RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema jukwaa la uwekezaji la mwaka 2025,
litakuwa chanzo kikubwa cha kuwavuta uwekezaji, kutoka maeneo mbali mbali ulimwenguni,
kuekeza Pemba.
Dk. Mwinyi aliyasema hayo jana, kwenye jukwaa la uwekezaji,
wakati akizungumza na wananchi kupitia vyombo vya habari, lililofanyika maeneo
huru ya uwekezaji wilaya ya Micheweni kisiwani humo.
Alisema, anaamini baada ya jukwaa hilo kumalizika, sasa
wawekezaji watamiminika kisiwani, na hasa kwa vile katike maeneo hayo huru, yapo
miundombinu rafiki kwa ajili yao.
Alieleza kuwa, jukwaa hilo sasa litachapuza maendeleo ya haraka
ya kisiwa hicho, kama ilivyo kwa Unguja, hasa kwa vile ujenzi wa barabara
kadhaa, unaendelea kwa kasi na zipo ambazo zimeshakamilika kwa kiwango cha lami.
Dk. Mwinyi alisema, hata ujenzi wa bandari za Mkoani
Pemba, imeshatanuliwa na huku ujenzi wa bandari ya Shumba ukiendelea, kama
ambavyo wakati wowote ujenzi wa kiwanja cha ndege cha kimataifa utaanza.
‘’Naamini baada ya kukamilika kwa miundombinu yote hiyo,
sasa kisiwa cha Pemba, hakitakuwa na sababu ya wawekezaji kutojitokeza,’’alifafanua.
Rais huyo wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Dk. Hussein Ali Mwinyi, alisema sio miundombinu pekee, inayoendelea
kurekebishwa na kuvutia wawekezaji, lakini hata uzinduzi wa mpango mkakati wa
ZIPA ni sehemu nyingine.
Alieleza kuwa, kupitia jukwaa hilo, tayari ZIPA ilishazindua
Mpango Mkakati wake wa mwaka 2025 hadi 2030, ambao ndani yake, yamo mambo
kadhaa kama ni kipaumbele.
Alifafanua kuwa, Mpango Mkakati huo, umeanisha maeneo
muhimu ya uwekezaji, ambapo kwa Pemba, vipo vivutizi maalum, kama vile vya uwekezaji
wa mkakati.
‘’Ndani ya Mpango huo, unaonensha kwa sasa mwekezaji
anaweza kuwekeza, uwekezaji wenye hadhi ya dola milioni 5, jambo ambalo ni tofauti
na kule kisiwa cha Unguja,’’alifafanua Dk. Mwinyi.
Akiendelea kuuchambua Mpango huo Mkakati wa miaka mitano
ijayo, alisema aidha unaweza kupata hadhi ya uwekezaji kwa dola milioni 2,
ingawa kwa sharti lake ni kuajiri wafanyakazi zaidi ya 100.
‘’Lengo la serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufanya
hivi, kwanza ni kuwavuta wawekezaji wengi zaidi, ili kisiwa cha Pemba, nacho
kifunguke kiuchumi,’’alifafanua.
Hata hivyo Dk. Mwinyi alisema, Mpango Mkakati huo wa
mwaka miaka mitano ijayo, ni kwa ajili ya Zanzibar nzima, ingawa kwa upande wa
kisiwa cha Pemba, umewekewa mkakati maalum.
Akizungumzia sheria za uwekezaji, alisema kwa sasa
Zanzibar inayosheria mpya, ambayo imeshafanyiwa marekebisho, hasa yale maeneo
ambayo yalionekana kuwa na utata.
‘’Kwa sasa sheria yetu ni mpya imeondosha vikwazo, na leo
(jana), tumeshazindua kanuni ambayo, inalengo la kuifanya sheria itumike vizuri
zaidi,’’alisema.
Katika hatua nyingine, Rais huyo wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, alisema majukwaa kama
hayo, ni muhimu kufanyika kila baada ya muda, kwani huwavuta wawekezaji kutoka
maeneo kadhaa.
