-Asema, changamoto ya kifedha inawarudisha nyuma kwenye kazi zao
NA ZUHURA JUMA, PEMBA
KHAMIS Ali Omar (32), umaarufu ‘dongo’, ni mkaazi
wa Kambini Kichokochwe wilaya ya Wete Pemba.
Yeye ni msanii wa kizazi kipya mwenye ndoto za kufika mbali kwenye
uigizaji wake.
Alianza fani hiyo
mwaka 2017, wakati huo haikuwa moyoni mwake, wala haikuwa katika malengo yake
aliyojiwekwea kwenye maisha.
Kipindi hicho alikuwa
kwenye kikundi cha mchezo wa sarakasi cha 'Kambini Art Group',
hivyo kulikuwa na maonyesho yanayofanyika kila mwezi wa mwisho kabla ya kuingia
kwenye funga, kijijini kwao, ambapo walikutana na vikundi mbalimbali ikiwemo
vya uigizaji.
"Hapa kwetu kila
mwaka mwezi wa ‘mrisho’, (siku moja kabla ya ramadhan),
kulikuwa kunafanyika onesho 'show', hivyo vikundi mbalimbali vya
burudani vilialikwa na kuonyesha vipaji vyetu," anaeleza Dongo.
Wakati wapo kwenye
sarakasi, mmoja wao alizaa wazo la kutaka kuigiza, ambalo halikupingwa kwenye
kikundi chao, wakati huo akiwa ni Katibu wa kikundi hicho.
Baadae ya kukubaliana,
kwa mara ya kwanza waliigiza mchezo unaoitwa 'Haidar' ambapo yeye
ndie aliebeba uhusika mkuu aliekuwa akiitwa 'Haidar'.
Walicheza vizuri filamu
hiyo, kiasi ambacho kiliwapatia umaarufu kikundi chao hicho na yeye mwenyewe
binafsi.
Anafafanua, walitoa kazi
mbili na ya tatu iliharibika, ambapo aliekuwa akiwatungia maudhui hayo ni
mwalimu Mussa Hamad Said, ambae fani yake hasa ni daktari wa binadamu.
Walizowea kumwita
mwalimu, kutokana na kuwafundisha kwake, hivyo wakampa heshima hiyo kubwa.
Dongo anaeleza, waigizaji
wengi maarufu na wakongwe walianza kuwatafuta ili kuunganisha nguvu za pamoja,
na kuona wanakuwa vizuri katika soko la filamu.
Anahadithia kuwa, hata
muigizaji maarufu anaejulikana kwa jina la 'Mau Mpemba' alipoona
filamu zao hizo, alifika kisiwani Pemba kuwaunga mkono, ambapo walianza kuigiza
klipu ya samaki ya vichekesho.
"Mau’ baada ya
kutuona vijana wa kwao tunaigiza, wakati huo yeye ameshasonga mbele kiuigizaji,
aliamua kuja kutuunga mkono, tulifurahia sana hatua hii," anasimulia
Dongo.
Kwa sasa Mau
akiwahitaji katika kazi zake anawaita Unguja kusaidiana, hivyo hawakupitia
changamoto kubwa ya kupata umaarufu wala kujijengea jina.
Kutokana na vipaji
vyao kuwa vizuri na kuivutia jamii, pia walifuatwa na kikundi cha 'Jufe
Film' ili waunganishe nguvu za pamoja, zitakazowafikisha mbali katika
soko la uigizaji.
"Na kweli
tumefika mbali kidogo, ingawa sipo tunapopataka, lakini tumesogea mbele, hivyo
tunaendelea kupambana ili kutimiza lengo letu," anafafanua.
Akiwa kwenye kikundi
cha 'Jufe Film', kwa mara ya kwanza Dongo, aliigiza kwenye filamu ya 'Mwizi
wa Futari' ambayo ilipata mashabiki wengi na kuendelea kupata umaarufu.
Walifanya kazi
nyengine ambayo iliharibika na haikutoka, jambo ambalo liliwatia hasara ya
zaidi ya shilingi 400,000.
"Lakini
tulichukulia ni jambo la kawaida, kwani hakuna kazi inayokosa changamoto, kwa
sababu kuna baadhi yetu walikata tamaa kabisa," anasema.
