NA ZUHURA JABIR,
ZNAIBAR
“Usafi ni nusu
ya afya."
Haya sio msemo
wa utani, bali ni ukweli unaogusa maisha ya kila siku ya wananchi.
Mazingira safi
yanamaanisha afya bora, heshima ya makazi na maendeleo ya jamii, lakini pale
ambapo mifumo ya usimamizi haieleweki, wananchi hubeba mzigo ambao haukupaswa.
Majadiliano
yaliyowakutanisha masheha, wahamasishaji wa jamii na wataalamu wa Baraza la
Manispaa Mjini, yameonesha wazi kuwa changamoto za usafi wa mazingira bado
zinahitaji mshikamano.
Methali isemayo,
"Kidole kimoja hakivunji chawa," inaakisi hali halisi ya mapambano
dhidi ya uchafu wa mazingira.
MGONGANO WA
MAMLAKA KATIKA UKUSANYAJI WA TAKA
Moja ya hoja
zilizojitokeza kwa uzito mkubwa ni mgongano wa mamlaka katika ukusanyaji wa
taka ndani ya shehia ya Mchangani.
Kwa mujibu wa sheha
Nassir Mohammed Ali, wananchi wanakabiliwa na hali ya kuchanganyikiwa, kutokana
na taasisi mbili, Baraza la Manispaa Mjini na Mamlaka ya Mji Mkongwe, kufanya
kazi katika eneo moja huku kila moja ikikusanya malipo yake.
Wananchi
wanajiuliza kwa haki kabisa, wamlipie nani, wakati taasisi moja inadai malipo
ya kiwango fulani kwa mwezi, taasisi nyingine nayo inawafuata wananchi haohao
kwa madai mengine.
‘’Mwisho wa
siku, mzigo unabaki kwa mwananchi, ambao ni wanyonge na wenye kipato cha
chini,’’anasema.
Anasema hali hiyo,
imeongeza malalamiko na kupunguza imani ya wananchi, katika mfumo wa utoaji wa
huduma.
Kilichosisitizwa
zaidi ni umuhimu wa taasisi hizo kukaa pamoja, kuweka mipaka ya kiutendaji na
kuzungumza kwa sauti moja, ili kuondoa mkanganyiko unaowakabili wananchi.
Sheria ya
Serikali za Mitaa pamoja na misingi ya utawala bora, inasisitiza ushirikishwaji
wa wananchi na viongozi wa maeneo husika, katika maamuzi yanayohusu maendeleo
yao.
Ushirikishwaji
hujenga uwazi, huondoa migogoro na kuongeza uwajibikaji.
Maamuzi
yasiyoshirikisha wadau mara nyingi huishia kuzalisha migogoro na mifarakano
ndani ya jamii.
Mshiriki wa
kikao hichon Ali Khami Mtumweni anasema licha ya vijana kupita nyumba kwa
nyumba kukusanya taka, bado wananchi hawajui wanafanya kazi chini ya taasisi
ipi.
Anaeleza kuwa,
wakati mwingine vijana hao husema wameitwa na Manispaa, wakati mwingine
wameitwa na Mji Mkongwe, anaona hilo sio sahihi.
VIZIMBA VYA
KISASA VYA TAKA NI HATUA NZURI
Suala la ujenzi
wa vizimba vya kisasa vya kuhifadhi taka lilizungumzwa kwa kina, kwenye
majadiliano hayo.
Masheha
walikubaliana kuwa, maeneo mengi ya Mji Mkongwe, hayana nafasi ya kutosha
kutokana na msongamano mkubwa wa nyumba.
Wanasema
washiriki wa majadiliano hayo kuwa, kwa upande mwingine, maeneo ya Mwembeladu
na sehemu nyingine za pembezoni, bado yana nafasi zinazoweza kutumika.
Hii inaonesha
kuwa suluhisho moja haliwezi kutumika kila mahali. Kila eneo linahitaji mpango
unaozingatia hali yake ya kijiografia.
