NA
MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
MAJI
ni rasilimali muhimu kwa maisha ya viumbe wote wanaoishi.
Kwa mujibu wa mitandao ya kijamii lita trillion 11 hadi
12.5 za maji, hutumika kwa siku duniani kote.
Itambulike maendeleo yote duniani, hutegemea
upatikanaji huduma muhimu za kijamii, ikiwemo maji safi na salama.
Mitandao ya kijamii imeripoti sekta ya kilimo pekee
inachukua karibu lita trillion 8.0 za maji kwa siku, ikifuatwa na ya viwanda inayokisiwa
kutumia lita trillion 2.3, huku matumizi ya nyumbani yakikisiwa kuchukua lita
trillion 1.2 duniani kote.
Ndio maana, serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huchukua
juhudi za makusudi, kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama,
kila siku.
Miongoni mwa juhudi hizo ni utekelezaji mradi wa
kimkakati, wa ujenzi wa matangi makubwa ya kuhifadhia maji, katika maeneo ya
mikoa miwili ya kisiwa cha Pemba.
Ofisa Mdhamini Ofisi ya Rais Pemba Shuweikha Abdallah
Omar anasema, mbali na kusogeza huduma ya maji kwa wananchi, mradi huo unalenga
kuchochea maendeleo ya kiuchumi.
“Mradi huu ni miongoni mwa juhudi za kuifungua Pemba
kiuchumi, pamoja na matumizi ya kawaida huduma ya maji ni kipengele muhimu,
katika uwekezaji wa miradi ya maendeleo,” anaeleza.
Hivyo serikali ya awamu ya nane, chini ya Dk. Hussein
Ali Mwinyi, imeweka nguvu kubwa katika ujenzi wa matangi makubwa ya maji,
ilioamini yatasaidia kutatua changamoto ya upatikanji huduma hii.
UJENZI
WA MIUNDOMBINU YA MAJI
Hapa Ofisa Mdhamini wizara ya Maji, Nishati na Madini
Pemba Mhandisi Suleiman Hamad Omar anasema, mwaka wa fedha wa 2025/2026, wizara imejenga matangi
manne makubwa ya maji (zinkAlminium) yenye uwezo wa kuhuifadhi maji mengi.
Anaeleza kila tangi lina uwezo wa kuhifadhi lita milioni
1, za maji kwa wakati mmoja, hatua inayofanya mradi huo kuwa miongoni mwa mradi
mkubwa wa miundombinu ya maji kisiwani Pemba.
Mhandisi Suleiman anasema, serikali haikukurupuka bali
ilifanya utafiti wa kina, kabla ya kuanza ujenzi wa mradi huo.
“Matangi haya yamejengwa kwa vigezo vya kimataifa,
yakiwa na uwezo wa kuhimili mabadiliko yoyote ya hali ya hewa, kwa kipindi
kisichopungua miaka 10, bila kufanyiwa matengenezo makubwa,” anafafanua.
Anasisitiza ubora huu ni kuhakikisha fedha za walipa
kodi zimetumika kwa njia endelevu, na yenye tija ya muda mrefu, huku ujenzi huo
ukizingatia maeneo yenye uhitaji mkubwa wa huduma.
Anafafanua kuwa, mkoa wa kaskazini Pemba, Matangi
mawili yamejengwa katika shehia za Mtambwe Kaskazini na Mtambwe Kusini.
Ambapo tangi la Mtambwe Kaskazini, linatarajiwa
kuhudumia wananchi zaidi ya 12,000, huku lile la Mtambwe Kusini, likitarajiwa
kuwahudumia zaidi ya wananchi 10,000.
Na Matangi mawili yaliobakia yamejengwa katika meneo ya Kengeja wilaya ya
Mkoani na kwa upande wa wilaya ya Wete lipo kijiji cha Raha.
Ujenzi huu unalenga kusawazisha huduma pande zote za
kisiwa, ili kusiwe na eneo linalobaki nyuma, na ujenzi wa matangi haya
umepangiwa shilingi zaidi ya billion 15.77.
“Mradi huu unatekelezwa na serikali ya awamu ya nane,
inayoongozwa na Dk. Mwinyi, unalenga kuhakikisha upatikanaji maji katika maeneo
yote, hadi kukamilika kwake utagharimu shilling billion 15.77,’’anaeleza.
Kubwa, akawataka wananchi, kuyatumia maji hayo, kwanza
kwa kukuza pato lao, kwani ndio miongoni mwa azma ya Dk. Mwinyi.
