‘MWA NASIASA hatakiwi kuwa mbaguzi,
watu wote ni sawa, ili mwisho wa siku, jamii ikuelewe tu,’’anasema Fatma Khamis
Juma Diwani wadi ya Tibirinzi.
‘’Tabia yangu hupenda
kujichanganya iwe kwenye kijiwe cha kahawa, sokoni nipo, masikani za vijana
nipo, na makundi mengine yenye rika tofauti.
Hii ni kauli ya Fatma Juma Khamis, anayehudumu udiwani wadi ya
Tibirinzi, Jimbo la Chake chake, kwa kipindi cha pili mfululizo sasa.
Katika siasa, mtu hatakiwi kuwa mbaguzi na badala yake awe kuwa karibu
na jamii iliyomzunguruka, kwa maslahi mapana.
Anakiri kuwa kuingia kwenye kinyang’anyiro cha siasa, watu wote hupitia
changamoto, ikiwemo kuitwa majina mabaya hasa kwa wanawake.
Kwenye jamii iliyo kubwa, tafsiri iliyopo, pindi mwanamke akiingia
kwenye siasa hubandikwa majina maovu na yenye kukatisha tamaa, au kuwindwa na
washindani wake.
Diwani Fatma anasema, kwa awamu ya kwanza ya udiwani wake, hakuishia
kuomba kura kwa mikutanao ya hadhara pekee, bali alifuata utamaduni wa nyumba
kwa nyumba.
“Katika mbinu zangu za kusaka udiwani wa mwaka 2020, niliamua kwenda
mlango kwa mlango, na sitosahau nilipokosea kuondolewa uhai wangu, baada ya kutaka
kupigwa panga kwa nyakati za usiku, na muombezi wangu ilikuwa ni mbio,”
anasimulia.
Kwa siku hiyo, msaka udiwani huyo, baada ya kuwahadithia wachache,
walimshauri aende polisi kutoa taarifa na chamani kwake, ili kuachia ngazi
nafasi hiyo, jambo ambalo alisita.
“Changamoto hiyo niliyokumbana nayo mwaka 2020, ilikuwa mbolea kwangu,
na ilinitia ari ya kutafuta uongozi, na hadi sasa nahudumu udiwani wadi ya
Tibirinzi, kwa awamu ya pili”, anaeleza.
Bado anashangaa, kuwa bado wapo baadhi ya watu, wanadhana kuwa,
mwanamke hawezi kuwa kiongozi, wakinasibisha na uhuni, kuacha utamaduni na
kuitupa familia, jambo ambalo sio sahihi.
“Mimi ni mama wa familia ya watoto wanne, na kushughulikia wazazi
wengine, lakini bado sijateteresha familia yangu wala udiwani wangu, haujaingia
kasoro.
ALIWAZAJE UONGOZI DIWANI HUYU
Fatma Khamis Juma ambaye ni mrefu wastani, mwekundu mwenye paji la ucheshi,
alianza kuusaka uongozi, tokea ngazi za vijana.
Kwa wakati huo, akiwa ndani ya chama cha Mapinduzi hakuishia kuwa
mwanachama wa kawaida, alianza kupanda daraja za kufika juu, kwa kugombea
nafasi za chini.
Kumbe kila siku zikienda mbele, zikilikuwa zikimpa ujasiri, kujiamini,
kumuonyesha njia na kumpa nguvu ya kutaka uongozi, hadi sasa akiwaongoza wananchi
3,000 wadi ya Tibirinzi.
Ujasiri wa diwani huyo, haunekani tu kwenye nafasi hiyo, bali hata
kwenye mikutano ya kawaida ya kijamii, au ya kitaasisi, husimamia msimamo wake,
wenye tija kwa taifa.
“Hata nilipokuwa masomoni, nilianza kuwa mtetezi wa wenzangu, ili
wasionewe, na wakati mwingine hadi kufika kwa Mwalimu mkuu, ili kutaka
ufafanuzi wa jambo,” anakumbuka.
HEKAHEKA ZA UDIWANI AWAMU YA PILI
Mwaka 2025, Diwani huyo machachari, alizikwea tena ngazi za CCM, wilaya
Chake chake, kwenda kuchukua fomu, ili kuwaongoza tena wananchi wa wadi ya
Tibirinzi.