Anasema, changamoto
haikuwa ndogo sana kwa sababu pesa hiyo ilikuwa ni ya wapigaji picha tu, kwani
mambo mengine wanafanya wenyewe zaidi kwa kujitolea.
Baada ya kuharibika
filamu hiyo, waigizaji wengi kwenye kikundi chao cha mwanzo, waliondoka kwenye sanaa,
na kubakia yeye, Naomba, Goro na marehemu Bikidecha.
Filamu nyengine na
clipu walizoigiza ni pamoja na Nyumba moja, Skujua, Wahuni si watu wazuri, Mke
wa ngomani, Mume wa mjini, Figo, Marejeo na kwa nini Ramadhani.
Kuna mafanikio mengi
aliyoyapata katika fani ya uigizaji, ikiwa ni pamoja na kupata heshima na
kujuana na watu mbalimbali, hali ambayo inamsaidia kufanya kazi zake kwa
urahisi.
Pia wanapata mahitaji
ya familia ingawa hayakidhi haja, lakini sio kama kukosa moja kwa moja, hivyo
anajishugulisha na kazi nyengine ili kujipatia kipato.
Kwenye jamii asilimia
kubwa ya wananchi inamkubali Dongo, isipokuwa changamoto kidogo ni kwa wasanii wenzao
wakike, kwa sababu mwanzo walipata shida sana kwa kuonekana wahuni na wasio na
heshima.
"Changamoto
zinazotukabili ni kutokuungwa mkono (support) kwa sababu zamani
tulikuwa tunatoa ‘CD’ lakini kwa sasa hazinunuliwi, lazima
tutumie mitandao ya kijamii," anaeleza.
Tena jambo hilo inawapa
shida kwa sababu ili wapate malipo kidogo wanatakiwa kuwa na ‘subscribe’ nyingi
na kutuma kazi zao kila siku, jambo ambalo ni ngumu kwani hawana fedha za
kutengeneza.
Ukosefu wa vitendea
kazi, hivyo wanalazimika kukodi vifaa, hali ambayo inazidi kuwaongezea gharama
kila wanapoigiza.
"Wadhamini
wanajitokeza kiasi, wakati mwengine tukiona kimya sana tunawafuata wao, hali ambayo
inasababisha kuwa kama wametununua,’’anasema.
Anaomba waungwe mkono kwenye
kazi yao, ili wapate soko kama wasanii wenzao wa Bara, kwani hawaumizi vichwa
sana kutokana na soko lao ni zuri.
Dongo anaiomba serikali
iwasaidie kupeleka kazi yao katika chombo cha habari cha jamii (ZBC), kwani
juhudi zao ziligonga mwamba walipokwenda kutafuta msaada.
"Ikiwa tutaungwa
mkono basi itakuwa na sisi tumejiajiri vizuri, kwa sababu tutapata pesa ya mahitaji
yetu angalau ya muhimu," anahadithia.
Anasema, wameona
kwamba, Shirika hilo kwa sasa limeboreshwa na kwa vile filamu zao zinapendwa
sana, basi ikiwa zitarushwa hata watazamaji wataongezeka.
"Kutengeneza filamu
mpaka kumaliza ni gharama kubwa, kwa sababu, lazima tuweka kambi, kula, usafiri,
hivyo kwa vile ni wenyewe kwa wenyewe tunabebana tu," anaeleza.
Hivyo kwa vile ni wao
wenyewe, filamu moja hutumia zisizopungua shilingi milioni saba kwa kujibana.
Wakati mwengine inawalazimu
watafute wasanii nje ya Zanzibar, hivyo wanatumia gharama kubwa zaidi mpaka
kumaliza.
Hivi karibuni
waliongeza nguvu na wasanii wa Bara, ambapo walitumia mwezi mmoja na
hawajamaliza, hivyo walitumia gharama za shilingi milioni nane.
"Hiyo ni ya ‘episode’,
kwa hiyo tumeiacha uporo kwa sababu hatuna pesa ya kuendeleza, na tulicheza
kisiwani Unguja kutokana na kuwa tungewaleta Pemba gharama ingezidi,"
anaeleza.
Waliipeleka kazi yao
hiyo kwenye kituo cha AZAM TV ili wapate gharama, angalau nusu kwa ajili ya
kwenda kumalizia, ingawa waliambiwa wamalizie kwanza ndipo waipeleke.
