KATIBU wa
Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said, amesema
tayari serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, imeanza kwa vitendo kukifungua kisiwa
cha Pemba kiuchumi.
Mhandisi
Zena aliyasema hayo jana, eneo huru la Micheweni mkoa wa kaskazini Pemba, mara
baada ya kuyapokea matembezi ya wanavikundi vya mazoezi na wananchi, kwenye
kongamano la uwekezaji la mwaka 2025, yalioandaliwa na Mamlaka ya Kukuza
Uwekezaji Zanzibar ‘ZIPA’.
Alisema,
kufanyika kwa kongamano hilo ni sehemu ya kukifungua kisiwa hicho kiuchumi,
ujenzi wa barabara kadhaa za kisasa pamoja na utanuzi na ujenzi wa bandari
mbali mbali.
Alisema,
serikali inayoongozwa na Dk. Hussein Ali Mwinyi, inaendelea kuonyesha kwa
vitendo nia yake ya kukifungua kisiwa cha Pemba, kama alivyokuwa akiinadi
wakati wakati wa kampeni.
Alieleza
kuwa, kilichobakia kwa wananchi wa Pemba, ni kushirikiana kwa karibu na serikali
yao, ambayo ina nia ya dhati kuona uchumi wa Pemba, unainuka.
Akizungumza
kuhusu kazi za ‘ZIPA’ Mhandisi Zena, alisema inafanyakazi kubwa ya kuhamasisha
uwekezaji ndani ya nchi, kwa kuwaleta wawekezaji na taifa kupata manufaa.
Aliongeza kuwa,
ujio wa wawekezaji hao, unatanua ongezeko la ajira kwa wananchi, na kuongeza
pato la tu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.
‘’Wenzetu wa
ZIPA, kwanza niwapongeze kwa dhati kwa kazi mnayoifanya ya kuitangaaza Zanzibar
na kusababisha kumiminika kwa wawekezaji,’’’alifafanua.
Hata hivyo Mhandisi
Zena, alimpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein
Ali Mwinyi, kwa kazi kubwa ya kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji.
‘’Kwa mfano
hapa eneo huru la Micheweni Pemba, sasa zipo barabara za kisasa zinazoingia
ndani, miundombinu ya umeme, ambayo ni sehemu ya kuwavutia wawekezaji,’’alifafanua.
Alieleza
kuwa, eneo jingine ni kuona ‘ZIPA’ imeshapanga kwenda kila mkoa wa Zanzibar
kutoa elimu ya uwekezaji na kwa upande wa mkoa wa kaskazini Pemba, elimu hiyo
itatolewa kwenye la hilo, kuanzia mwezi Septemba, mwaka huu.
Hata hivyo, amewakumbusha
wananchi hao wa mkoa wa kaskazini Pemba, kuitumia fursa hiyo, ili wajifunze
namna ya uwekezaji bora.
Mapema Mkurugenzi
Mtendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar ‘ZIPA’ Saleh Saad Mohamed, alisema
wanaendelea na jukumu la kuhakikisha, kuna na uwekezaji wenye manufaa kwa watu
wote.
Alieleza kuwa,
juhudi za Dk. Mwinyi katika kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji, inawapa ari
ya kufanyakazi kwa bidii, jambo ambalo ni manufaa kwa wananchi.
Mkuu wa Mkoa
wa kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib, alisema katika uwekezaji uliopo Pemba,
umesababishwa na utendaji kazi kwa watendaji wa ZIPA.
‘’Nichukuwe nafasi
hii, kuwapongeza sana wenzetu wa ZIPA kwa kazi kubwa wanayoifanya, ya kuvuta
wawekezaji na sasa eneo huru la Micheweni, limekuwa la kuvutia,’’alifafanua.
Waziri wa
Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar Shamata Shaamed Khamis,
alisema sasa Micheweni imekuwa mpya, baada ya kufunguliwa kwa eneo huru la
Micheweni.
‘’Kwa hakika
eneo hili, lilitangaazwa tokea mwaka 1992, kuwa ni eneo huru, ingawa kwa wakati
huo, halikufanyiwa kazi, ingawa kwa sasa ndani ya mwaka 2025, limefunguliwa kwa
kivitendo,’’alifafanua.
Baadhi ya wananchi
wa wilaya ya Micheweni Pemba, walisema hatua ya Dk. Mwinyi ya kukifungua kisiwa
cha Pemba, ni ishara ya ukweli wake na nia yake thabiti.
Nae Bahati
Mansour Kassim, alisema aliwaomba wawekezaji kuangalia kwa jicho la pekee, nafasi
za wanawake katika ajira za muda na za kudumu.
Leo Juni 16,
mwaka huu Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali
Mwinyi, anatarajiwa kuwahutubia wananchi wa mikoa miwili ya na wawekezaji
katika viwanja vya maeneo huru Micheweni, kwenye jukwaa la uwekezaji la mwaka
2025.
Mwisho
Comments
Post a Comment