NA SULEIMAN SAID, PEMBA
“Fikiria mtoto anapokuwa tumboni, macho yake bado yamefumba,’’inafahamika.
Ingawa ndani ya kichwa chake kuna mabilioni
ya seli zilizo tayari kumsaidia kujifunza.
Cha kushangaza ni
kwamba, msingi wa seli hizo, uliwekwa wiki chache, tu baada ya mama kutunga
mimba.
Lakini cha
kujiuliza je, unajua kipindi hiki ndicho kinachoweka msingi muhimu wa maendeleo
yake ya baadaye?’’.
Mtaalamu
wa eneo hilo hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani, anasema wazazi wengi huamini
kuwa elimu ya mtoto huanza siku ya kwanza, anapoingia darasani, lakini ukweli
wa kisayansi ni kwamba kujifunza huanza sambamba na safari ya ukuaji wa ubongo.
Tena
inafahamika kuwa ni, wiki chache baada ya mimba kutungwa, na kadiri ujauzito
unavyokuwa mtoto huanza pia kuitikia na kujifunza kutokana na mazingira yake
akiwa tumboni.
Anasema kuanzia takribani wiki ya tatu, baada ya
mimba kutungwa, ubongo wa mtoto huanza kukua kwa kasi.
Katika kipindi hiki, mabilioni ya miunganiko ya seli
za ubongo, huundwa na kuweka msingi wa uwezo wa mtoto wa kufikiri, kujifunza,
kuwasiliana, kutatua changamoto, kudhibiti hisia.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Ulimwenguni na ‘WHO’
na UNICEF kuhusu malezi na makuzi ya mtoto, hasa kipindi kinachoanzia ujauzito,
hadi mtoto anapofikisha miaka mitatu, takribani asilimia 80 ya ukuaji wa ubongo
hutokea.
Anaeleza kuwa, hili ina maana kwamba, kila siku ya
ujauzito, ni muda muafaka wa kumuandaa mtoto kwa maisha ya baadaye.
Kila
familia inaweza kuchagua makuzi ya ubongo kwa mtoto wao
Anaeleza kuwa, fikiria familia mbili katika kijiji
kimoja, mfano cha Mtambile Pemba au Matemwe Unguja, na hata watoto wenye vina
sawa vya afaya, wanaweza kukua tofauti.
Ndio maana katika
familia ya kwanza, mama mjamzito hupata chakula chenye lishe, huhudhuria
kliniki/kituo cha afya mara kwa mara, hupata muda wa kupumzika na baba au
familia humtia moyo na kumsaidia kazi zake.
Katika familia ya pili, mama hubeba mizigo mizito,
hukosa chakula chenye virutubisho, hahudhurii kliniki na hukabiliwa na migogoro
ya kindoa na kifamilia.
Anaeleza kuwa, ingawa watoto hawa wanaweza kuzaliwa
siku moja, makuzi yao ya ubongo yanaweza kuwa tofauti.
Kumbe hilo ni kutokana na mazingira waliyokulia
kabla hata ya kuzaliwa, ambapo kitaalamy hiyo ndiyo sababu wataalamu wa
maendeleo ya mtoto hutaka kuandaliwa tangu tumboni.
Lishe
bora kwa mjamzito
Mtaalamuy huyo anasema, mjamzito anapopata mlo
kamili, si mwili wake pekee unaonufaika, bali hata ubongo wa mtoto anayekua
tumboni.
Anasema kwa bahati nzuri, Zanzibar ina vyakula vingi
vinavyoweza kusaidi ukuaji wa ubongo wa mtoto, kama samaki, dagaa, mayai.
Vyakula vingine ambavyo sio adimu ni maharage, kunde,
ufuta, njugu, mboga za majani, nafaka, papai, embe, ndizi, chungwa na
parachichi.
Ndio maana dk. Fadhila kupitia mradi wa makuzi na
malezi ya watoto amesisitiza kuwa, lishe bora haihitaji vyakula vya gharama,
kama wingi wanavyofikiria.
Utulivu
wa mjamzito na faida ya mtoto aliyetumboni
Mama anayepitia msongo mkubwa wa mawazo, kwa muda
mrefu, anaweza kupata athari zinazoweza kuathiri ukuaji wa mtoto.
Dk. Fadhila, anasema tafiti zinaonyesha kuwa
mazingira salama, yenye upendo na msaada wa familia, huchangia ukuaji wa ubongo
wa mtoto tangu akiwa tumboni.
Akaeleza kuwa, katika jamii mara nyingi, ujauzito
huonekana kuwa jukumu la mama pekee, na kusahauliwa baba kwamba nae ana mchango
sio gtu wa ukuaji, bali hata mtoto kuzaliwa hai.
Hivi karibuni
akizungumza kwenye moja ya mafunzo ya ukuaji wa mtoto, Afisa Ustawi wa jamii na
hifadhi ya mtoto Chakechake Rashid Said Nassor, anasema baba anapomuhimiza mama
kwenda kliniki, ni jambo jema.
Eneo wajibu wa baba ni kuzungumza na mtoto akiwa
tumboni, kusaidia kazi za nyumbani na kuwa karibu na mama ambapo yote hayo, hujenga
furaha na kuepusga msongo wa mawazo.
‘’Kwa mfano, baba anayechukua dakika chache kila
jioni, kuzungumza na mke wake, kuuliza hali yake na kupanga pamoja mahitaji ya
ujauzito, huchangia kujenga mazingira yenye utulivu na makuzi bora ya ubongo wa
mtoto,’’anasema.
Kila
ziara ya kliniki ni fursa ya kulinda afya ya mama na ukuzaji wa ubongo wa mtoto
Wapo wanaoamini kuwa, kliniki ni sehemu ya kujifungulia
tu, jambo ambalo sio sahihi, ukweli ni kwamba, ni eneo la ushauri na mafunzo ya
kuchochea makuzi ya ubongo wa mtoto.
Kliniki hufanya uchunguzi wa makuzi na afya ya
mtoto, mama hupatiwa virutubisho muhimu, chanjo na elimu ya malezi.
Huduma hizi husaidia kugundua changamoto mapema na
kulinda afya ya mama na mtoto, kwa ajili ya kupata watoto wenye afya njema.
Haya
hapa mambo matano ya kukumbuka
Kwenye
ukuaji wa ubongo wa mtoto, huanza kukua wiki chache baada ya mimba kutungwa, jingine
ni kipindi cha ujauzito hadi miaka mitatu ni muhimu zaidi kwa ukuaji wa ubongo.
Jambo
la tatu ni lishe bora na mahudhurio ya kliniki huchangia ukuaji mzuri wa ubongo
wa mtoto, huku eneo jingine ni msaada wa baba na familia hupunguza msongo wa
mawazo kwa mama na malezi bora huanza kabla mtoto hajazaliwa.
Hitimisho
Ubongo wa mtoto hauanzi kujengwa siku ya kwanza ya
skuli; huanza kujengwa tangu tumboni.
Kila mlo wenye lishe, kila ziara ya kliniki, na kila
neno la faraja ni uwekezaji katika kizazi kijacho.
Kuwekeza katika mama mjamzito leo ni kuweka jiwe la
msingi la viongozi, walimu, na wabunifu wa kesho.
mwisho





Comments
Post a Comment