungufu wa damu, kuzaliwa mtoto ambae ana udumavu.

‘’Tunajitahidi kuwafahamisha wajawazito kuwa vitu hivi havina faida kwao, lakini hii inakuwa kama ni kileo, hivyo ni vigumu kumshauri mama huyu na akakusikiliza,’’ anaeleza.

Anaeleza, wajawazito wengi wanakula vitu ambavyo sio sahihi kwa afya, jambo ambalo humsababishia kukosa damu na hatimae kuzaa mtoto akiwa na matatizo mengi.

Afisa Mtendaji wa Maabara ya  Afya ya Jamii Pemba Said Mohamed Ali anasema kuwa, walifanya utafiti mwaka 2011/2012 kujua sababu zinazomfanya mama mjamzito kula vitu hivyo, ambapo waligundua kuwa ni ukosefu wa madini ikiwemo ya chuma na culsium.



Anasema, ukosefu wa madini ya chuma inasababisha mtu kuwa na safura na ndio maana mjamzito anapokosa, inamjia ale kitu ambacho atayapata, jambo ambalo linaweza kusababisha madhara kiafya.

‘’Madhara yanayopatikana inategemea na vitu anavyokula, vyengine haviwapi madhara na vyengine vinawapa madhara, lakini huwezi kujua ni kipi kisicho madhara, ,’’ anaeleza.

Ali Hassan Bakar mkaazi wa Limbani Wete anasema, akinamama wajawazito wanapoamua kula kitu Fulani, hakuna ambae ataweza kumzuia, jambo ambalo linawapa wakati mgumu sana wanaume.

‘’Na sisi huwa tunaamini kweli kutokana na kuwa akishakujifungua anakuwa sawa na wala hatumii tena vitu hivyo, kwa hiyo ikiwa anataka udongo sisi ndio wanunuzi wakuu kwa kweli’’, anasema baba huyo.

Mkaazi wa Chanjaani Chake Chake Suleiman Khamis Said anaeleza kuwa, mwanamke anapokuwa katika hali ya ujauzito, anakuwa hayupo sawa kiakili na hata kimwili.

NINI KIFANYIKE?

Dk. Aisha anawashauri akinamama wajawazito kuweka vitu mbada kama chipis za muhogo, chauro na njugu ili pale inapowajia hamu ya kula, wavitumie badala ya mawe na udongo.

 Aisha anawashauri akinamama hao kula vyakula vya mboga, matunda na maji mengi ili kuimarisha afya yake na mtoto atakaezaliwa.

Dk. Rahila anawashauri mama wajawazito kuacha tabia ya kula vitu hivyo na badala yake wale vyakula vyenye lishe, ili awe salama tangu siku ya kutunga mimba, mpaka kumlea mtoto.

Anasema kuwa, endapo mama mjamzito atakosa lishe bora, hata mtoto anapozaliwa anaweza kupata udumavu na utapiamlo, hivyo wanaume waelewe umuhimu virutubisho kwa wenza wao.

Afisa Mtendaji wa Maabara ya Afya ya Jamii Wawi Chake chake,  ‘PHL’ Pemba anawashauri mama wajawazito wasitumie vitu hivyo,  ambavyo havina faida kwao.

‘’Elimu kwa jamii inahitajika kuhusu afya ya uzazi, ili wanawake wanapokuwa wajawazito waweze kuimarika kiafya,’anaushauri.

                                                      MWISHO.

   

 

 

 

Comments