NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
KITUO cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’ sasa kimeelekeza nguvu yake kwa wananchi wa shehia ya Wingwi Mjananza wilaya ya Wete Pemba, kwa kambi ya siku tatu, ya kutoa elimu, ushauri na msaada wa sheria bila ya malipo.
Kambi hiyo, ipo ndani ya skuli ya Msingi ya Mjananza, ambayo ilianza jana April, 16, na ikitarajiwa kumalizika kesho majira ya saa 8:15 jioni.
Akizungumza na wananchi hao, juu ya utaratibu wa utoaji wa msaada huo, leo April 17, 2025 skulini hapo, Afisa Miradi wa ‘ZLSC’ Beny Louis Mlingi, alisema kwanza, mwananchi atapaswa asajiliwe, kwenye fomu maalum kambini hapo.
Alieleza kuwa, baada ya hapo atakutana na wanasheria nguli pamoja na mawakili na Vakili, wanaofanyakazi Kituo cha Huduma za Sheria, kwa ajili ya kusikilizwa lalamiko lake.
Alifahamisha kuwa, katika kambi hiyo, inawakaribisha wananchi wenye changamoto za kisheria, kama vile migogoro ya mipaka, ardhi, matunzo kwa watoto, waliokosa vyeti vya ndoa, vya kuzaliwa.
Eneo jingine wanaloshughulikia na kumpa muathirika ushauri na maelekezo ya kisheria na wale ambao wamekoseshwa mirathi, kutomaliziwa mahari pamoja na wale ambao, kesi zao zimekwama vituo vya Polisi.
‘’Lakini hata kama kuna mtu aliombwa rushwa wakati anafuatilia haki zake, au wakati mwingine alifanyiwa udhalilishaji na kiongozi, tunawahitaji kwa ajili ya kuwashauri kisheria,’’alifafanua.
Kwa upande wake Afisa Sheria wa ‘ZLSC’ Asha Maulid Khamis, aliwataka wananchi hao, kuondoa woga, wakati wanapofuatilia haki zao.
‘’Hatakama muume au baba amekutendea visivyo au wakati mwingine kuna mjomba au kaka, amekalia mirathi kwa muda sasa, ni vyema kwa wananchi wakatufika kutueleza na kuwashauri kisheria,’’alieleza.
‘’Kwa mfano tulipokuwa shehia ya Uwandani wilaya ya Chake chake, zipo kesi za mirathi tumezipata na sasa wale warithi wanaweza kurithi, baada ya kuwapa ushauri na msaada wa kisheria,’’alifafanua.
Hata hivyo, aliwakumbusha wananchi kuwa, ‘ZLSC’ haishughulikii upatikanaji wa vyeti vya kuzaliwa pekee, bali hata migogoro kama ya ndoa, ardhi, madeni tunawakaribisha.
Sheha wa Mjananza, Hamad Said Ali, alisifu ubunifu wa ‘ZLSC’ wa kufunga safari na kuwafuata wananchi wake, jambo ambalo kama sio kuwepo wao, wengeendelea kuishi na changamoto zao.
Hata hivyo, amewakumbusha wananchi, ambo kwa jana na leo hawakupata nafasi ya kufika kwenye kambi hiyo, nafasi ya kesho ipo, na wafike ndani skuli ya Msingi Mjananza, ili kupata ushauri wa kisheria.
‘’Sio busara kama mtu anamgogoro wa ardhi, mirathi, matunzo ya watoto kukaa nyumbani, kwani wanaotoa ushauri na msaada wa kisheria, wapo ndani ya shahia yangu,’’alifafanua.
Wakizungumza nje ya kambi hiyo baada ya kuhudumiwa, wananchi wa shehia ya Mjananza, walielezea kufurahishwa kwao, na msaada wa kisheria walioupata.
Moza Haji Hamad na Salma Omar Pandu, walisema wanatamani kuona kila mwaka, wanapata kambi kama hizo, ili kufikisha malalamiko yao.
Kambi hiyo ya siku tatu, ilianza jana na inatarajiwa kumalizika kesho April 18, 2025, ambapo tayari ‘ZLSC’ kimeshawahudumia wananchi 112, wakiwemo wanawake 80 na wanaume 32 wa shehia ya Uwandani wilaya ya Chake chake hapo juzi.
Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’, kimeasisiwa mwaka 1992, kwa kutoa huduma za maktaba, kuwasomesha wasaidizi wa sheria na kutoa elimu, msaada na ushauri wa kisheria kwa wananchi bila ya malipo.
Mwisho
Comments
Post a Comment