NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
"UONGOZI sio cheo, ni matendo na
matokeo yanayobadilisha maisha ya watu" ni maneno ya wananchi wa shehia ya
Kendwa wilaya ya Mkoani.
Wanasema sheha wao ni mwanamke aliyethibitisha kuwa,
uongozi wa mwanamke una nguvu ya kubadilisha kabisa muelekeo wa jamii.
Wanakendwa ni kama wanaungana na Mkataba wa umoja wa
Mataifa wa kutokomeza aina zote za udhalilishaji (CEDAW) wa 1979 hasa ibara ya
7.
Ibara inayozitaka “Nchi wanachama zihakikishe
zinawapa wanawake fursa za kushiriki katika uongozi’’.
Aidha lengo namba 5.5 la maendeleo endelevu ‘SDGs’ ya
mwaka 2015 hadi 2030, lililozitaka nchi zote kuhakikisha ushiriki kamili wa
wanawake na fursa sawa za uongozi katika ngazi zote, iwe kisiasa, kiuchumi na
kijamii.
Pia Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ibara yake ya 21
(1) inayoeleza kila Mzanzibari anayo haki ya kushiriki katika shughuli za
utawala wa nchi, ama moja kwa moja au kwa kupitia Wawakilishi waliochaguliwa
kwa hiari.
Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya mwaka 2000
(ambayo ilihuishwa na kuzinduliwa rasmi kama Sera ya Taifa ya Jinsia na
Maendeleo ya Wanawake ya Mwaka 2023) inahimiza ushiriki wa wanawake katika
nafasi mbali mbali za uongozi.
Fursa hii imefika katika shehia ya Kendwa iliopo
wilaya ya Mkoa wa kusini Pemba.
Kama ilivyo kwa maeneo mengine ya Pemba, hupo pia watu
wake ni wakarimu, wenye umoja na
mshikamano.
Nyuma ya taswira hiyo, jamii ya wakaazi wa eneo hilo,
inasena kwa miaka mingi ilikabiliwa na changamoto nzito za kimaendeleo.
Ikiwa ni pamoja na ukosefu wa huduma za afya za
karibu, miundombinu duni ya elimu, maji safi na salama, na barabara
zisizopitika kwa urahisi.
Shida hizi zilidumu kwa miaka mingi, hadi
ilipofika mwaka 2021, mwaka ambao Fatma
Othman Pandu aliteuliwa kuwa sheha wa Shehia hiyo.
“Uteuzi wake haukuwa tu wa kujaza nafasi ya kiutawala,
bali ulikuwa mwanzo wa zama mpya za maendeleo jumuishi kwa wanakendwa,” maneno
ya Asha Khamis mkaazi wa Kendwa.
Anasema kwa kutumia mchanganyiko wa ujasiri,
ushawishi, na ushirikishaji wa jamii, sheha wake, amethibitisha kuwa, uongozi
wa mwanamke ni nguzo imara ya mabadiliko ya kijamii.
Mohamed Haji Mohamed, anasema ukitaka kujua kuwa
wanawake wanaweza kuongoza, utembelee shehia yao na hilo litadhirika kwa
vitendo.
Maryam Haji Omar, anasema wao ndani ya shehia hiyo,
damhawana tena shida ya huduma za afya na hasa za mama na mtoto.
‘’Hatusemi kuwa alitoa fedha zake mfukoni, lakini kero
zake kwa serikali kuu, tunajivunia uongozi wake, maana hata miundombinu ya
elimu imeirika,’’anasema.
YEYE NI NANI HASA?
Jina lake ni Fatma Othman Pandu, mzaliwa wa Kendwa
wilaya ya Mkoani kusini Pemba.
Aliepata elimu yake ya msingi, skuli ya Kangani
kuanzia mwaka 1980 hadi 1987, alipomaliza darasa la nane, na kujiunga skuli ya elimu ya sekondari skuli
ya Kendwa 1988 hadi alipomaliza kidato cha tatu mwaka 1990.
Kwa vile alikua ni mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi,
mwenyewe anasema baada ya kumaliza masomo yake, alijiingiza katika harakati za
kukitumikia chama.
