Skip to main content

NADYA JUMA : KIJANA ANAEANZA POLE POLE KUUSAKA UONGOZI, ALIPOANZIA PATAMU

 


NA ZUHURA JABIR, ZANZIBAR@@@@

"Uongozi hauanzi unapopewa cheo; huanza pale unapokuwa tayari kuwahudumia wengine,’’ kauli hii inaelezea kwa ukamilifu safari ya Nadya Juma Idrissa, kijana ambaye ameonyesha kuwa uongozi wa kweli hujengwa kwa kujituma, nidhamu na huduma kwa jamii.

 

Katika kipindi ambacho vijana wengi bado husita kushiriki katika masuala ya uongozi, Nadya, aliamua kuchukua hatua mapema.

 Alianza kama mwanachama wa kawaida wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), lakini leo ni Katibu wa Hamasa wa Tawi la ‘UVCCM’ katika Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU).

Safari yake ni ushahidi kwamba mafanikio hayaji kwa bahati, bali hujengwa hatua kwa hatua.

 

MWANZO WA SAFARI YA UONGOZI

Nadya anasimulia kuwa, safari yake ilianza akiwa bado mwanafunzi, alipokuwa akishiriki kwa hiari, katika shughuli mbalimbali za CCM kwenye tawi la eneo analoishi.

Hakuwa na cheo wala mamlaka, lakini alijitokeza kila mara, kushiriki shughuli za chama, mikutano na kazi za kujitolea.

Kupitia uzoefu huo, alijifunza thamani ya uwajibikaji, nidhamu, ushirikiano na kufanya maamuzi yenye manufaa kwa jamii.

 

Kwa mtazamo wake, kuwa mwanachama wa kawaida kulimjengea msingi imara wa kuelewa kwamba uongozi ni huduma, si mamlaka.

 

Baada ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU), hakubadili mwelekeo wake, kwani aliendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za ‘UVCCM’, akihudhuria mikutano, semina, kampeni za uhamasishaji.

ALIVYOPATA IMANI YA WANACHAMA

Bidii yake haikubaki bila kuonekana, kwani wanachama wenzake walimuamini na kumchagua kuwa, Katibu wa Hamasa wa Tawi la UVCCM katika Chuo Kikuu cha Zanzibar.

Kwa hakika nafasi hiyo iliyompa jukumu la kuhamasisha vijana kushiriki katika shughuli za maendeleo na kuimarisha mshikamano ndani ya chama.

 

"Sikuwahi kufikiria kwamba ningepewa nafasi ya uongozi mapema kiasi hicho, nilichokifanya ni kujituma, kuheshimu watu na kutekeleza majukumu yangu kwa uaminifu," anasema.

 

Kupitia nafasi hiyo, Nadya alipata uzoefu wa kupanga shughuli za chama, kuzungumza mbele ya hadhara, kushirikiana na viongozi wa ngazi mbalimbali na kujenga uwezo wa kuongoza makundi yenye mitazamo tofauti.

UONGOZI ULIBADILI MAISHA YAKE

Kwa Nadya, uongozi haukumletea uzoefu wa kisiasa pekee, bali ulimjengea kujiamini, kumpa uwezo wa kufanya maamuzi kwa haraka na yenye busara.

Anasema nafasi alizopata zimemfungulia milango ya fursa nyingi, zimemsaidia kujenga mtandao mpana wa watu na kumwandaa kwa majukumu makubwa zaidi.

"Nimejifunza kuwa mafanikio hayaji kwa bahati pekee, bali yanahitaji nidhamu, uvumilivu, kujifunza kila siku na kuheshimu watu unaofanya nao kazi," anasimulia.

CHANGAMOTO HAZIKUKOSEKANA

Kama ilivyo kwa safari nyingi za mafanikio, njia yake haikuwa rahisi.

Changamoto kubwa ilikuwa kusawazisha masomo na majukumu ya uongozi, wakati mwingine alilazimika kusafiri kwa ajili ya shughuli za chama, katika kipindi ambacho masomo yalikuwa yanaendelea.

Anasema kulikuwa na nyakati ambazo, alikosa kuhudhuria vipindi kwa takribani wiki mbili kutokana na majukumu ya kichama.