Baada ya mchakato mzito wa ndani ya chama, hatimaye Fatma aliibuk tena
na ushindi, na kukabidhiwa bendera, ili kuusaka udiwani kwenye uchaguzi mkuu.
Hapo ikawa ni mikutano ya hadhara ya kampeni, kutembea kwa miguu, gari
za matangazo na kurejea tena, kuwafikia wananchi uso kwa uso, ili kuwaomba
kura.
Wakati wa matokeo ya uchaguzi, wanachi kwa mara nyingine walimuamini,
na ndio maana wakaamua kumchagua tena, kushika hatamu ya udiwani Tibirinzi.
CHANGAMOTO ALIZOKUSUDIA KUZIPATIA UFUMBUZI
Diwani Fatma anasema, wakati wa kampeni aligundua ukosefu wa huduma ya
maji safi na salama, kwa baadhi ya vijiji, utoro wa wananfunzi, matumizi ya dawa
za kulevya, na mitaji midogo kwa wajasiriamali.
“Viongozi wote wanajali sana shida za wananchi, lakini akiwa kiongozi
mwanamke kama mimi, huwa tunajali mara dufu, shida zao,” anasimulia.
YALIYOJIRI BAADA YA KUWA DIWANI
Sasa Diwani Fatma Khamis Juma, anakiri kuwa huduma ya maji safi na
salama, kwa kushirikiana na serikali kuu, katika baadhi ya vijiji, imeshakuwa
historia.
Kuhusu matumizi ya dawa za kulevya kwenye wadi hiyo, hivi karibuni
amesharikiana na mamlaka husika, kutoa elimu katika vijiwe sugu, na baadhi yao
kushikiliwa na vyombo vya kisheria.
“Nilikusudia nikiwa Diwani utoro wa wananfunzi iwe skuli au madrassa,
nao umebaki historia, na sasa baadhi ya maeneo yanaridhisha ikiwemo Wesha, na Ndagoni”,
anasema.
WANAOFANYA KAZI NA DIWANI FATMA
Mstahiki Meya, Manispaa ya
Chake Chake, Suleiman Makame Ali, anasema kuwa wadi ya Tibirinzi ilimpima Fatma
kutoka uongozi wake wa awamu ya kwanza, na kumuona anafaa, ndio maana awamu ya
pili, akarejeshwa tena.
“Zipo wadi kadhaa wilaya ya Chake Chake, zimeshapiga hatua ya
kimaendeleo, kwa huduma mbalimbali kuimarika, ingawa hii ya Tibirinzi mwenyewe
kaja”, anasema.
Meya huyo anaeleza kuwa, Wadi ya Tibirinzi ni kubwa, ingawa ukubwa huo
na aina ya Diwani aliyepo, utendaji wake wa kazi ni zaidi ya utendaji wa baadhi
ya wanaume.
Sheha wa Msingini Mkubwa Ali Kombo anakiri kuwa,
wadi yao kwa wamu ya pili mfululizo, imepata kiongozi mwenye maono, ujasiri na
kutimiza ahadi zake kwao.
“Mfano, shehia yetu zipo huduma za ujenzi wa
njia za ndani, ikiwemo ya Msingini kupanda juu, katika kijiji cha Mitambuuni,
na huduma ya maji safi na salama, ambazo zimeshajengwa utawala wa diwani huyu,’’anasema.
Kaimu Mkurugenzi Manispaa ya Chake Chake Mayasa
Amani Vuai anakiri kuwa, katika wadi 10, zote zimetimiza malengo, ingawa ya
Tibirinzi, iko juu zaidi.
“Wadi ya Tibirinzi inang’ara kwa huduma za
kijamii na hapa, nathibitisha kweli mwanamke akipewa madaraka, wananchi
huneemeka,’’ anasimulia.
WANANCHI WA TIBIRINZI WANASEMAJE
Nunuu Mwalim Ngwali anasema Diwani huyo, amekuwa akimfahamu, tokea
ujana wake kwa uchakarikaji na kusimamia misimamo yenye tija.
