‘Aweka mikakati wanabaki daraja la kwanza na la
pili tu.
IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA
"Nilipoteuliwa kuwa Mwalimu Mkuu, mwanzo
nilipata hofu hasa pale nilipojiona, naenda kuongoza watu wenye kiwango cha
elimu sawa na mimi,’’anasema.
Ni maneno
ya Mwalimu Mkuu skuli ya Sekondari ya Wanawake Utaani Wete, Siti Faki Ali
mkaazi wa Chasasa Wete.
Mwalimu
huyo ambae alitokea skuli ya Chasasa akiwa Msaidizi Mwalimu Mkuu, alipata hofu
mara ya kupokea barua ya kwenda kuiongoza skuli hiyo.
Anasema,
kwa vile ameshakaa uongozi katika mambo mbalimbali ya kijamii na Serikali
kwenye nafasi ndogo ndogo, ndipo alipoona kwamba na nafasi hiyo anaweza
kuiongoza.
Mara
baada ya kukabidhiwa madaraka, alianza kuweka mikakati, ikiwemo kuondosha zero
kwa wanafunzi kuanzia kidato cha pili hadi cha sita.
"Nilipofika
nilianza kuangalia kitu gani nifanye, ili kuifanya skuli hii, iwe nzuri na ya
mfano wa kuigwa, nikaamua kwanza niwaandae walimu wangu vizuri, ili wapate
nguvu ya kufundisha,’’anabainisha.
Anasema, hilo limeanza kufanikiwa, maana mwaka jana,
kidato cha nne na mwaka huu cha sita hakuna mwanafunzi alietoka na zero, hali
ambayo haijawahi kutokea kwa kidato cha nne.
Atajipanga zaidi kuimarisha mipango yake na mikakati,
kuhakikisha wanafunzi wa skuli ya Utaani, wanakuja na daraja la kwanza na la
pili tu.
Matokeo
ya Kidato cha nne
Mwaka
2023 wanafunzi waliofanya mitihani ni 159, ambapo daraja la kwanza walikuwa 15,
daraja la pili 20, daraja la tatu 26, daraja la nne 91 na zero saba (7).
Mwaka 2024,
wanafunzi wote ni 87, ambapo daraja la kwanza ni 11, daraja la pili 12, daraja
la tatu 24, daraja la nne 39 na zero moja (1).
Huku
mwaka 2025, wanafunzi waliofanya mitihani ni 113, ambapo daraja la kwanza 29,
daraja la pili 44, daraja la tatu 27, daraja la nne 12 na hakukuwa na zero.
Matokeo
ya kidato cha sita
Mwaka
2023, wanafunzi waliofanya mitihani ni 31, ambapo daraja la pili ni sita (3),
daraja la tatu 20, daraja la nne watatu (3) na zero mbili (2), huku mwaka 2024,
wanafuzi wote ni 21, daraja la kwanza moja (1), daraja la pili 13 na daraja la
tatu, ni saba (7).
Mwaka
2025 wanafuzi waliofanya mitihani ni 35, daraja la kwanza nne (4), la pili 14,
na daraja la tatu 17, ambapo mwaka 2026, wanafunzi wote ni 49, daraja la kwanza
wakiwa watano (5), la pili 21 na daraja la tatu 23.
Mwalimu
huyo anasema, mwaka huu 2026 wanaotarajiwa kufanya mitihani ni wanafunzi 35 wa
kidato cha nne, na mwaka 2027 watafanya mitihani wanafuzi 64 wa kidato cha
sita.
Katika
mikakati yake ya kuifanya skuli hiyo inakuwa bora kwa Tanzania nzima, kwanza
amekuwa akitafuta njia ya kutatua matatizo kwa walimu wake.
"Nilipofika
katika skuli hiyo nilikuta kuna mpasuko kidogo, hivyo nilirekebisha kwa kusikiliza
kero zao na kuzitafutia ufumbuzi, ikiwemo kupatiwa maslahi bora," anasema.
Hilo
limewapa nguvu walimu na hamasa ya kuwafundisha wanafunzi kwa juhudi zote,
jambo ambalo anajivunia hadi sasa.
Mwalimu
huyo anafanya kazi kwa uwazi na uwajibikaji, kwani anawashirikisha walimu wake
kwa kila jambo, linalofanyika na hatua inayofikiwa.
"Viongozi
wengi wanaokuja hapa kututembelea, wanasifu maendeleo yaliyofikiwa katika skuli
yetu, kwa kweli tunajivunia," anasema.
Anaeleza,
walimu wake wanapohitaji vifaa vya kufundishia, huwapatia vilivyopo na ikiwa
hakuna, basi hufanya juhudi mbalimbali, kuhakikisha vinapatikana.
Mikakati
mingine ameanzisha masomo ya ziada, kuhakikisha wanapata muda mzuri wa
kujisomea, na kuwatafutia walimu wa masomo, ambayo hayana mwalimu wa kutosha.
