IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA
BIZUME Haji Zume,
mkaazi wa shehia ya Kinyasini Jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, ni miongoni
mwa wanawake mashuhuri wenye nia ya kufika mbali kiuongozi.
Ingawa matarajio yake yeye mpaka sasa, ni kugombea nafasi za
ndani ya chama tu kuanzia tawi hadi Taifa, na sio Jimboni kwa kile anachodai
kwamba ni lazima kwanza ushikilie nafasi hizo ili uwe imara zaidi.
Atapojijenga zaidi kwa nafasi za ndani ya chama, hapo ndipo
ataanza kutafuta njia ya kusonga mbele kwani, huwezi tu kufika huko ikiwa
hukuanza nafasi za chini.
"Nataka na mimi nifikie kugombea Uwakilishi na Ubunge
katika Jimbo lakini, huwezi kufika huko ikiwa bado kwenye chama hujashika
nafasi yeyote," anasema Bizume.
Lengo la mama huyo kugombea nafasi hizo, ni kuhakikisha anajijengea
uwezo zaidi wa kiuongozi, kujenga mahusiano mazuri na wanachama, pamoja na
kukubalika kwenye chama chake.
Anasema, hiyo itampa fursa ya kusonga mbele kiuongozi kuanzia tawi
hadi Taifa, na hatimae kupata nafasi ya kuwasaidia wananchi kuwatatulia
changamoto zinazowakabili.
"Hizi hizi nafasi za kwenye chama, ukifika ngazi za juu
unapata fursa ya kuingia kwenye vyombo vya maamuzi, hivyo nitawatetea wananchi,
ili kuhakikisha matatizo yanaondoka katika majimbo yote kwenye mkoa wetu,"
anaeleza.
Bizume anaeleza, nafasi za Ubunge na Uwakilishi huwezi kugombea
ikiwa hujaanza kwenye chama na kujulikana, ndio maana wanaanzia ngazi hadi
ngazi mpaka wafikie huko na kuapa kwamba hatorudi nyuma.
Anasema, kwanza ni wakati wa kukichangia chama kwa kufanya
shughuli za chama na kuwa mzalendo, ndipo zitakuja tu nafasi nyengine na sio
kukurupuka tu.
"Naendelea kujiimarisha kwenye chama change, ili nipate
kuwa mzuri katika kupambana na harakati za chama cha Mapinduzi, na kuna siku
naamini nitafanikiwa," anafafanua Bizume.
Kutokana na uwanaharakati wake kwenye chama na Serikali, watu
wengi kwenye jamii, husema mama huyo anaweza kusimamia na ana moyo wa kujitolea.
Hivyo linapotokea jambo kwenye jamii, wananchi wanapenda achukue
yeye nafasi ya kuwa kiongozi kwani hata kwenye suala la michango yupo mstari wa
mbele, kufuatilia na kusimamia.
Bizume anasema, nafasi anazokamata kwa sasa, zote ni za
kinyang'anyiro cha kugombea na anafanikiwa kupata, ingawa bado ana safari ndefu
ya kufika ngazi ya Taifa.
Alijiunga kwenye chama cha Mapinduzi CCM mwaka 1992, ingawa
tangu miaka hiyo, hakuwa nyuma katika kupambana na kuwa mwanaharakati bora.
Baada ya kujiunga na chama, Bizume hakuridhika kukaa tu
nyumbani, bali alishiriki shughuli mbalimbali za chama, hivyo ilikuwa
anaposimama kiongozi kuzungumza na yeye anapata hamasa ya kuwa kiongozi.
"Ilikuwa nasema kwa nini na mimi nisigombee wakati naweza
kuzungumza, ndipo nilipoanza kuingia kwenye mchakato na nashkuru nimeshaanza
kufanikiwa katika ngazi za chini," anaeleza.
Bizume alianza kuwa Mjumbe wa Jumuiya ya UWT tawi la Kinyasini na
mwaka 2017, aligombea na kuwa Mwenyekiti wa UWT Jimbo la Pandani mpaka 2022
alipogombea nafasi nyengine.
Anasema, aligombea nafasi nyingi ingawa kura hazikutosha na
kubahatika kuwa Mjumbe wa Kamati Tekelezaji Tawi la Kinyasini UWT, ambapo pia
ni Mjumbe wa siasa Tawi hilo.
"Kwa sasa ni Mjumbe wa Kamati Tekelezaji Jimbo la Gando,
Mjumbe wa Kamati Tekelezaji wilaya ya Wete, lakini pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu
CCM wilaya ya Wete," anaeleza.
"Hivyo unaona zile harakati zangu ninazopanda ngazi hadi
ngazi juu ya kuimarisha masuala ya chama, naamini ndizo zitakazonifikisha
ninapopataka," anasema.
Lakini pia mama huyo amewahi kugombea nafasi ya Wadi UWT na alipitwa
kwa kura moja, ingawa hakuishia hapo aligombea nafasi nne za wajumbe wanne wa
Jimbo, ingawa nako kura pia hazikutosha.
Bizume aligombea Baraza kuu, aligombea Kamati Kuu ingawa pia
kura hazikutosha, na kusema bado hajakata tamaa kwani mwaka 2027, atagombea
kuanzia Tawi mpaka Taifa ndani ya chama bila kurudi nyuma.
Anasema, kutokana na hali ilivyo kwenye Dunia ya sasa,
utandawazi, unawaathiri sana vijana wao, hivyo atatumia fursa ya uongozi atakayoipata
kuhakikisha wanakuwa na muelekeo nzuri wa maisha yao.
