Skip to main content

'NGUVU MOJA' USHIRIKA WA WATU WENYE ULEMAVU PEMBA, WALIA KUFANYIWA UKATILI WA KIUCHUMI

 


 NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@

UMEWAHI kuwaza maisha bila kuona, kusikia, kusema au kusimama.

Basi hayo ndio maisha ya kila siku ya watu, wenye ulemavu, aidha wa viungo, uoni, uziwi na aina nyengine.

Lakini watu wenye ulemavu ni sawa na watu wengine, wanahaki zote za msingi, kama ilivyo kwa wengine.

Miongoni mwa haki hizo ni kushiriki katika shughuli za kiuchumi, kama ilivyoelezwa katika mikataba na sheria mbalimbali.

Mkataba wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu wa 2006, ambao ibara yake ya 27 (f) inasisitiza ushiriki na ushirikishwaji wao kiuchumi.

“Nchi wanachama wakuze fursa za watu wenye ulemavu kujiajiri, kuanzisha na kuendesha shughuli za ujasiamali, vyama vya ushirika na mtu binafsi kuanzisha biashara zake”, inaeleza sehemu ya mkataba huo.

Sheria ya watu wenye ulemavu ya Zanzibar nambari 8 ya mwaka 2022, kifungu cha 28 (e) inaeleza, watu wenye ulemavu wanastahiki haki zote za msingi za kibinaadamu sawa nawatu wengine ikiwemo kujitegemea na kujumuishwa katika shughuli za kijamii.

Katika hili Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekua ikifanya juhudi, katika kuwaendeza watu hao, hasa kupitia vikundi vyao vya ushirika na hata mtu mmoja mmoja.

Ikiwa ni kwa kuwapatia mikopo na mafunzo ya ujasiriamali, pamoja na kutetea haki zao za msingi kwa kuitaka jamii iwashirikishe katika fursa ambazo wanaziweza.

Hili limeonekana kwa wanaushirika wa kikundi cha watu wenye ulemavu wa aina mbali mbali kilichopo Tibirinzi Chake chake Pemba, kilicho wakusanya wenye ulemavu wa viungo, wasioona na Alibino.

Ambao kwa pamoja mwaka 2021, walijikusanya na kufikia idadi ya watu 23 na kujiita “Nguvu moja”.

Safari yao ilianza kwa kuwekeza kwenye kilimo cha migomba, ambapo walimiliki shamba yenye wastani wa  migomba 600.

Kutokana na kile baadhi yao walichokiita tabu na dhiki baadhi yao, walikata tamaa na kuishia njiani, na sasa kikundi kimebakiwa na watu 9 pekee wanawake 7 na wanaume wawili 2.

Wahenga walisema ‘Ng’ombe wa maskini hazai’, wakiwa na maana mtu, asiyenacho anaweza kutumia nguvu kutafuta na hata akipata alichotafuta hakidumu.




Kwani migomba yao hiyo, ilikumbwa na changamoto ya kuungua mithili ya iliochomwa moto na kupelekea kupungua uzalishaji.

Makamu Mwenyekiti wa kikundi hicho, Fatma Hafidh Suleiman anasema, hali hiyo iliwapa wakati mgumu kiuzalishaji na walipowafikia wataalamu wa kilimo waliwashauri, kuachana na kilimo hicho na badala yake waanzishe kilimo cha Mua, jambo lililowawia ugumu.

“Tulianza kwa kikilimo cha migomba tukapanda wastani wa migomba 600, ingawa ikaathiriwa na joto kali, ikawa kama ilioungua, wataalamu wakatushauri kubadilisha kilimo chengine, ila ilikuwa ngumu kwetu”, anahadithia.

Hapo ndipo upepo ulipobadilika, kutoka kwenye kilimo cha migomba na kuanza  biashara ya nguo, viatu, haliudi na mikoba ya kike.

Anaeleza walianza kwa mtaji wa Shilling 300,000 zilizotokana na uuzwaji wa ndizi, ambayo ilikuwa ni biashara yao tegemezi, tokea mwanzo.

Baadae ziliwazalishia hadi 500,000 kila baada ya mauzo, jambo lililowatia moyo na kuongeza, juhudi zaidi ya upambanaji.



Mjumbe wa kikundi hicho Zaitun Bakar Shante anasema, juhudi zao, ziliungwa mkono na serikali kupitia mkopo wa shilling milioni 2, kutoka Wakala wa uwezeshaji wananchi kiuchumi ‘ZEEA’, zilizo wawezesha kuongeza wingi wa bidhaa na kutanua soko lao.