Alikitumikia chama kama mwana chama wa kawaida, hadi
mwaka 1994, ambapo aligombea ukatibu wa umoja wa wanawake ‘UWT’ wa tawi la
Kendwa, na kupata nafasi hiyo, kwa idadi
kubwa ya kura.
“Nilianza kua kiongozi nipomaliza skuli kwa kushika
nafasi kama uongozi wa darasa, Naibu waziri wa mazingira, na nilipomaliza
kusoma, nilipoanza harakati za
kukitumikia chama hadi 1994
nikachaguliwa kua Katibu wa UWT jimbo la Kendwa,”anaeleza.
Anahadithia nafasi hio aliitumikia hadi mwaka 2021,
ambapo aliteuliwa kuwa sheha wa Kendawa, ingawa kabla ya kushika nafasi hiyo,
alikua msaidizi wa sheha.
Katika hili, mtoto wake Fatma aitwae Othman Ali
anasema hata kabla ya kua sheha, mama yake alikua ni mwenye kujitolea na
kuitumikia jamii kwa moyo mmoja.
Hilo liliwafanya familia na wanakendwa kumuamini,
kumkubali na kumshirikisha katika masuala mbalimbali ya kimaendeleo.
Kwa miaka sita sasa, Fatma ni sheha, na mwanamke wa
pili kushika nafasi hiyo katika historia ya shehia yao, baada ya mtangulizi
wake Sabiha Mohamed Ali.
Na ni mmoja kati ya masheha 36 wa wilaya ya
Mkoani, yenye masheha wanawake 13 na
wanaume 23.
Ilioiwacha nyuma wilaya ya Chake chake yenye masheha
wanawake nane na wanaume 24 kati ya masheha 32.
Idadi inayofanya Mkoa wa Kusini Pemba kua na masheha
68, wakiwemo wanaume 47 na wanawake 21, takwimu zilizotolewa na Mkuu wa Mkoa wa
Kusini Pemba Rashid Hadid Rashid.
Mwenyewe anasema, haikua rahisi kwake kukubali kama
yeye ni kiongozi, baada ya kupewa nafasi hiyo, kutokana na kukosa mafunzo ya
kutosha, juu ya uongozi, huku hofu yake
ikiwa atawezaje kuisimamia jamii yote.
“…..ahhh, haikua rahisi kwakukukubali kwamba ningeweza
kuongoza na kuiletea jamii yangu maendeleo, sikua naamini juu ya uwezo wangu,
ingawa walionizunguka waliniamini”. anaeleza.
Kwa sasa yeye ni hazina na tunu ya wanakendwa,
kwani kwa juhudi zake na mashirikiano
na wananchi ameizawadia Kendwa mambo mbali mbali ya kimaendeleo.
AMEIFANYIA NINI KENDWA
Wananchi wa shehia ya Kendwa wanasema, awali walipata
tabu kupata huduma za afya, hasa kwa wajawazito na watoto.
Mmoja wa wananchi hao Rehema Ussi Juma anaeleza,
walilazimika kwenda Hospitali ya Abdaulla Mzee Mkoani, kufuata huduma za msingi za mama na mtoto,
wakati wa kujifungua, hii ilihatarisha maisha ya wengi wakati wa
dharura.
Anaeleza kipindi ambacho Fatma amekua sheha, hilo
lilikua kipaumbele cha kwanza, kwani alifanya juhudi za kuomba ujenzi wa kutuo
kipya cha afya.
Hadi pale viongozi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii
Tanzania ‘TASAF’ walipowapa fursa ya kuchagua mradi wa maendeleo, na kuchagua
ujenzi wa kituo cha afya.
“Juhudi za sheha hazikuishia hapo, sisi nayeye
tulishirikiana kushika pauro, sururu na jembe kuchimba misingi na kukoroga zege
na saruji, hadi kituo cha afya kiloposimama na sasa tunapata huduma
nzuri,’’anaeleza.
Na leo hii kinamama wa Kendwa, wanajifungulia katika
mazingira salama na yenye staha, jambo linalowapa faraja.
Wanaendelea kusema, miundombinu ya
skuli katika shehia hiyo kwa sasa ni
yenye ubora, tofauti na zamani, ambapo ilikuwa finyu na yenye uchakavu mkubwa.
