NA
SAIDA ALI, PEMBA@@@@
UDHALILISHAJI
katika vyombo vya usafiri ni pamoja na ukatili wa kijinsia, inayoashiria uvunjifu
wa haki za binaadamu.
Kwa wenzetu wenye ulemavu,
wao wamekuwa nambari moja kudhalilishwa, wakati wanapokwenda ama kurudi kwenye
mipango yao ya maisha.
Hali hiyo hujumuisha kuguswa mwili bila ridhaa,
matusi, kauli za kubaguliwa au kulazimishwa kukaa katika mazingira yanayoshusha
heshima na utu wao.
Mkurugenzi wa Jumuiya ya watu wenye ulemavu Juma
Kombo Hija Pemba anasema, vyombo vya usafiri havipo rafiki kwao.
Anasema ukiangalia
Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimeridhia mikataba mbalimbali ya
kimataifa, inayolenga kuweka mazingira rafiki kwa watu wenye ulemavu, pamoja
kusimamia haki zao.
Katika kuweka mazingira mazuri ni pamoja kusimamia
haki zao na ujumuishwaji katika vyombo vya usafiri, hususana watu wenye ulemavu
wa viungo.
Anasema yapo matukio matatu yaliyoripotiwa kwa mwezi
Juni na Jualai mwaka huu, katika jumuiya hiyo amabapo mtu mmoja mwenye ulemavu
wa viungo, alilipishwa nauli yeye pamoja na kiti mwendo chake.
Yupo abiria mmoja hajachukuliwa kisa dereva kuona
kupotezewa muda na ipo kesi moja mtu mwenye ulemavu, amepakiwa ila kigari chake
kimeachwa chini siku hiyo.
Mwinyi Hamad Othman ni mkaazi wa Majenzi wilaya ya
Micheweni mwenye ulemavu, anasema, udhalilishaji wanaoupata kwa kuachwa na
kutochukuliwa, hususan kwa daladala, ni sehemu ya udhalilishaji.
"Makonda na madereva wamekuwa wakitudhalilisha
kwa kutudharau na kutuacha tunapokuwa njiani tunaposimamisha daladala, hawatupakii
maana wanajua mpaka watubebe, watupandishe na wanaona tunawapotezea muda,’’anasema.
Faudhia Bakari Omar anasema, udhalilishaji wanaupata
kwenye vyombo vya usafiri wa umma ni pamoja na kushikwa shikwa ovyo kwa kuwakamata
baadhi ya maeneo na siyo rasmi.
Anasema wanataka wapande wenyewe kutokana na hali
wanashindwa hupelekea mpaka kubebwa na mazingira hayapo rafiki, hasa kwa gari aina
ya dyna.
Mtumwa Khamis Kombo anasema, wakati mwengine
hukutana na madereva na makonda, huwalipisha wao wenyewao na vigari vyao.
‘’Kwa kiasi fulani, udhalilishaji tunaupata maana hutuambia
tulipe nauli yetu na vigari nyetu, mbona wenye miguu yao hawalipishi,
miguu,’’anahoji.
MIONGOZO
INASEMAJE
Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha 12 (1) kinasisitiza kuwa, ‘watu wote ni sawa na wanayo haki, bila ya
ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria’.
Sheria ya Watu wenye Ulemavu Nambari 8 ya mwaka 2022
kifungu cha 30 (1) kinakubali kuwa, ‘watu wenye ulemavu hawatobaguliwa na
kudhalilishwa kwa namna yoyote na katika ngazi zote kutokana na ulemavu wake’.
Na katika kifungu cha 2, kimfafanua kuwa, ‘Baraza
litaanzisha program mbalimbali kuzuwia watu wenye ulemavu kubaguliwa au
kudhalilishwa ikijumuisha kuitwa majina yasiyofaa, kudharauliwa, kukejeliwa na kutumiwa
vibaya’.
Azimio la Ulimwengu juu ya Haki za Binaadamu Toleo
maalumu la kuadhimisha miaka 60 ya mwaka 1948 mpaka 2008 katika kifungu cha 5 mtu yoyote asiteswe,
asidharauliwe kutendewa kinyama au kikatili.
Na katika kifungu cha 7 kikafahamisha mbele ya
sheria watu wote ni sawa na wanastahili haki sawa za kulindwa kutokana na
ubaguzi wowote unaoweza kuvunja.
Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu wenye Ulemavu
wa mwaka 2006, Ibara yake ya 15 kifungu cha 1 kinsisitiza kuwa, ‘hapana mtu atakayewekwa
katika hali ya mateso au udhalimu, kutendewa au kuadhibiwa kinyume cha
ubinadamu, kiudhalilishaji au kikatili kwa namna yoyote ile’.
Na katika kifungu cha 2, kikeleza kuwa, nchi
wanachama zitachukua hatua za kisheria, kijamii, kielimu ili kuwalinda watu
wenye ulemavu, katika misingi ya usawa na watu wengine, ili wasiteswe,
wasifanyiwe udhalimu, kudhalilishwa.
BARAZA
NA JUMUIYA ZA WATU WENYE ULEMAVU ZINASEMAJE
Mashavu Juma Mabrouk ni Mratibu wa Baraza la Taifa
la Watu Wenye Ulemavu Pemba anasema, vyombo vya usafiri, havipo rafiki kwa watu
wenye ulemavu.
Anasema malalamiko huwa anayapata kwa watu wa kundi
hilo, ikiwemo kuachwa wanaposimamisha gari pamoja na kuvunjiwa viti vyao
mwendo.
‘’Mila, dini na taratibu haiwezekani mwanammke
kubebwa na mwanamme, ila hapana jinsi na watu wenye ulemavu hukutana na
viashiria pamoja na udhalilishaji,’’anasema.
