Skip to main content

AWENA SALIM KOMBO: MWANAMKE ANAEPAMBANIA UONGOZI KWENYE JIMBO LAKE

 



IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA

 

"SIKATI tamaa ipo siku nitafanikiwa lengo langu nililolikusudia kwa sababu kila kitu kimepangwa kwa muda maalumu, hivyo naamini bado wangu haujafika"

 

Sio maneno ya mtu mwengine bali ni Awena Salim Kombo mwenye umri wa miaka 50 mkaazi wa shehia ya Kangagani Wadi ya Kiuyu, Jimbo la Kojani Wilaya ya Wete Pemba.

 

Awena ni mwanamke shupavu mwenye ndoto ya kuwa kiongozi tangu akiwa kijana mdogo, na ndipo mwaka 1990 alipoamua kujiunga kwenye chama cha Mapinduzi CCM, ili kusudi apate nafasi ya kuwa kiongozi.

 

Lengo lake la kusaka uongozi ni kutaka kusaidia jamii kwenye mambo mbalimbali ikiwemo kutatua changamoto zinazowakabili.

 

"Hivi sasa baadhi ya wanajamii wenye matatizo hunifuata kutaka msaada, hivyo wakati mwengine nashindwa kutokana na hali yangu kutomudu" anaeleza.

 

Mwaka 2017 Awena alianza kupata nafasi za uongozi katika chama chake, ambapo alijiona tayari anaenda kutimiza ndoto zake alizokuwa akiziwaza mara kwa mara kwenye maisha yake.

 

Alianza kushika nafasi ya Mjumbe wa Wadi UWT, na baadae akagombea nafasi ya Katibu wa Jimbo wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) ingawa hakufanikiwa kwenye nafasi hiyo.

 

Kwa sasa Awena anashikilia nafasi ya Katibu wa Wazazi Wadi ya Kiuyu, ambapo nafasi zote hizo aligombea na kushinda.

 

"Kwa vile lengo langu ni kuwa kiongozi na kuwaletea wananchi maendeleo, sikufikia hapo bali niliendelea kugombea na kushikilia nafasi mbalimbali ndani ya chama changu," anaeleza Awena.

 

Anasema, bado hajachoka ataendelea kugombea nafasi za uongozi, ili aweze kutimiza ndoto zake za kuwasaidia wananchi wa Jimbo lake.

 

Mama huyo anashikilia nafasi mbalimbali ndani ya chama, ndipo alipoona sasa kuna haja ya kuingia kwenye vyombo vya maamuzi ili lengo lake la kuwatumikia wananchi aweze kulifikia.

 


"Nilijiona kuna nafasi nyingi nimeshikilia ndani ya chama changu, lakini nilisema kuwa bado lengo langu sijalifikia, hivyo lazima nipambane, ingawa nimeshawahi kugombea udiwani viti maalumu lakini kura hazikutosha kwa upande wangu," anasema.

 

Awena anasema ni mwiko kukata tamaa, na ilipofika mwaka 2020 hakuwa nyuma alikwenda kuchukua fomu ya kugombea uwakilishi Jimboni, ingawa hakupita kwenye kinyang'anyiro hicho tangu ngazi ya nchini.

 

Alipokwenda kuchukua fomu baadhi ya wananchi walimkebehi na kumuhisi kwamba hawezi, ingawa hakusikiliza maneno hayo na kuamua kusonga mbele.

 

Anahadithia kuwa, ilikuwa ni ngumu kuingia jimboni kugombea kutokana na wanaume kumkwaza kwa kile wanachodai kuwa, nafasi za wanawake ni viti maalumu pekee na za majimboni ni za wanaume tu.

 

"Kwa kweli maneno yao yanaweza kukuvunja moyo ikiwa hukusisimama kidete kwenye jambo hili, na niliwaambia kuwa nimeshaweka nia ya kugombea na nimeamua," anahadithia 

 

Baadhi ya wanajamii pia walikuwa na mtazamo hasi tofauti na sasa, hivyo waliona kama nahangaika na kuharibu pesa bila kujua kwamba anatarajia kitu gani kwa kile anachokipambania.

 

Aliwaeleza kuwa, hawezi kupindisha kauli ya lengo lake hasa kwa vile chama chao kinazingatia jinsia, jambo ambalo linampatia nguvu zaidi.

