By
PEMBA TODAY
| NA AMRAT KOMBO, ZANZIBAR@@@@ |
JUMUIYA ya Maimamu Zanzibar (JUMAZA) imesema inaunga mkono tamko la maridhiano ya chama cha CCM na ACT Wazalendo kwani ni hatua ya msingi katika kuimarisha amani, umoja na maendeleo ya Zanzibar.
Katibu Mtendaji wa Jumuiya hiyo, Shekh Ali Abdalla Amour, aliyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Jamatkhan Vuga mjini Unguja.
Alisema jumuiya hiyo imepokea kwa faraja na furaha maridhiano yaliyotangazwa hadharani Julai 9, katika viwanja vya Ikulu
Zanzibar mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan.
Aidha alisema ni vyema kwa viongozi hao kutofanya khiyana katika utekelezaji wa makubaliano hayo ili kuendelea kujenga amani, umoja na mshikamano kwa wananchi wa Zanzibar.
Alieleza kuwa jambo hilo limeonesha utayari wa viongozi kuweka mbele maslahi ya Zanzibar na wananchi wake badala ya tofauti za kisiasa.
Alisema mafanikio ya maridhiano hayo yatategemea uaminifu, dhamira ya kweli na utekelezaji wa makubaliano kwa ikhlasi hivyo viongozi wote wana wajibu wa kutekeleza ahadi walizoweka mbele ya wananchi na mbele ya Mwenyezi Mungu.
Sambamba na hayo aliwapongeza viongozi wastaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, Dk. Amani Abeid Karume na Juma Duni Haji kwa mchango wao katika kusimamia maridhiano katika awamu ya uongozi iliyopita.
" Viongozi wetu wameonyesha ukomavu wa kisiasa uliowezesha kufikiwa kwa makubaliano tunayoyaona sasa" alisema.
Nae, Naibu Amiri JUMAZA Taifa, Shekh Mohammed Haji Omar, alisema nia ya dhati inapokuwepo mambo yanafanikiwa
kwa asilimia kubwa na anaamini matumaini yake jambo hilo litakwenda vizuri.
Alifahamisha kuwa kuna na manufaa makubwa kutokana na historia kwani serikali ya awamu ya nane ina maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii katika sekta mbalimbali.
“Jambo moja lilobaki ni hili la wananchi kuwa pamoja kimaadili,kisiasa na kimaendeleo hivyo tuna imani kubwa mambo yatakuwa mazuri kutokana na serikali ilivyoonesha maendeleo makubwa,” alisema.
Katibu wa Bodi ya Wadhamini JUMAZA, Masoud Hemed Nassor, alisema JUMAZA ipo tayari kushirikiana na wadau mbalimbali wakati wowote itakapohitajika ili kuhakikisha maridhiano hayo yanadumu na kuzaa matunda yenye manufaa kwa Zanzibar na wananchi wake.
Baadhi ya wananchi wa Zanzibar walisema wanauunga mkono mchakato wa maridhiano hayo kwani suluhu na maelewano ni sehemu ya mafundisho ya dini ya kiislamu na ndio njia bora ya kulinda amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.
MWISHO
- Get link
- X
- Other Apps
- Get link
- X
- Other Apps

Comments
Post a Comment