Kwa sababu kwenye chama kuna nafasi ya malezi, itikadi na
uenezi, ambayo inazungumzia suala la malezi kwa watoto na wapi waelekee katika
mustakbali mzuri wa malezi yao.
Vilevile anafafanua, kuna mambo yanayoweza kumtayarisha kijana
ili aweze kujua wapi aelekee na kitu gani anatakiwa atafute kwa mustakbali bora
wa maisha ya baadae.
"Hivyo nikifanikiwa kuwa kiongozi wa juu nitawasaidia
vijana katika masuala yanayowahusu wao, watoto na wanawake, ili kuhakikisha
tunakuwa na Taifa lenye wananchi wanaofuata maadili mema," anafafanua.
Changamoto zilizomkumba Bizume wakati wa kugombea anasema, ni pale
mwanzo tu alipokuwa hajajulikana baada ya Wadi yao kuhamishwa wilaya ya
Micheweni na kwenda Wete.
Lakini kutokana na uchangamfu wake, wanachama wameshaanza
kumjua, viongozi wote wanashirikiana vizuri, hivyo anaamini atafika
anapopatarajia.
"Pia nimepata mafanikio ya kujuana na watu mbalimbali kwani
napenda sana uhamasishaji na kujitolea, naonesha uzalendo na kukipenda chama
changu," anafafanua.
Mbali na nafasi anazoziongoza kwenye chama, Bizume pia ni Afisa
Maendeleo ya jamii wilaya ya Micheweni, na amekuwa akipambana na udhalilishaji,
kuhamasisha mambo ya kimaendeleo kwenye jamii, malezi bora na ushirikiano.
Kwa upande huo, anawasaidia wanajamii kuwapa elimu, ushauri,
mapendekezo, maelekezo na wakati mwengine hata kuwapa misaada kwa mujibu wa
uwezo wake.
Bizume ameolewa na ana watoto sita, ambapo amepata elimu ya
cheti katika masuala ya Maendeleo ya vijana.
Mtoto wake Bizume, Fatma Omar Juma mkaazi wa Kinyasini Wete
anasema, mama yake ni mwanaharakati kwa muda mrefu sasa, kwenye chama, serikali
na hata kwenye jamii.
‘’Hapa tunapoishi likifanyika jambo yeye ndio anakuwa mstari wa
mbele na wanajamii wanamuani sana, kwani anasimamia majukumu vizuri, hivyo kazi
ya uongozi anaiweza,’’ anaeleza.
Raiye Amour Othman mkaazi wa Kinyasini Pemba ambae ni Mjumbe wa
Kamati Tekelezaji wa UWT Mkoa wa Kaskazini Pemba anasema, Bizume ni mwanamke
anaejali, kuthamini na wala hamdharau yeyote katika harakati zake za chama.
‘’Anaweza kuongoza na kushughulikia sana mambo ya uongozi kwenye
chama, Serikali na jamii, na ni mwanamke anaekubali kukosolewa, hivyo yupo
tayari kujifunza mambo mbalimbali,’’ anaeleza.
Katibu wa CCM Jimbo la Gando Panya Yahya Ali anasema, Bizume ni
mchapa kazi na anaependa kujitolea popote katika kuhakikisha kazi zinaenda
vizuri.
‘’Bizume ni kiongozi mzuri ambae sio mvivu na ni mwenye kupenda
maendeleo, hivyo atakapofika mbali kiuongozi, naamini ataisaidia jamii katika
kufikia maendeleo tunayoyataka katika nchi yetu,’’ anamsifia.
Mratibu wa Programu ya SWILL kutoka TAMWA Zanzibar Sabrina Ali
Mwatanga anafafanua, wanaendelea kuelimisha na kuhamasisha uongozi kwa wanawake
ili waingie kwa wingi katika vyombo vya maamuzi na kusimamia mambo yanayowahusu
na kuiletea maendeleo jamii.
Hiyo ina lengo la kuongeza ushiriki wao katika uongozi na siasa,
kuimarisha mipango ya maendeleo jumuishi na kuweka msingi imara wa maandalizi
ya uchaguzi wa mwaka 2030.
‘’Itakapofika mwaka 2030 tunataka tuwaone wanawake wengi wanaingia
kwenye mchakato wa uchaguzi na kufanikiwa, hii itasaidia kutetea mambo yao
yanayowahusu na masuala mengine ya kijamii ,’’ anasema.
Mwatanga anawanasihi wanawake wote ambao wana nia ya kugombea nafasi
mbalimbali za uongozi, wasivunjike moyo, bali waendelee kupambana, ili kuona
kwamba kunakuwa na usawa kwenye vyombo vya maamuzi.
Mkurugenzi wa Jumuiya ya Utetezi wa Mazingira na Jinsia Pemba ‘PEGAO’ Hafidh Abdi Said, anasema wanaamini kwamba lengo lao la kufikia 50 kwa 50 katika safu ya uongozi litafanikiwa, kwani elimu inayotolewa itaendelea kuwajengea ukakamavu na kujiamini.
Serikali kwa kutambua umuhimu
wa mwanamke, sera na sheria mbalimbali za Zanzibar zimeeleza kuhusu haki ya
wanawake kushiriki katika demokrasia na uongozi.
Kifungu cha 21 (2) cha Katiba
ya Zanzibar ya mwaka 1984 kimeeleza kwamba, kila mzanzibari anayo haki na uhuru
wa kushiriki kikamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomuhusu
mwanamke na taifa lake.
Azimio la kimataifa juu ya haki
za binadamu la mwaka 1948 ambalo ndio msingi wa haki zote za binadamu, ikiwemo
haki za kiraia na kisiasa linatoa haki kwa kila mtu katika uongozi wa nchi.
MWISHO.



Comments
Post a Comment