Hidaya Mjaka Ali Msimamizi wa huduma za marekebisho
kwa watoto wenye ulemavu Pemba anasema, udhalilishaji wa kufanyiwa kitendo
kwenye vyombo vya usafiri, vimepungua isipokuwa vyombo havipo rafiki kwao.
Kumbe zipo badhi ya nchi kuna vyombo vya usafiri
vipo rafiki kwa watu wenye ulemavu wa viungo, huenda safari zao bila kupata
changamoto na viashiria vya udhalilishaji.
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania
Zanzibar TAMWA kupitia Afisa Programu wa kupambana na udhalilishaji Asia Hakim,
ametahadharisha juu ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji kwa wenye ulemavu.
Katika kupunguza athari hizo, TAMW imewajengea uwezo
waandishi wa habari, kuripoti matukio ya udhalilishaji hasa maeneo yasiopewa
kipaumbele, ikiwemo kwenye vyombo vya usafiri.
‘’Tunao mradi wa ‘Tunaweza Pamoja’
unaotekelezwa na UN-Women kwa kushirikiana na TAMWA Zanzibar, hasa kwa wialaya
za Wete na Micheweni,’’anafafanua.
SERIKALI
KUU INAFANYAJE
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi akifungua Ijitimai ya Kimataifa Kidoti,
anasema vitendo hivyo vinatia aibu jamii na inaenda kinyume na maamrisho ya
dini.
Anasema lazima jamii ishirikiane kutokomeza vitendo
hivyo, kwa kuchukua na kutoa ushirikiano kwa vyombo vya sheria.
Anasema kupitia njia hiyo itaweza kuandaa jamii
ambayo itapiga vita mambo yote yanayosababishwa na mmongonyoko wa maadili
katika jamii ikiwemo vitendo vya udhalilishaji
Akiwasilisha bajeti ya wizara ya Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto ya mwaka 2026/2027, Waziri wa wizara hiyo, Athanas Paul anasema, wizara itahakikisha kuimarisha
uratibu wa ufikiwaji wa usawa wa kijinsia na kupambana na vitendo vya udhalilishaji.
Akasema katika kupunguza wimbi hilo, wizara kwa
kushirikiana na taasisi mbalimbali, inaendelea kutumia mbinu tofauti
kukabiliana na vitendo hivyo.
‘’Wizara inaendelea kuweka mikakati mbalimbali inayolenga
kutatua na kuratibu, kusimamia na kutekeleza Mpango Kazi wa Pili wa Kitaifa wa
Kupambana na Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji wa wanawake na atoto,’’
anaelezea.
Hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha
mwaka 2025/2026 ya makamo wa kwanza wa rais iliyosomwa Harusi Said Suleimanam
inasema imendelea kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kubadili tabia kwa
kuachana na tabia hatarishi.
Kuwajengea uelewa watu wenye ulemavu na jamii kuhusu
masuala ya watu wenye ulemavu na kuendeleza mapambano dhidi ya udhalilishaji.
MKUU WA VYOMBO VYA MOTO ANALIPI
Mkuu wa waendesha bodaboda wilaya ya Micheweni Juma
Khamis Nassuha anasema, zipo sheria ndogo ndogo na kubwa na ipo katiba ya
Jumuiya yao, ambapo hayo yote yanapigwa vita.
Nae dereva wa
gari ya Wete- Chake chake Abdalla Ali Akida, anakiri kuwa baadhi yao, huwaacha
watu wenye ulemavu, ingawa ni kutothamini tu utu wao.
‘’Mimi huwasikubali kuwaacha, labda iwe gari
imeshajaa, hapo huwawashia taa na kuwapita,’’anasema.
Haida Juma Jabu, kondakta wa gari ya Micheweni-
Chakechake, anasema hajawahi kuwaacha watu wenye ulemavu wala kuwalipishia viti
vyao mwendo.
‘’Ni kweli tabia zetu sisi makondakta na madereva
tunatofautiana na sikatai, kwamba wapo wenzetu wanawaacha, lakini mimi
huwabeba,’’anasema.
NINI KIFANYIKE
Fatma Mkaha Sharifu anasema ni serikali kuwasaidia, ili kuepukana na
changamoto hiyo, ikiwemo kuwepo kwa adhabu kali kwa wanaowaripoti.
Mashavu Juma Mabrouk, anasema elimu iendelee kutolewa
kwa maderava, makondakta na watu wenye ulemavu, ili mwafaka upatikane.
TAKWIMU
Kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2023
mpaka 2025 Zanzibar iliripoti matukio 609 ya ukatili na udhalilishaji wa
kijinsia kwa wanawake ikihusishwa matukio ya kubakwa, kuingiliwa kinyume na
maumbile, kutoroshwa, shambulio la aibu kukashifiwa na shambulio.
Ikiwa mwaka 2023 matukio yalikuwa 236 ya ukatili na udhalilishaji wa
kijinsia kwa waathirika wanawake sawa na asilimia 12.0 na kwa mwaka 2025
yalikuwa 211 sawa na asilimia 11.7 na mwaka 2025 yalikuwa162 sawa na
asilimia 13.2.
Na katika mwaka 2023 hadi 2025 matukio ya kubaka
yaliyoripotiwa yalikuwa 234 kwa
wanawake, matukio ya kuingilia
kinyume na maumbile yalikuwa 31, matukio
ya kutorosha 22 , matukio ya shambulio
la aibu, kukashifu yalikuwa 148, na matukio ya shambulio yalikuwa 174.
MWISHO.




Comments
Post a Comment