NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
KITUO cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’, kimewakaribisha wananchi wa shehia za Uwandani wilaya ya Chake chake, kufika ofisini kwao, kwa ajili kupatiwa ufumbuzi wa migogoro mbali mbali ya kisheria, kama vile ya ardhi, tena bila ya malipo.
Kauli hiyo imetolewa leo April 13, 2025 na Mwenyekiti wa kituo hicho Pfro: Chris Maina Peter, alipokuwa akizungumza na wananchi hao, kwenye kambi maalum ya siku tatu inayoendelea skuli ya Uwandani.
Alisema, kituo hicho hakijasita kutoa ushauri, elimu na msaada wa kisheria bila ya malipo kwa wananchi wasiokuwa na uwezo, kwani sio muda wa kukaa kinyonge kwa wananchi.
Profesa Chris, alisema bado mpango wa kituo hicho ni kuendelea kuwasaidia wenye changamoto kama za kukoseshwa vitambulisho, vyeti vya kuzaliwa na fidia kwa ardhi zao.
‘’Ni kweli leo tupo hapa shehia ya Uwandani kwa muda wa siku tatu, tumewafuata wananchi lengo ni kuwasikiliza ikiwa wanachangamoto za mambo ya kisheria, kuwasaidia bila ya malipo,’’alifafanua.
Mapema Ofisa Mipango wa ‘ZLSC’ Benny Louis Mlingi, aliwakumbusha wanawake nchini, kukataa kuolewa kwa njia ya mkopo wa mahari, kwani mwisho wake hukosa haki zao.
‘’Wakati mwingine wapo baadhi ya waowaji, hukosa kumaliza mahari, ingawa malalamiko huibuka baada ya ndoa kuvunjika, sasa hili pia tunashughulika nalo,’’alifafanua.
Katika hatua nyingine Afisa huyo Mipango, aliwakumbusha wananchi kuwa, wasikubali kupokonywa haki zao na kisha kukaa kimnya, kwani watetezi wao ni ‘ZLSC’.
Kwa upande wake Afisa Sheria wa ‘ZLSC’ Asha Maulid Khamis, aliwataka wanawake waliodhulumiwa haki zao, kuzitumia siku tatu za kambi hiyo, ili kutoa malalamiko yao.
Sheha wa Uwandani Ali Hamad Mussa, aliwapongeza watendaji hao wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’, kwa uamuzi wao wa kuwafuata kijijini hapo.
Mwananchi Mwajuma Ali Salim na Khamis Abdalla Hamad, walisema, kambi hiyo imewasaidia kupata ufumbuzi wa changamoto za kisheria, zilizokuwa zikiwakabili kwa muda mrefu.
Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’, kimeasisiwa mwaka 1992, kwa kutoa huduma za maktaba, kuwasomesha wasaidizi wa sheria na kutoa elimu, msaada na ushauri wa kisheria kwa wananchi bila ya malipo.
Mwisho
Comments
Post a Comment