MAPENDEKEZO YA
MAGARI MADOGO YA UKUSANYAJI TAKA
Miongoni mwa
mapendekezo yaliyopokelewa vizuri ni matumizi ya magari madogo yanayopita usiku
au alfajiri kukusanya taka moja kwa moja kutoka kwa wananchi.
Magari hayo
yanaweza kutumia vipaza sauti kuwatangazia wananchi kutoa taka kwa wakati
maalumu.
Mfumo huu
unapunguza muda ambao taka hukaa mbele ya nyumba na kupunguza uwezekano wa
kusambaza harufu mbaya pamoja na magonjwa. Ni mfano wa ubunifu unaoweza
kusaidia hasa maeneo yenye msongamano mkubwa.
MITARO YA MAJI
MACHAFU BADO NI CHANGAMOTO
Mbali na taka
ngumu, changamoto nyingine kubwa ni mifereji ya maji machafu.
Baadhi ya
mifereji husafishwa na mingine huachwa kwa muda mrefu hadi kufunikwa na magugu
pamoja na uchafu unaosukumwa wakati wa mvua.
Kutokana na
hali hiyo, maji hushindwa kupita vizuri na kuongeza hatari ya mafuriko pamoja
na kuzaliana kwa wadudu wanaosababisha magonjwa. Mazingira haya yanahitaji usimamizi endelevu
badala ya kusubiri hadi pale kunapotokea dharura.
UHAMASISHAJI WA
JAMII UMEANZA KULETA MABADILIKO
Fatma Khamis
Ali, mhamasishaji wa jamii kupitia mradi unaotekelezwa na TAMWA, ZAFELA,
JUWAUZA na PEGAO, alieleza namna wananchi walivyoanza kushiriki kutatua
changamoto zinazowazunguka. Kupitia
kamati za wananchi, baadhi ya kero zimeanza kupatiwa ufumbuzi bila kusubiri
maamuzi kutoka ngazi za juu pekee.
Katika Shehia
ya Kikwajuni, suala la usafi wa mazingira lilifuatiliwa kwa kushirikiana na
Manispaa. Katika Shehia ya Kwahani,
tatizo la maji yaliyokuwa yanatiririka kutoka kwenye nyumba mpya lilifuatiliwa
na kupatiwa suluhisho kupitia ushirikiano kati ya wananchi, sheha na Shirika la
Nyumba.
Aidha, kampeni
dhidi ya utoro wa wanafunzi zimeonesha mafanikio kwa kupunguza idadi ya watoto
wanaokosa kuhudhuria masomo. Hii ni
ishara kuwa pale wananchi wanapopewa nafasi ya kushiriki, maendeleo yanakuwa ya
kudumu.
WANAWAKE NA
WATU WENYE ULEMAVU WANAONGEZA USHIRIKI WAO KATIKA UONGOZI
Mradi huo pia
umeongeza mwamko kwa wanawake kushiriki katika nafasi za uongozi.
Wanawake wengi
wamejitokeza kuwania nafasi mbalimbali za kisiasa badala ya kusubiri uteuzi wa
viti maalumu.
Hatua hii
inaendana na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 pamoja na Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, ambazo zinatambua haki ya usawa, ushiriki
wa wananchi na kutobaguliwa katika masuala ya uongozi na maendeleo.
Aidha,
inaendana pia na malengo ya usawa wa kijinsia yaliyoainishwa katika Dira ya
Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa ya mwaka 2030.
MTARO WA
KWAALINATU BADO UNAHITAJI NGUVU ZA PAMOJA
Sheha wa
Kwaalinatu, Salum Shabaan Mzee, alieleza kuwa pamoja na jitihada za wananchi
kusafisha mtaro mara kwa mara, bado changamoto hiyo ni kubwa. Alibainisha kuwa ukosefu wa vifaa vya kazi
unafanya juhudi za wananchi kuwa ngumu zaidi.
Hii inaonesha
kuwa ushiriki wa wananchi pekee hautoshi bila kuwepo msaada wa taasisi
zinazohusika.
