NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
KAIMU Mkurugenzi Mwendeshaji Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Pemba Msabah Masoud Msabah, aliwataka waajiri kufuata sheria zilizowekwa na Mfuko huo ili kuhakikisha upatikanaji wa haki za msingi za wanachama wao.
Aliyasema hayo April 16 2025, wakati akizungumza na wadau wanaohusika na uandaaji wa malipo ya michango katika mfuko huo kutoka taasisi binafsi, huko Tibinzi Chake Chake Pemba.
Alisema iwapo waajiri watafuata sheria zilizowekwa na mfuko huo, itasaidia kupata haki zao zote za msingi ndani ya mda husika, jambo ambalo ni kipaombele cha mfuko huo.
Alisema kwa sasa mfuko umeanzisha mfumo maalumu, utakaomuwezesha mwanachama kuweka pamoja na kupata taarifa zake zote za mwenendo wa uchangiaji wake, hivyo ni vyema kwa waajiri kutumia mfumo huo ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa.
"Mfuko wa hifadhi ya Jamii (ZSSF) umeandaa mfumo maalumu utakaomuwezesha mwanachama kupata taarifa zake kwa urahisi ( employers potlal), basi ni vyema kwa waajiri kutumia mfumo huo ili kuboresha huduma ", alieleza.
Hata hivyo alitoa wito kwa washiriki hao kuendelea kutoa mashirikiano ili kuimarisha huduma za mfuko huo.
Akiwasilisha mada kuhusu umuhimu wa hifadhi ya jamii Afisa hifadhi ya jamii Pemba Said Omar Juma alisema kua, mfuko huo unaumuhimu mkubwa kwa jamii kwani inamuhakikishia kipato mwanachama baada ya kustaafu pamoja na kutoa ulinzi wa kifedha kwa wanufaika.
Hata hivyo alisema Mfuko wa hifadhi ya jamii unahuduma ya uchangiaji wa hiari ambao walengwa wake ni wajasiriamali, mamalishe, boda boda na watoto wenye umri kuanzia siku moja hadi miaka 18, hivyo aliwataka wananchi kutumia fursa hiyo ipasavyo.
Alisema iwapofursa hiyo itatumika ipasavyo itasaidia kuongeza usawa kwa jamii, pamoja na kuchangia katika miradi ya maendeleo kutokana na uwekezaji unaofanywa na mfuko huo.
Hata hivyo akiwasilisha mada kuhusu fao la ajali kazini afisa huyo alisema ni vyema mwanachama aliefikwa na kadhia hiyo kufuata taratibu zilizowekwa ikiwemo kuwasilisha taarifa za ajali kazini mapema iwezekanavyo.
Nae Afisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wa mfuko huo Pemba Madi Jaf, akiwasilisha mada kuhususu upatikanaji wa huduma za wanachama kwa njia ya mitandao alisema kwa sasa mfuko unaprogramu tatu zitakazomuwezesha mwanachama kupata taarifa zake.
Hivyo aliwataka wadau hao kuitumia pamoja na kutoa elimu kwa wanachama wengine kujiunga na programu hizo ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa sahihi ili kuondosha usumbufu na kuongeza ufanisi katika utoaji huduma.
Nao washiriki wa mafunzo hayo wameshauri mfuko huo kuboresha zaidi mifumo hio, ili itoe taarifa kwa wakati na usahihi pamoja na kuipongeza "ZSSF" kwa kuwapatia mafunzo hayo yatakayowasaidia katika utendaji wao.
Awali katika ufunguzi wa mkutano huo Mratibu wa tume ya maadili ya viongozi wa Umma Abdullah Muhammed Mbarouk alisema, lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo watendaji hao ili kuimarisha utendaji kazi wa taasisi zao.
Hata hivyo aliwaomba watendaji hao kutumia lugha nzuri wakati wa kutoa huduma kutokana na umuhimu wao katika taasisi zao.
Mfuko wa hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) ulianzishwa chini ya sheria ya mfuko wa Usalama wa Zanzibar Na 2 ya 1998, ikiwa miongoni mwa kazi zake ni kuhifadhi michango ya wanachama na kutoa mafao kwa wanachama wake, huku fao lake kuu likiwa ni fao la ustaafu na inafanya kazi katika visiwa vya Unguja na Pemba.
MWISHO
Comments
Post a Comment