 

"Pia mume wangu na familia yangu inaniunga mkono kwa hiyo sikutetereka katika hili, nilikwenda kuchukua fomu, na nashukuru hata kama nimekosa nafasi lakini kila siku zinaposogea nazidi kuwa jasiri na imara," anasema Awena.

 

Katibu huyo wa Wazazi Wadi ya Kiuyu, anasema licha ya kukosa awamu zote kwa nafasi mbili za udiwani na moja ya uwakilishi, lakini hajakata tamaa na itakapofika mwaka 2030 atagombea tena kwenye jimbo lake.

 

Anaeleza kuwa, kipindi kifupi kijacho pia kutakuwa na chaguzi za ndani ya chama, hivyo nazo hatokuwa nyuma katika hilo na atagombea.

 

Mama huyo anaeleza, pindi atakaopata nafasi na kuingia kwenye chombo cha maamuzi, anaamini atapata nafasi ya kuwasilisha changamoto zinazowakabili wananchi na kuweza kutatuliwa kwa haraka.

 

Vile vile atapata fedha za kuwasaidia wananchi wake pale wanapotokezewa na tatizo ama la jamii kwa pamoja au la mtu mmoja mmoja kama anavyofanya sasa.

 

"Jamii inanipenda hasa pale wanaponiona nasaidia wenzangu kwa hali na mali, hivyo naamini nikipitishwa tu kwenye chama changu kugombea, basi naamini Jimbo nitalichukua," anaeleza.

 

Mama huyo hakushawishiwa na mtu yeyote kugombea uongozi, bali yeye mwenyewe anaupenda kutoka moyoni ili apate nafasi ya kuwasaidia wanajamii na Taifa kwa ujumla.

 

Kupitia nafasi aliyonayo kwa sasa Awena amepata faida nyingi ikiwemo kujuana na watu mbalimbali na kushirikiana nao, sambamba na kupatiwa usafiri wa pikipiki ambayo inamsaidia kutekeleza vizuri majukumu yake ya chama na Serikali.

 

"Hata jamii inanikubali sana na kuniamini, kwani panapokuwa na jambo huniweka mstari wa mbele, hivyo najivunia sana," anaeleza.

 

Mbali na uongozi wa chama anaosimamia, pia ni Mratibu wa Wanawake na Watoto wa shehia ya Kangagani na pia ni mjasiriamali wa kilimo cha chakula, mboga na matunda.

 

"Sijazoea kukaa tu bila kujishughulisha, kwa sababu hicho ninachokipata pia nasaidia wengine wanapotokezewa na shida, ingawa soko la bidhaa hizo wakati mwengine ni shida," alieleza.

 


Awena ameolewa na ana watoto kumi, ambapo amesoma skuli ya msingi Ole na kumalizia kidato cha nne katika skuli ya Sekondari Utaani Wete.

 

Mume wa Awena, Hasnuu Fakih Hassan anasema kuwa, mke wake ni mchapa kazi katika kila sekta, hivyo anaamini akipewa nafasi ya kuwatumikia wananchi basi atafanya kazi kwa juhudi zote.

 

Anaeleza kuwa, anamuunga mkono kwenye harakati zake zote za uongozi na kugombea nafasi mbalimbali, kwani ameshamuona kwamba ni mwanamke jasiri na anaweza kusimama popote kutetea haki za wananchi.

 

"Hata hapa nyumbani anasaidia sana wananchi wanapokuja na matatizo yao, hivyo atakapopata nafasi ya kuingia kwenye chombo cha maamuzi atatetea wananchi na changamoto zote zitaondoka," anasema.

 

Badria Juma Issa ni dada anaemfahamu Awena na kusema kwamba, ni mwanamke anaefaa kuwa kiongozi kwa imani yake ya kusaidia wengine hata kama alichonacho hakitoshi, hivyo wanawake kama hao ni muhimu katika maendeleo ya jamii husika.

 

Anasema, Awena anajiamini sana na ndio maana hawezi kukata tamaa kirahisi kwa sababu kama ni mtu mwengine angekuwa hagombei tena kutokana na vipindi kadhaa kukosa nafasi.

 

Ingawa kwake yeye amechukulia changamoto hiyo ni kama fursa ya kujiandaa upya katika chaguzi zijazo.