“Baada ya ule mtaji wetu wa shilingi 300,000 tulikuwa tunazalisha wastani wa shilingi 500,000 kila baada ya mauzo, hapo ndipo ‘ZEEA’ wakatushika mkono kwa kutupatia mkopo wa shilingi million 2,” anaeleza.



Mshika fedha wao Raya Mohamed Nassor anasema, fedha hizo, walizitumia kwa kuongezea mtaji wao, ili kukuza biashara yao, kwani ilikuwa ni tegemeo lao kubwa katika kujiinua.

  MAFANIKIO

Katibu Faidha Said Kassim, anaeleza moja ya mafanikio walioyapata ni kupata fedha za kujikimu kimaisha, jambo ambalo halikuwepo kabla.

Jingine anasema wamefanikiwa kupata kushiriki na kushirikishwa katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Anaeleza walifanikiwa kuongeza mtaji, ambapo wamefika shilling million 1.5, iliowawezesha kupata wastani wa shilling million 2, kila baada ya mauzo.

Anafahamisha kati ya hizo hutoa pesa za mtaji, kulipa mkopo ‘ZEEA’, huweka hakiba kwa ajili ya uendeshaji shughuli za kikundi na nyingine kwa kujikimu.

“Mafanikio tulioyapata ni kupata fedha za kujikimu kimaisha, kupata kushiriki na kushirikishwa katika shughuli za kiuchumi na kuongeza mtaji wetu”, anaeleza.

Anasisitiza mafanikio hayo hayakuja kwa bahati mbaya, bali ni kwa uungwaji mkono wa serikali na wadau wa kupigania haki za watu wenye ulemavu, kwa kupatiwa mkopo wa shilling million 2.

Faidha mwenye ulemavu wa uoni anasema, kutokana na hatua waliopiga, walishapata mlango wa duka ambao unawawezesha kuuza bidhaa zao kwa utulivu.

 CHANGAMOTO WASIOISAHAU HII HAPA

Ghafla mambo yakabadika baada mtu asie thamini nguvu na juhudi za wengine, kubadilisha mzigo wenye bidhaa zao za biashara kama nguo, viatu na mikoba na kuacha mzigo wenye nafaka.

Kwakuwa wanaushirika hao wote ni wenye ulemavu na huchukua bidhaa zao nje ya kisiwa cha Pemba, walimchagua mmoja wa wanakikundi, kuwa ni mnunuaji bidhaa hizo.

Ambae ni Aisha Ali Abdallah na yeye ni mwenye ulemavu wa uoni, hufanya safari ya kwenda kuchukuwa bidhaa hizo kila pale inapo hitajika.

Aisha anaeleza siku moja, akiwa katika harakati hizo  mzigo wao wenye bidhaa zenye thamani ya shilling million 1.5 akiwa ndani ya meli, ulibadilishwa.

Anahadithia kwakuwa ni mwenye ulemavu wa uoni wakati msaidizi wake, kashamuingizia kwenye meli anarudi Pemba, alibadilishiwa mzigo wake na kupewa mzigo mwengine wenye nafaka.

 “Siku moja wakati narudi Dar-es-Salam kuchukua bidhaa za mauzo wakati wa kupakia bidhaa kwenye gari,  nilibadilishiwa mzigo, ambapo sikugundua hadi nilipofika nyumbani, hii ilitokea kwa kutokuwa na uwezo wa kuona,” anahadithia.

Anasema hili limesababisha kupoteza fedha zao za mtaji na biashara yao kuporomoka na maendeleo ya kikundi kwa ujumla.

Wanakikundi hao ambao ni wenye ulemavu kwa pamoja wanaomba wadau mbalimbali, kuwasaidia kutatua changamoto yao hiyo, kwa kuwapatia mtaji utakao wawezesha kuanza tena upya biashara yao.

Wanaeleza kwa sasa, hawana tena pakushika ni kama kibatali walichokitegemea kimezimika, kwani biashara yao hiyo, iliwasaidia kulipa mkopo uliobakia kuweka pamoja  na kujikwamua kiuchumi.



Wanafahamisha lengo la kuanzisha kikundi hicho, ni kujitengenezea mazingira ya kujipatia kipato, kujikwamua kiuchumi, ili kuepuka utegemezi.