 

Hata hivyo, hakuruhusu changamoto hizo zimrudishe nyuma, ikiwemo kukatisha masomo au kukubali kuwa pocho darasani.

"Niliona changamoto hizo kama sehemu ya kujifunza, zilinifundisha kupanga muda, kuwajibika na kufanya maamuzi kwa haraka,"anasema.

Kwa upande wake, Afisa Programu na Mawasiliano kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Zanzibar (TAMWA-Zanzibar) Khairat Ali, amesema lengo  la mafunzo wanayoyatoa ni kuwajengea uwezo waandishi kuhusu masuala ya wanawake na uongozi.



Akiamini kuwa, hatua hiyo itasaidia kuibua changamoto za wanawake na jamii kwa ujumla, ili zipatiwe ufumbuzi kutoka kwa mamlaka husika.

MAMA YAKE ANASEMAJE ?

Mama yake mzazi, Fatma Haji Khatib, anasema ameshuhudia mabadiliko makubwa tangu mtoto wake, aanze kushiriki katika shughuli za uongozi.

Anaona sasa, uongozi umemjengea Nadya kujiamini, uwezo wa kushirikiana na watu na kufungua milango ya fursa mbalimbali za maendeleo.

 

"Nina imani naye sana, nitaendelea kumuunga mkono katika kila hatua ya safari yake, kwa sababu naamini ana uwezo wa kuitumikia jamii kwa uadilifu na kujituma,"anasimulia mama yake.

 

Hajra Ramadhan Juma, ninayo heshima kubwa kutoa shuhuda yangu kuhusu kiongozi huyu ambaye nimepata fursa ya kumfahamu katika safari yake ya uongozi ndani ya chama.

Katika kipindi chote nilichomfahamu, ameonyesha uadilifu, uwazi na kujituma kwa hali ya juu, huku, akitanguliza maslahi ya wanachama na maendeleo ya chama.

Aanasema amekuwa mstari wa mbele kusikiliza maoni ya wanachama, kutatua changamoto na kuimarisha mshikamano.

Kama wahenga walivyosema, "Umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu," na hilo amelidhihirisha kupitia uongozi wake, unaojenga ushirikiano na kuleta matokeo chanya.

 

Kwa kuzingatia uwezo wake wa kuongoza na maono yake, ana imani ataendelea kukipeleka chama mbele, na wameahidi kuendelea kumuunga mkono kwa dhati, ili afikie ndoto zao.

Nadya mwenyewe anaamini wanawake wameendelea kuthibitisha uwezo wao katika nafasi mbalimbali za uongozi.

Kwa sasa wanashiriki kikamilifu katika kuhamasisha wananchi, kupanga shughuli za maendeleo na kushiriki katika maamuzi yanayoathiri maisha ya jamii.

 

Hata hivyo, anaona bado zipo changamoto zinazowazuia wanawake wengi kujitokeza kugombea nafasi za uongozi.

 

Anataja hofu ya unyanyasaji wa kisiasa, ukosefu wa mafunzo ya uongozi na siasa, changamoto za kiuchumi pamoja na mitazamo hasi ya kijamii kama baadhi ya vikwazo vinavyopunguza ushiriki wao.

SHERIA ZINASEMAJE?

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, zinatambua usawa wa wananchi na kupinga ubaguzi.

 

Aidha, Tanzania imeridhia Mkataba wa CEDAW pamoja na Itifaki ya Maputo ya Umoja wa Afrika, ambazo zinahimiza wanawake kushiriki kikamilifu katika uongozi na maamuzi ya umma.

Aidha lengo la Tano la Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG 5) linahimiza usawa wa kijinsia na kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi.

 

Hii inaonyesha kuwa, ushiriki wa wanawake katika uongozi si suala la hiari pekee, bali ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa haki za msingi na maendeleo jumuishi.

WANAUME/SERUKALI INASEMAJE

Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi, akizungumza mjini Wete Pemba, kwenye ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi, aliahidi kuongeza nafasi za uteuzi kwa wanawake.

‘’Wanawake wamekuwa wakichapakazi bila ya kusita, hivyo kila ninapofanya teuzi, ntahakikisha nao wanakuwemo, maana ni wachapakazi,’’alisisitiza.

