NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
AFISA Mdhamini Wizara ya Fedha na Mipango Pemba, Abdulwahab Said Abuu-bakar aliwataka wadau wanaohusika na uandaaji wa malipo ya michango katika mifumo ya Mfuko wa hifadhi ya jamii (ZSSF) kutumia mifumo hiyo kwa usahihi ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa wanachama wake.
Aliyasema hayo April 15, 2025 katika mkutano wa kuwajengea uwezo wadau hao uliofanyika katika ukumbi wa (ZSSF) Tibirinzi Chake Chake Pemba.
Alisema kumekua na malalamiko ya ucheleweshwaji wa upatikanaji wa mafao ya ustaafu kutoka kwa wanachama, yanayosababishwa na taasisi kushindwa kuweka kumbukumbu vizuri, katika mifumo hiyo.
Hivyo alisema ni vyema kwakila taasisi kuhakikisha inatimiza majukumu yake vizuri ili kupunguza malalamiko hayo kwa wastaafu wa serikali na taasisi binafsi.
"Ni vyema taasisi zihakikishe zinatimiza majukumu yake vizuri ili kupunguza malalamiko kutoka kwa wastaafu wa serikali na taasisi binafsi" alisema.
Alieleza kua serikali imeandaa utaratibu wa kuwalipa wastaafu mafao yao ndani ya wiki mbili baada ya kustaafu, hivyo amewataka wadau hao kutumia vizuri mifumo ya habari na mawasiliano ili kulifanikisha hilo.
Alisema mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar (ZSSF) inatumia mitandao ya kijamii ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa, hivyo amewaomba wadau hao kutumia mitandao hiyo pamoja na kushajihisha wengine kuitumia ili kuondoa changamoto ya ucheleweshwaji wa mafao kwa wanufaika.
Aidha aliipongeza (ZSSF) kwa kua na utaratibu wa kukutana na wadau hao mara kwa mara, ambayo ni hatua muhimu katika kuchochea maendeleo, huku akiwasihi kuendeleza utaratibu huo.
Akiwasilisha mada kuhusu umuhimu wa hifadhi ya jamii Afisa hifadhi ya jamii Pemba Said Omar Juma alisema, Mfuko wa hifadhi ya jamii ni kwaajili ya watu wote wenye ajira rasmi na zisizo rasmi.
Alieleza kua hifadhi ya jamii inaumuhimu mkubwa kwa jamii kwani inamuhakikishia kipato mwanachama baada ya kustaafu pamoja na kutoa ulinzi wa kifedha kwa wanufaika.
Alisema ingawa kunachangamoto ya uelewa mdogo kwa wananchi, pamoja na uhaba wa mashirikiano kutoka kwa wananchi, lakini wamekua wakifanyajitihada mbali mbali ikiwemo kutoa elimu kwao.
Alisisitiza kua hifadhi ya jamii ni nguzo muhimu kwa maendeleo ya Taifa, hivyo ni wajibu wa serikali, taasisi binafsi na wananchi kuungamkono ili kuzidi kuimarika.
"Hifadhi ya jamii ni nguzo muhimu kwa maendeleo ya Taifa, hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kuanzia serikali, taasisi binafsi na wananchi kuungamkono ili uzidi kuimarika" alieleza.
Nae Afisa tehama wa ZSSF Pemba Madi Jafar Khamis alisema matumizi ya mifumo katika ukusanyaji wa taarifa itasaidia kuweka sawa kumbukumbu za fedha pamoja na kuhifadhi taarifa kwa usahihi na kwa wakati.
Akiwasilisha mada kuhusu fidia ya ajalikazini inayotolewa na( ZSSF) Ali Mtemani Hussen Afisa hifadhi ya jamii Pemba alisema, fidia hio ni haki ya msingi ya kila mwanachama atakaepata kadhia hii, huku akisisitiza kua (ZSSF) ipo kwa ajili ya kustawisha jamii.
Kwaupande wake Kaimu Mkurugenzi ZSSF Pemba Msabah Massoud Msabah aliwataka wadau walioshiriki mafunzo hayo kuendelea kutumia mitandao ya mfuko huo kwa kutoa maoni na ushauri ili kuongeza ufanisi katika utendaji wao wa kazi.
Hatahivyo alitoa shukrani kwa wadau walioshiriki mafunzo hayo huku akiwaomba kuripoti changamoto zao ili kupatiwa ufumbuzi wa haraka.
Nae mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo Ali Talib Bakkar kutoka wizara ya Fedha na mipango, alitoa pongezi kwa mfuko wa hifadhi ya jamii kwa kuwapatia mafunzo hayo, huku akiwataka wadau wengine kurahisisha upatikanaji wa taarifa muhimu ili wanachama wapate mafao yao kwa haraka.
MWISHO
Comments
Post a Comment