"Masomo
haya ya ziada ni kwa ushirikiano wetu pamoja na wazazi wa wanafunzi, hivyo kwa
sasa hata walimu wanaosomesha masomo ya ziada, nimefanya utaratibu wa
kuwaongezea malipo, kwa hiyo wamepata moyo,’’anasema.
Anasema,
huwafanyia wanafunzi majaribio ya kila wiki, kila mwezi, kufanya ushindani
baina ya skuli yake na nyingine, ili kuona wanafunzi wanasoma kwa bidii.
"Tunatofautiana
kwenye ufahamu, kwa kuliona hilo, wale wanafunzi wenye ufahamu mzito, tunawatafutia
wenzao kuwasaidia zaidi, na vilevile walimu hutenga muda maalumu kuwaelewesha,’’
anasimulia.
Katika
mipango mengine ya kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora, Serikali
imewawekea Programu za kusomeshea walimu, ikiwemo ya 'Smart body TV' ambayo mwalimu anatoka chuo kikuu cha Shangai
nchini China.
Program
hiyo, inafundisha walimu wa somo la hisabati wa skuli hiyo, pamoja na
kushirikiana na walimu wa skuli za Chasasa, CCK, Fidel Castro na Madungu, ili
kusudi wanafunzi wao wawe bora.
Ipo Programu
ya "But Camp' ya sayansi, ambayo
wanafunzi wake, walikwenda kusoma Pujini na kupata zawadi kwa jinsi
walivyofaulu vizuri.
Mwalimu
huyo Mkuu, anasema kwa upande wa masomo ya Sanaa 'Art' pia wanafaidika na programu hizo na wanafunzi, wanafaulu
vizuri katika masomo yao.
Mambo
hayo wanayoyafanya wanashirikiana na Kamati ya skuli, huku jamii ikifurahia
mfumo wake wa kutatua kesi za wanafunzi bila upendeleo.
Skuli ya
Sekondari Utaani ina wanafunzi wanawake 712 ambao ni michepuo, na ni kuanzia
kidato cha kwanza mpaka cha sita.
Anasema,
uongozi kwa wanawake ni changamoto kwa sababu wanaonekana ni wadhaifu, pia
wanaume hawataki wala hawapendi kuongozwa na wanawake.
Mwalimu
huyo alianza kazi yake ya ualimu katika skuli ya msingi Kizimbani Wete, na
baada ya kupata elimu ya cheti na diploma, alihamishiwa skuli ya Sekondari
Utaani, akiwa mwalimu wa kawaida.
Mwaka
2013, alipelekwa skuli ya Sekondari Chasasa, na ilipofika mwaka 2021 ndipo
alipoteuliwa kuwa Msaidizi Mwalimu Mkuu skuli hiyo.
Mwaka
2025, aliteuliwa kuwa Mwalimu Mkuu skuli ya Sekondari ya Wanawake Utaani,
nafasi ambayo anaitumikia hadi sasa.
Alisoma
elimu yake ya msingi katika skuli ya msingi Jadida Wete, na Sekondari alisoma
Wingwi katika skuli ya Sekondari ya ‘Dodeani
Technical’ ambayo ilianzishwa na Jumuiya ya Wazazi.
Kidato
cha tano na cha sita, alisoma skuli ya Sekondari Lumumba Unguja, na kwa sasa
ana elimu ya chuo kikuu ngazi ya digirii ya pili (Masters) katika fani ya lugha
ya Kiswahili.
Mwalimu
huyo, nje ya saa za kazi ni Msaidizi wa Sheria Wilaya ya Wete, akiwa mshika fedha
wa jumuiya yao.
WALIMU WENZAKE
Mwalimu
Fatma Kombo Mbarouk anasema, mwalimu huyo ni mfuatiliaji na mpambanaji, katika
shughuli zake za kitaaluma, na anawashirikisha kikamilifu.
Wanajivunia
kuwepo kwake, kwa sababu ufaulu umenyanyuka, kwani kulikuwa na wanafunzi ambao
wameshakosa muelekeo, hivyo baada ya kufika yeye kwa hekima na busara, alichangia
ufaulu.
“Yupo
vizuri kusimamia kila kwenye kasoro kurekebisha, unapofanya kosa anakuelekeza, anaondoa
migogoro, itayotendeka baina yetu,’’anaeleza.
Mwalimu
Sharif Juma Fakih, anakiri kuwa, Mwalimu huyo ana sifa ya kupokea fikra,
zinazotoka kwao, huzipima na kuzifanyia kazi kwa uweledi.
“Ana ile
hamasa ya kutaka kuleta ufaulu mzuri katika skuli yetu, anafuatilia na
kusimamia mahitaji ya walimu, na namna gani skuli itafanya vizuri zaidi, jambo
ambalo, ndio ndoto yetu walimu,”
anasema.