Ali Khamis Makame wa Mikunguni, anasema wanawake, wanayohaki sawa na wanaume katika kushika hatamu za nchi.

‘’Maana mikataba, sera, sheria, katiba na miongozo mbalimbali ya kikanda, Afrika na ulimwenguni haijambagua mwanamke,’’anaeleza.

Katibu mkuu wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar Matar Zahor Massoud, aliwahi kusema kuwa, wanawake hawajawahi kupewa nafasi wakaharibu za uongozi.

Omar Juma Hassan wa Tunguu, alisema jamii isipowaamini wanawake kwenye uongozi, wasitarajie mabadiliko ya kimaendeleo.

Ofisa Mdhamini wizara ya Elim una Mafunzo ya Amali Pemba Mohamed Nassor Salum, moja ya juhudi wanazozifanya ni kuweka serikali za wanafunzi, ambapo wanafunzi wa kike wanapata kujifunza.

Akizungumza kwenye hafla ya kutoa zawadi kwa waandishi wa habari za takwimu, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Dk. Hamad Omar Bakar, alisema wanawake kupewa uongozi sio hidaya, bali ni sheria na kanuni zinaagiza hivyo.

USHAURI WAKE KWA WANAWAKE VIJANA

Nadya anawahimiza wanawake vijana kuamini uwezo wao na kutokata tamaa wanapokutana na changamoto.

Anasema mwanamke anayetamani kuwa kiongozi anapaswa kutafuta elimu, kujifunza mbinu za uongozi, kujenga mtandao wa watu wanaomuunga mkono.

"Usisubiri kupewa nafasi; jitengenezee mazingira yatakayokufanya uaminiwe. Uongozi hujengwa kwa tabia, maadili na utendaji mzuri." anasema.

Safari ya Nadya Juma Idrissa ni zaidi ya simulizi ya mafanikio binafsi; ni somo linaloonyesha kwamba uongozi hujengwa kwa hatua ndogo ndogo, kwa kujituma, kujifunza na kuhudumia wengine.

Kutoka kuwa mwanachama wa kawaida hadi kuwa kiongozi wa UVCCM, ameonyesha kuwa bidii, nidhamu na uadilifu vinaweza kufungua milango ya mafanikio.



Kwa wanawake na vijana wanaoota kuingia katika uongozi, simulizi yake ni ukumbusho kwamba changamoto ni sehemu ya safari, si mwisho wa ndoto.

Kwa kutumia fursa zilizopo, kuendelea kujifunza na kuzingatia maadili, kizazi cha leo kina nafasi ya kuwa nguvu kubwa katika kujenga Tanzania yenye usawa, uwajibikaji na maendeleo endelevu.

                Mwisho


Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

Vikausha damu vya mjamzito hivi hapa, umo mchele, udongo, mkaa, chaki Uwezekano wa kuzaliwa watoto wenye udumavu, utapiamlo ni mkubwa

  NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@ ‘’KILA ninapobeba mimba nimezoea kula mchele kwa wingi naweza kusamehe pilau au biriani,’’ ndio maneno ya mwanzao ya Bahati Mohamed Ali (sio jina lake halisi). Nilimfuma akiwa barazani kwake, mjini Ole wilaya ya Chake chake, pembeni yake akiwa na kibakuli cha mwazi, kwa umbali utaona amejaza chakula aina ya pepe, kumbe ni mchele wa Mbeya. Hujichotea kidogo kidogo na kuushindilia mdomoni mwake, huku akiendela kupiga storia na wenzake, bila ya kujali kuwa ujauzito alionayo na mchele huo hauna mwisho mwema. Kawaida yake akiwa mjamzito, kila anapoamka asubuhi anaroweka mchele upatao robo kilo hivi…na baada ya kumaliza kupika, yeye huchukua mchele wake kutafuna (kula). Wakati mwenza wake na watoto wao, wanakula chakula cha mchana, Bahati yeye hukaa pembeni na kibakuli chake cha mchele akiendelea kubahatisha afya yake. ‘’Mimba nyengine hupenda sana kutafuna mchele wa Mbea na nyengine hupenda mchele wa mapembe, kwa kweli huwa nina hamu (kileo), kwan...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...