“Kwa awamu ya kwanza, alipotangazwa kuwa Diwani, sote tulifurahika
maana ukakamavu wake, mbio zake, ujasiri na kuchangamka na kila mtu, tulijua
kuna shida zitatuondokea”, anasema.
Ali Kombo Khamkis anakiri kuwa, ujio wa Diwani Fatma, wadi ya
Tibirinzi imepata heshima kubwa ya kimaendeleo, ni tofauti na awamu zilizopita.
Anakiri kuwa, wameshapita madiwani kadhaa tena wanaume, na walihudumu
kwa vipindi tofauti, walizikuta shida na waliondoka na kuziwacha ndani ya wadi.
Maryam Mohamed Said, anaona kuwa wakati umefika, kwa mfano wao ndani
ya wadi ya Tibirinzi, nafasi za ngazi ya maamuzi viongozi wanawake, wakapewa
fursa zaidi, kwani wanajicho la huruma.
“Naamini kuwa wadi nyingi za wilaya ya Chake Chake, zimefanya vizuri
kwa kuwepo miradi mikubwa na ya kimaendeleo, ingawa wadi yao, inaongoza hasa
baada ya kupata Diwani mwanamke”, anasimulia.
WANAHARAKATI
Mkurugenzi Mtendaji Jumuiya ya Tumaini jipya Pemba (TUJIPE) Tatu
Abdalla Msellem, anasema kwa sasa wanawake, wamekuwa wakiaminiwa na wapiga kura,
kutokana na matokeo mazuri ya baadhi ya wachache, walioshika hatamu.
Anasema wanaendelea kuielimisha jamii, hususani wanaume, kuhusiana na
umuhimu wa kuwaamini viongozi wanawake, kuanzia ngazki ya familia hadi taifa, kwa
mifano iliyo hai.
“Hata hapa Pemba, yapo majimbo, shehia, na wadi zinang’ara kwa miradi
ya maendeleo, na ukiyafuatailia walioshika hatamu ni wanawake”, anasema.
Kaimu Mratibu Chama cha Waandishi wa Habari Wananwake Tanzania TAMWA -Zanzibar,
Ofisi ya Pemba, Amina Ahmed Mohamed, anakiri kuwa nguvu zinazoendelea kuchukuliwa
na TAMWA, wanaharakati, serikali kuu na wadau wake, juu ya kuwapa nafasi wanawake,
zimefanikiwa kiasi.
Anasema kwa miaka ya hivi
karibuni, walau wanawake wanaonekana katika baadhi ya nafasi ya uamuzi, kuanzia
udiwani, usheha, uwakilishi na ubunge, jambo linalotia tamaa kuelekea sera ya
50 kwa 50.
“TAMWA imekuwa na miradi kadhaa, ya kuwawezesha wanawake kutambua haki
na wajibu wao, na kuieleza jamii nafasi ya mwanamke katika kuongoza, iwe ngazi
ya familia, kijiji, mtaa wilaya mkoa hadi taifa”, anaeleza.
VIONGOZI WA DINI
Sheikh Said Abdalla Nassor wa Ofisi ya Mufti Pemba, anasema katika
uislamu, wanawake wanaweza kuwa viongozi katika nyanja nyingi za elimu, jamii,
na maendeleo.
“Wanawake wengi wamekuwa wanazuoni, walimu wa dini na wahifadhi wa
hadithi katika historia ya uislam, hivyo kuwepo diwani mwanamke inaongeza
uwajibikijai,’’anasema.
Katika eneo jengine, Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kifungu cha
21(1), kinabainisha kuwa ‘kila Mzanzibari
anayohaki ya kushiriki, shughuli za utawala wa nchi, ama moja kwa moja, au kwa
kupitia wawakilishi waliochaguliwa kwa hiari’.
Mkoa wa kusini Pemba, unaoundwa na wilaya za Chake chake na Mkoani,
unayo majimbo tisa na wadi 16, ambapo kati ya hizo wadi tatu pekee, zinazoongozwa
na wanawake, ikiwemo Tibirinzi.
MWISHO.


.jpg)

Comments
Post a Comment