Alieleza kuwa, kupitia jukwaa kama hilo, wawekezaji
hupata taaluma na mikakati ya serikali na fursa zilizopo katika eneo husika la
uwekezaji.
‘’Unaona kwa mfano kupitia jukwaa hili, kumesainiwa kanuni,
kuzinduliwa kwa Mpango Mkakati wa miaka mitano pamoja na jarida maalum,
linaloelezea mpango na fursa za uwekezaji Zanzibar,’’alieleza.
Hata hivyo, aliwahakikishia wananchi wa ukanda wa
Micheweni, kwamba wataifaidika na ajira pamnoja na ujenzi wa miradi ya kijamii
kutoka kwa wawekezaji.
‘’Tunawashauri kuwa, kila mwekezaji anaeekeza katika eneo
hilo na jingine, aone umuhimu wa kuwasaidia wananchi, katika kufanikisha miradi
yao mbali mbali, kupitia faida wanazozipata,’’alifafanua.
Mapema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi, Uchimu na Uwekezaji
Zanzibar Sharif Ali Sharif, alisaini kanuni ya Uwekezaji, ambayo imekuja
kuimarisha na kuweka hadhi maalum ya uwekezaji Zanzibar na hasa kisiwa cha Pemba.
Alisema, inafahamika wazi, kuwa mwaka 2023, Rais wa
Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi, alishasaini sheria ya Uwekezaji, ambayo ina
mambo mingi mazuri, ikiwemo kukitaja kisiwa cha Pemba, kama eneo la mkakati.
Alieleza kuwa, sasa ni aimani yake kuona wawekezaji,
wanaingia kwa wingi kisiwani Pemba, katika maeneo na visiwa vidogo vidogo.
Katika hatua nyingine waziri Sharif, alisema kanuni
imebainisha mambo ya kuzingatia katika visiwa, ambavyo ni muhimu katika uwekezaji.
Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji
Zanzibar ‘ZIPA’ Saleh Saad Mohamed, mara baada ya kuzindua mfumo, uzinduzi wa jarida
na kusaini mkataba wa ushirikiano baina ya taasisi kadhaa, alipongeza hatua
hiyo.
Alisema mkataba huo umesainiwa baina ya ZIPA, Kamisheni
ya Utalii na Shirika la Bandari, kwamba sasa minara iliyokuwa ikiongoza meli
pekee, iwe ni sehemu ya kivituo cha utalii.
‘’Hivyo sasa, minara iliyopo visiwani, uwekezaji utawekwa,
kama wanavyofanya wenzetu baadhi ya mataifa, ambayo huwa ni kivutio kwa wageni,’’alieleza.
Akigusia mfumo uliozinduliwa, alisema ni sehemu ya pili,
na sehemu ya kwanza, ulizinduliwa mwaka 2023, ambapo unamsaidia mwekezaji kujisajili
ZIPA, kielektroniki.
‘’Kwa uzinduzi wa mfumo kwa awamu ya pili, utamsaidia
mwekezaji kuwasilisha ripoti na changamoto zake kwa wakati, pamoja na taasisi
nyingine za serikali kama TRA, ZSSF, ZRA na kamisheni ya kazi kufutilia taarifa
wanazozihitaji,’’alisema.
Mkurugenzi huyo Mtendaji alieleza kuwa, mfumo huo
utasababidha serikali na taasisi zake, kuona kwa uwazi uchangiaji, ulipaji kodi
pamoja kufuatilia kodi stahiki kwa mwekezaji.
Sheria ya Uwekezaji ya mwaka 2023, imemtaka Waziri husika
wa uwekezaji, kutengeneza kanuni ‘regulation’ ili utekelezaji wa
sheria hiyo, iwe rahisi.
Katika jukwaa hilo la uwekezaji, wawekezaji mbali mbali
wa ndani ya nje, walihudhuria, ambapo pia ZIPA ilizindua jarida lake, ambalo
sasa litakuwa linachapishwa kila miezi sita.
Mwisho
Comments
Post a Comment