Mwananchi Saleh Mussa Alawi anasema, kwenye hili
pia Sheha Fatma alijitahidi kufuatilia
na kuiomba serikali ujenzi na ukarabati wa skuli, ili kuondoa changamoto
zilizokuwepo.
“Kwasasa Kendwa, kuna skuli maalumu kwa ajili ya
wanafunzi wa mchepuo wa sayansi na kilimo, yenye miundombinu yote muhimu ya
kufundishia, na kujifunzia, watoto wetu wanasomea maabara ya Kompyuta na
majengo yenye hadhi,” anaeleza.
Wananchi wanasema sheha wao pia, alianzisha mikutano
ya mara kwa mara na wazazi na walezi, ili kusisitiza umuhimu wa elimu, hasa kwa
mtoto wa kike, hatua iliyopunguza viwango vya wanafunzi kuacha masomo.
Si hayo tu, Juma Mohamed Said wa Kendwa
anasema, katika sekta ya huduma ya maji safi na salama, sheha wao hakukaa ndio maana, alipoona uwepo wa
changamoto hiyo.
Alifanya juhudi za kumfikia Mbungea na Mwakilishi, nao
kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji Zanzibar ‘ZAWA’ wakajenga visima viwili,
vyenye uwezo mkubwa wa kusambaza maji, katika vitongoji vyote vya shehia hiyo
na sasa changamoto hiyo imebaki stori tu.
Kendwa ni eneo lenye shughuli nyingi za kiuchumi,
ikiwemo biashara na kilimo, na wakaazi
wake husafirisha bidhaa na mazao ya kilimo, kila siku.
Maryam Hassan Salim wa Kendwa anasema miundombinu ya
barabara za ndani kwa miaka mingi iliopita ilikuwa katika hali duni.
Anaeleza wakati wa mvua, barabara hizo zilijaa tope na
maji, na kufanya usafiri kuwa wa shida kwa wakaazi wake.
Anahadithia, barabara ya mwanzo ya ndani kujengwa
Kendwa ilikua sheha Fatma aliomba msaada wa kifusi kilichomwagwa na baadae,
serikali kuu sasa imeshaijenga kwa lami.
Sheha huyo, amefanikiwa kushajihisha wananchi kuunda
vikundi vya ujasiriamali, vinavyojishughulisha na kazi mbalimbali,
ambavyovimefanikiwa kupiga hatua za kimaeneleo.
NJE NA USHEHA
Fatma Othman Pandu ni mke na mama wa watoto sita,
anaetimiza majukumu yake ya kuilea familia, bila kuathiri upande wowote.
Ni mkulima na mfugaji anaeamini kwamba “mtaji wa
masikini ni nguvu zake” wenye maana kwamba kujituma ni njia pekee ya kupata ukitakacho.
Ni msuluhishi mzuri wa migogoro ya kifamilia, “Napenda
sana kua mpatanishi, na jamii yangu inanitumia vizuri kwenye hili.
Anawasihi wanawake wawajibike kutendea kazi nafasi na
nyadhifa wanazopata, ili kuondoa dhana za kwamba mwanamke hawezi.
Ali Omar ni muume wa sheha huyo, anasema imani yake ni
kwamba, mwanamke anahaki ya kua kiongaozi, na ni mwenye uwezo mkubwa kwenye
hili.
Anaihakikishia jamii, kumpa moyo na ushauri wenye
kujenga kila siku, ili azidi kua imara na mwenye mafanikio katika nyadhifa hio.
Anaeleza kiu yake ni kuona watoto wake hasa wa kike,
hawako nyuma katika uongozi, jambo analoanza kulijenga hivi sasa.
MITANDAO YA KIJAMII
Kwa mujibu wa mitandao ya kijamii uwakilishi wa
wanawake katika uongozi wa ngazi za chini ni mdogo ikilinganishwa na ngazi za juu za kitaifa.
Takwimu za kimtandao zinaonyesha ni wastani wa asilimia 2.1 katika ngazi za
vijiji.
Huku ikisisitza mitazamo ya Jamii na imani potofu za
kijinsia kuhusu uwezo wa wanawake kuongoza katika ngazi za misingi ya jamii
ndio sababu ya hali hio.
MWISHO
.jpg)


Comments
Post a Comment