 

Katibu wa CCM Jimbo la Kojani Tamimu Ali Omar mkaazi wa Mchangamdogo anamuelezea Awena kuwa ni, mtendaji na mfuatiliaji mzuri wa masuali mbalimbali ya chama na jamii, kiasi ambacho kinampa siha ya kuwa kiongozi bora.

 

‘’Tayari ameshaanza kuonesha uwezo wake kwa kujitolea katika kusaidia wengine wenye changamoto, pia kwa vile ni mama lazima atakuwa na huruma juu ya kuwasaidia wanawake wenzake na jamii kwa ujumla,’’ anasema Katibu huyo.  

 

Mratibu wa Programu ya SWILL kutoka TAMWA Zanzibar Sabrina Ali Mwatanga anafafanua, wanaendelea kuelimisha na kuhamasisha uongozi kwa wanawake ili waingie kwa wingi katika vyombo vya maamuzi kwa ajili ya kutetea mambo yanayowahusu pamoja kuleta maendeleo kwenye majimbo yao.

 

Hiyo ina lengo la kuongeza ushiriki wao katika uongozi na siasa, kuimarisha mipango ya maendeleo jumuishi na kuweka msingi imara wa maandalizi ya uchaguzi wa mwaka 2030.

 

‘’Itakapofika mwaka 2030 tunataka tuwaone wanawake wengi wanaingia kwenye mchakato wa uchaguzi na kufanikiwa, hii itasaidia kutetea mambo yao yanayowahusu na masuala mengine ya kijamii, kwani tunawaona waliofanikiwa namna wanavyoleta maendeleo katika maeneo yao,’’ anasema.

 

Anawanasihi wanawake wote ambao wana nia ya kugombea wasivunjike moyo bali waendelee kupambana, ili kuhakikisha kwamba kunakuwa na usawa kwenye vyombo vya maamuzi.

 

Kwa mujibu wa ripoti kutoka TAMWA Zanzibar mwaka 2020-2025 wawakilishi wanawake walikuwa nane (8) sawa na asilimia 16, huku wanaume wakiwa 42 sawa na asilimia 84, ambapo idadi ya wote walikuwa 50.

 

Mwaka wa uchaguzi uliofuata wa 2025-2030 wawakilishi wote ni 50, ambapo wanawake ni wane (4) sawa na asilimia nane na wanaume ni 46 sawa na asilimia 92.

Serikali kwa kutambua umuhimu wa mwanamke, sera na sheria mbalimbali za Zanzibar zimeeleza kuhusu haki ya wanawake kushiriki katika demokrasia na uongozi.

Kifungu cha 21 (2) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kimeeleza kwamba, kila mzanzibari anayo haki na uhuru wa kushiriki kikamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomuhusu mwanamke na taifa lake.

Azimio la kimataifa juu ya haki za binadamu la mwaka 1948 ambalo ndio msingi wa haki zote za binadamu, ikiwemo haki za kiraia na kisiasa linatoa haki kwa kila mtu katika uongozi wa nchi.

                               MWISHO.

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

Vikausha damu vya mjamzito hivi hapa, umo mchele, udongo, mkaa, chaki Uwezekano wa kuzaliwa watoto wenye udumavu, utapiamlo ni mkubwa

  NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@ ‘’KILA ninapobeba mimba nimezoea kula mchele kwa wingi naweza kusamehe pilau au biriani,’’ ndio maneno ya mwanzao ya Bahati Mohamed Ali (sio jina lake halisi). Nilimfuma akiwa barazani kwake, mjini Ole wilaya ya Chake chake, pembeni yake akiwa na kibakuli cha mwazi, kwa umbali utaona amejaza chakula aina ya pepe, kumbe ni mchele wa Mbeya. Hujichotea kidogo kidogo na kuushindilia mdomoni mwake, huku akiendela kupiga storia na wenzake, bila ya kujali kuwa ujauzito alionayo na mchele huo hauna mwisho mwema. Kawaida yake akiwa mjamzito, kila anapoamka asubuhi anaroweka mchele upatao robo kilo hivi…na baada ya kumaliza kupika, yeye huchukua mchele wake kutafuna (kula). Wakati mwenza wake na watoto wao, wanakula chakula cha mchana, Bahati yeye hukaa pembeni na kibakuli chake cha mchele akiendelea kubahatisha afya yake. ‘’Mimba nyengine hupenda sana kutafuna mchele wa Mbea na nyengine hupenda mchele wa mapembe, kwa kweli huwa nina hamu (kileo), kwan...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...