Menyekiti
wa Kamati ya skuli hiyo Maulid Abdi Aweis anasema, mwalimu huyo yupo vizuri
katika utendaji wa kazi na anawashirikisha walimu wenzake pamoja na kamati yao
kwa kila jambo.
Anasema,
anaweza kuongoza vizuri kwa sababu ana elimu ya uongozi na sheria, hivyo
ameleta mabadiliko kwenye ufaulu pamoja na walimu kushirikiana nao.
“Anafanya
maamuzi ya pamoja, na nikiwauliza walimu wanasema hawajapata changamoto yeyote,
hivyo namuomba azidishe ushirikiano ili kusiwe na makundi yatakayosababisha
kushusha ufaulu wa wanafunzi wao,” anasema.
Mwanafunzi
Hafsa Mkubwa Salum anasema, mwalimu huyo ana hekima na upendo kwa wanafunzi
wake, kwani ana tabia ya kuwatafutia walimu, na kuwaweka karibu na kuwasaidia
sana wanafunzi ambao wana uwelewa mzito.
Mzazi wa
mwanafunzi anaesoma skuli hiyo mkaazi wa Ole, Fatma Ali anasema, mwalimu huyo
ana juhudi sana na alifanya mabadiliko wa watoto wao kwa sababu walisoma kwa
bidii zaidi.
“Ukimpelekea
changamoto anaitatua kwa haraka, ana moyo wa kujitolea, na nimeshukuru mtoto wangu
alipata daraja la pili kidato cha nne mwaka jana,” anasema.
WIZARA YA
ELIMU
Ofisa
Mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Pemba Mohamed Nassor Salim anasema,
utendaji wa Mwalimu huyo, ni mzuri na anaongoza skuli ya wanawake kwa ufanisi
na utulivu.
Anasema wizara,
ilimchagua kusimamia skuli hiyo, baada kuona anakidhi vigezo vyote vya uongozi,
ikiwemo elimu, kuwa na maadili mema, kujiamini.
Kumbe kilichowasukuma
kumpa dhamana hiyo, ni kutokana na ubunifu alionao, ushirikiano na wadau wao wakiwemo
wazazi, kamati za skuli na jamii kwa ujumla.
Mdhamini
anamshauri Mwalimu huyo, kuwa kuendeleza uzalendo wa kweli, aendelee kuwa na
nidhamu ya hali ya juu, pamoja na kujiendeleza kielimu.
ASASI ZA
KIRAIA
Mratibu wa Programu ya mradi wa ‘SWIL’ kutoka TAMWA- Zanzibar
Sabrina Ali Mwatanga anasema, wanaendelea kuelimisha na kuhamasisha uongozi kwa
wanawake, ili waingie kwa wingi katika vyombo vya maamuzi.
“Naamini kwamba, mwalimu huyu ataendelea kuwasimamia vizuri
wanafunzi hao, ili wafaulu vizuri, na kwa vile ni wanawake atakuwa amewasaidia,
kwani miongoni mwa changamoto zinazowakumba wanawake kuingia kwenye uongozi,’’anasema.
Mkurugenzi wa Jumuiya ya Utetezi wa Mazingira na Jinsia Pemba ‘PEGAO’ Hafidh Abdi
Said, anasema juhudi za Mwalimu Mkuu huyo, zinaleta matumaini bora kwa watoto
wa kike, kujiendeleza kielimu.
“Lengo letu ni kufikia 50 kwa 50, hivyo naamini mikakati
aliyoiweka Mwalimu huyo, kwenye skuli yake, itasaidia kutoa viongozi bora wa
baadae, ambao wataleta maendeleo katika nchi yetu,” anaeleza.
Kifungu cha 21 (2) cha
Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kimeeleza kwamba, kila mzanzibari anayo haki
na uhuru wa kushiriki, kikamilifu katika kufikia uamuzi, juu ya mambo yanayomuhusu
mwanamke na taifa lake.
Serikali mbalimbali
duniani, zimeridhia mikataba na matamko mbalimbali ya usawa wa kijinsia na
uwezeshaji wanawake kwenye uongozi na nafasi za kisiasa, tangu mwaka 1948
ziliporidhia tamko la haki za binadamu.
Matamko na mikataba
mbalimbali ya kimataifa na kikanda, yanaainisha haki za kiraia na kisiasa kwa
wote bila kujali jinsia, rangi au dini.
Huku Azimio la
kimataifa, juu ya haki za binadamu la mwaka 1948 ambalo ndio msingi wa haki za
binadamu, ikiwemo za kiraia na kisiasa, linatoa haki kwa kila mtu katika
uongozi.
Skuli ya sekondari
Utaani Wete imeanzishwa mwaka 1954 kabla ya Mapinduzi, ambapo ilipofika mwaka 2014,
Rais Mstaafu wa Zazibar Dk. Ali Mohamed Shein aliitangaza rasmi kwamba skuli
hiyo ni ya wasichana tu.
MWISHO.


Comments
Post a Comment