Wanasisitiza kitendo hicho kimewarudisha nyuma kimaendeleo, hivyo wanaomba msaada zaidi ili kuanza upya.

  ZEEA

Wakala wa uwezeshaji wananchi kiuchumi ndio yenye jukumu la kuwawezesha wananchi kiuchumi kwa kuwapatia mikopo ya kujiendeleza.

Afisa habari wake Abdi Juma Suleimani anasema, kwa mujibu wa taratibu za ‘ZEEA’ watu wenye ulemavu wanahaki ya kupatiwa mkopo, kama ilivyo kwa wengine.

Ndio maana ZEEA kupitia program yake ya 4,4,2 ilishawapatia wajasiriamali wa kikundi hicho mkopo wa shilingi million 2, kwa mara ya kwanza.

Kwa mujibu wa hutuba ya bajeti ya wizra ya vijana kazi na uwekezaji kwa mwaka wa fedha 2024/2025 kupitia ‘ZEEA’ shilling 6,616, 166, 637.o3 zimetolewa kwa ajili ya wajasiriamali, ambapo kati ya hizo shillingi 1699, 288, 637 ni kwa wajasiriamali 969 wa Pemba.

Huku hutuba ya wizara hiyo ya mwaka wa fedha 2025/2026 ikileza  vipo  vikundi 380  ambapo Unguja ni  256 na Pemba 124,  vilivyopata mikopo kwa ajili ya kujiendeleza vikiwemo vya watu wenye ulemavu.

Aidha hutuba hiyo imeeleza Serikali kupitia ZEEA imetumia Shilling 12, 779, 637, 967, kuwawezesha wajasiriamali 6,135, ambapo shilling 1,581310, 263 zimetolewa kwa wajasiriamali wa Pemba pekee.

WADAU WA WATU WENYE ULEMAVU

Mratibu Baraza la taifa la watu wenye ulemavu Pemba Mashavu Juma Mabrouk anasema, bado kuna changamoto za watu wenye ulemavu kwenye eneo la kiuchumi.

Anahimiza uungwaji mkono kwa watu hao, katika masuala ya kiuchumi, ili waweze kujitegemea.

Anasisitiza elimu ya ujasiriamali pamoja na mikopo yenye masharti nafuu, ni suala muhimu katika kuhakikisha wanapata fursa za kujiendeleza kiuchumi, kama ilivyo kwa watu wengine.

Afisa watu wenye ulemavu Pemba wa “UWZ” Maryam Mohamed Salum anasema,  jamii iungemkono juhudi za serikali na watu wenye ulemavu za kujiendeleza kiuchumi, ili kuondoa utofauti wa kiuchumi uliopo.

TAMWA-Zanzibar inasisitiza jamii kuwa sehemu ya mapambano dhidi ya vitendo visivyo vya kiungwana kwa watu wenye ulemavu, huku wakihimiza kuwaunga mkono katika mapambano yao ya kichumi.

                               MWISHO

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

Vikausha damu vya mjamzito hivi hapa, umo mchele, udongo, mkaa, chaki Uwezekano wa kuzaliwa watoto wenye udumavu, utapiamlo ni mkubwa

  NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@ ‘’KILA ninapobeba mimba nimezoea kula mchele kwa wingi naweza kusamehe pilau au biriani,’’ ndio maneno ya mwanzao ya Bahati Mohamed Ali (sio jina lake halisi). Nilimfuma akiwa barazani kwake, mjini Ole wilaya ya Chake chake, pembeni yake akiwa na kibakuli cha mwazi, kwa umbali utaona amejaza chakula aina ya pepe, kumbe ni mchele wa Mbeya. Hujichotea kidogo kidogo na kuushindilia mdomoni mwake, huku akiendela kupiga storia na wenzake, bila ya kujali kuwa ujauzito alionayo na mchele huo hauna mwisho mwema. Kawaida yake akiwa mjamzito, kila anapoamka asubuhi anaroweka mchele upatao robo kilo hivi…na baada ya kumaliza kupika, yeye huchukua mchele wake kutafuna (kula). Wakati mwenza wake na watoto wao, wanakula chakula cha mchana, Bahati yeye hukaa pembeni na kibakuli chake cha mchele akiendelea kubahatisha afya yake. ‘’Mimba nyengine hupenda sana kutafuna mchele wa Mbea na nyengine hupenda mchele wa mapembe, kwa kweli huwa nina hamu (kileo), kwan...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...