Hakuacha kuwakumbusha wananchi, kwamba ulinzi wa miundombinu
yake, wa kwanza ni wananchi wa maeneo husika, wakiongozwa na weingine.
UIMARISHAJI
VYANZO VYA ASILI NA MIUNDOMBINU YA USAMBAZAJI
Ujenzi wa matangi makubwa hauna maana, ikiwa hakuna
vyanzo vya uhakika vya kujaza maji hayo.
Mhandisi Suleiman anabainisha kuwa, sambamba na ujenzi
wa matangi, serikali imeweka nguvu kubwa katika kuboresha na kuongeza vyanzo
vya asili vya maji, ikiwa ni pamoja na kuchimba na kukarabati visima.
Maana anasema, lengo ni kuhakikisha matangi yanapokea
maji ya kutosha na kwa muendelezo bila kukatika katika, kama ilivyo hapo zamani.
Jitihada hazikuishia hapo, kwani wizara pia, inafanya
ukaguzi wa kina wa mfumo mzima wa usambazaji wa nuduma ya maji uliopo.
"Tumeimarisha vyanzo vya maji na tunapitia upya miundombinu
iliopo, ili kujiridhisha kwamba itafaa au kuna uhitaji wa kubadilisha,”
anaeleza.
Haya yote yanalenga kuhakikisha udhibiti wa maji hayo
ili yawafikie wananchi yakiwa safi, salama na mengi pale yatakapoanza rasmi matangi,
kutumika.
Kazi hii ya kutathmini upya mabomba na miundombinu ya
zamani, itahakikisha maji yanayotoka kwenye matangi hayo mapya, yanawafikia wananchi
bila ya vikwazo.
JINSI
WANANCHI WATAKAVYO FAIDIKA
Mradi huo upo katika hatua za kutumika, huku matunda
yake yakitarajiwa kuwafaidisha wananchi wengi.
Mwanaid Juma Khamis wa Mtabwe kusini wilaya ya Wete
anasema, ile tabu ya kutembea umbali mrefu na kutumia saa nyingi kutafuta maji,
inaenda kumalizika.
Bakar Said Bakkar wa Mtambwe Kaskazini, anamatarajio kua. mradi huo utafungua milango mipya ya
fursa za kiuchumi, hususan katika sekta ya kilimo.
“Mbali na matumizi ya kawaida, mradi huu utakuza sekta
ya kilimo cha umwagiliaji, ambayo kwa takriban miaka miaka minne iliyopita,
ilikwama kutokana na tabu ya maji,” anaeleza.
Akikagua mradi wa ulazaji mabomba ya Maji Kengeja wilaya
ya Mkoani Pemba, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdullah, alisisitiza
kuwa serikali haitaishia hapo.
“Mpango uliopo ni kuendelea kujenga matangi mengine ya
aina hio, katika maeneo kadhaa, yenye shida ya huduma ya maji safi na salama,”
anasisitiza.
Dira hii inaungana kikamilifu na Mipango ya Maendeleo
ya Zanzibar, pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa, hasa
lengo namba sita, linalotaka kila mtu apate maji safi na salama, ifikapo mwaka
2030.
Kwani hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maji, Nnishati na Madini
ya mwaka 2026/2027, inaeleza kiwango cha uzalishaji maji, kimeongezeka kutoka
wastani wa lita million 211 na kufikia lita milioni 218 kwa siku.
Kiasi hicho ni sawa
na asilimia 86.5 ya mahitaji kwa mwaka 2025/2026, huku mahitaji halisi yakiwa
ni lita million 252 kwa siku, hali inayopelekea kuwepo kwa upungufu wa wastani
wa lita million 34 kwa Zanzibar.
Katika kuungamkono juhudi hizi wananchi wanalojukumu
la kulinda miundombinu hii dhidi ya uharibifu wa makusudi au wizi.
Kwani Matangi na mabomba haya ni mali ya umma iliyowekezwa
kwa manufaa ya umma.
Hivyo ni lazima jamii ishirikiane na serikali kulinda
mazingira yanayozunguka vyanzo vya maji na visima ili kuzuia kukauka kwa maji
ya ardhini kutokana na ukataji miti au shughuli zisizo endelevu za kibinadamu.
Mradi wa ujenzi wa matangi manne ya maji yenye uwezo
wa kuhifadhi lita milioni moja kila moja kisiwani Pemba, ni ushahidi wa vitendo wa dhamira ya Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwaletea wananchi wake maendeleo ya kweli.
MWISHO
Comments
Post a Comment