MAAJAA YALIYO
KARIBU NA MAKAZI NI KERO YA MUDA MREFU
Mhamasishaji
Ismail Khamis Akhui alieleza kuwa katika maeneo ya Kwahani, Jang'ombe na
Kikwajuni wananchi bado wanaishi karibu sana na maeneo ya kutupa taka.
Hali hiyo
inaleta wasiwasi wa kiafya hasa kwa watoto pamoja na familia zinazozunguka
maeneo hayo. Wananchi wanahitaji kuona
maboresho yanayoonekana kwa macho badala ya kuendelea kuishi karibu na taka kwa
miaka mingi.
MPANGO WA
MANISPAA KUHUSU VIZIMBA VYA KISASA
Afisa Mazingira
wa Baraza la Manispaa Mjini, Ikrima Jumanne Khamis, alifafanua kuwa mwaka 2018
Manispaa ilipata ufadhili kutoka Benki ya Dunia uliowezesha kujengwa vituo 73
vya taka.
Baadhi ya vituo
hivyo viliondolewa kutokana na kupisha miradi ya maendeleo au kukosa sifa za
kuendelea kuwepo karibu na makazi ya watu.
Kwa sasa,
kupitia mradi wa BIG-Z, unaotekelezwa kwa kushirikiana na kampuni husika,
Manispaa inaendelea kujenga vizimba vya kisasa vitakavyoficha taka na kupunguza
uchafu unaoonekana wazi. Lengo ni
kuboresha usimamizi wa taka huku ikipunguza athari kwa afya ya jamii.
Hata hivyo,
Manispaa imeeleza kuwa bado inakabiliwa na changamoto ya uhaba wa magari ya
kutosha kwa ajili ya kukusanya taka moja kwa moja kutoka kwenye nyumba za
wananchi.
SHERIA ZINASEMA
NINI?
Masuala ya
usimamizi wa taka na afya ya mazingira yanatambuliwa katika Sheria ya Afya ya
Jamii ya Zanzibar, Na. 11 ya mwaka 2023, ambayo inaweka wajibu wa kulinda afya
ya jamii kwa kuhakikisha mazingira yanakuwa safi na salama.
Pia, Sheria ya
Serikali za Mitaa ya Zanzibar, Na. 7 ya mwaka 2014, inazipa mamlaka serikali za
mitaa kusimamia usafi wa mazingira, ukusanyaji wa taka na utoaji wa huduma kwa
wananchi kwa kuzingatia uwazi na ushirikishwaji.
Kwa upande wa
mazingira, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya Zanzibar, Na. 3 ya mwaka 2015,
inasisitiza wajibu wa taasisi na wananchi kushirikiana kulinda mazingira na
kuzuia uchafuzi unaoweza kuhatarisha afya za watu.
Sheria hizi
zinatoa msingi wa kuhakikisha kila taasisi inawajibika ndani ya mipaka yake na
wananchi wanapata huduma bora bila kubebeshwa migongano ya kiutawala.
MWISHO
Kauli za
masheha, wahamasishaji wa jamii na wataalamu zimeonesha jambo moja muhimu:
changamoto nyingi hazikosekani kwa sababu ya ukosefu wa nia, bali mara nyingi
husababishwa na ukosefu wa uratibu.
Wananchi wanahitaji huduma iliyo wazi, inayotabirika na isiyowalazimisha
kulipa mara mbili kwa huduma moja.
Pale taasisi
zinaposhirikiana, viongozi wanaposhirikisha wananchi na jamii inapopewa nafasi
ya kushiriki katika maamuzi, hata changamoto kubwa hupata ufumbuzi. Kama isemavyo methali ya Kiswahili,
"Umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu." Huu ndio msingi wa kujenga
miji safi, afya bora na jamii yenye maendeleo endelevu. Usafi wa mazingira si
jukumu la taasisi pekee, bali ni wajibu wa kila mmoja wetu.

Comments
Post a Comment