"Walituambia siku
hizi hawapokei tena kazi nusu kwa sababu, baadhi ya vikundi wakishakupewa pesa
tu wanakimbia, hivyo wameshaibiwa sana," anasema.
Anaeleza kuwa,
wanaendelea kutafuta wadhamini ili wamalizie kazi yao, ambapo wangepata pesa
ndani ya miezi miwili wangemaliza yote.
Na wao pia wamekuwa
wakichukuliwa kwenda kuongeza nguvu kwenye filamu za Bara, ambapo hivi karibuni
walikwenda Lushoto na walitumia mwezi mmoja kwa episode 20.
‘’Tupo tuliosomea fani mbalimbali lakini hatuna ajira rasmi, hivyo kupata fedha ya kuendeleza shughuli zetu za uigizaji ni ngumu sana, tunahitaji msaada," anaeleza.
Mdogo wake Dongo
mkaazi wa Kambini, Said Ali Omar (Goro) anamuelezea kaka yake kwenye fani ya
uigizaji kwamba, ni kijana anaefanya vizuri ambae anashirikiana na waigizaji
wenzake vizuri na hata kwenye jamii.
‘’Yeye ni mkarimu sana
kwa sababu hata akitafutwa na wanafunzi wa skuli kutaka waigize nae hapingi, bali
anashirikiana nao na wanafanya vizuri, hivyo jamii inampenda sana,’’ anaeleza.
Anasema kuwa, familia
yake wanampa ushirikiano huku wakimnasihi kwamba aendelee kupambana kwani
hakuna mafanikio yanayokuja kwa urahisi.
‘’Kila jambo mwanzo
unakuwa mgumu, hivyo na yeye ipo siku atavuna matunda mazuri, muhimu asirudi
nyuma kwa changamoto anazopitia,’ anaeleza.
Amina Hamad Ali
(Naomba) mkaazi wa Ole ambae ni msanii mwenzake anasema, anamfahamu Dongo
kwamba ni mpambanaji na ni msanii asie na shida, hivyo kila mmoja yupo karibu
nae.
Anasema kuwa, yeye
alimkuta katika fani hiyo ya uigizaji kwa sababu aliingia mwazo, ingawa
mashirikiano anayoyapata anafarijika sana, kwani yanamjenga kuwa bora kila siku
zinaposonga mbele.
‘’Dongo namfahamu sana
kwa sababu nimekuwa nae kwa muda mrefu sasa kwenye uigizaji, anapambania kazi
zake vizuri, hana shida na mtu, na anajitolea sana kwa wenzake,’’ anasema
Naomba.
Mwenyekiti na
Mwanzilishi wa kikundi cha Uigizaji cha ‘Jufe Film’ Pemba, Mohamed Yussuf Hemed
anasema, alimjua msanii huyo tangu akiwa bado hajawa maarufu sana kwenye fani
ya uigizaji.
Anaeleza kwamba, baada
ya kumuona kwenye filamu ya Haidar, walimfuata na kuja kusajili rasmi kwenye
kikundi chao na kuanza kufanya nae kazi.
‘’Kwa kweli Dongo ni
mzuri sana kwenye kazi kwa sababu anaipenda sana kazi yake na ukimpangia sini
yeyote anacheza bila kusita,’’ anaeleza.
Anahadithia kwa,
msanii huyo yupo tayari muda wowote kwa kazi, hivyo anapopigiwa simu anakuja
haraka na anashirikiana na wenzake kwa kila jambo.
‘’Kwa kweli siwezi
kuyamaliza kuyataja mazuri yake kwa sababu, sio mvivu na yupo tayari kwa chochote
kwenye uzalishaji (production), hata umwambie afanye kazi gani anafanya na kubeba
vifaa, hajali kuwa amekuja kwa uigizaji tu,’’ anasema.
Msanii huyo ana mke na
watoto watatu, ambae alipata elimu yake ya msingi katika skuli ya Mchangamdogo
na kumalizia kidato cha nne katika skuli ya Sekondari Mchangamdogo.
Dongo hakuwa nyuma
kujiendeleza na elimu ya juu ambapo alisomea fani ya umeme katika chuo cha
Elimu Amali Vitongoji Wilaya ya Chake Chake Pemba.
MASHABIKI WA DONGO
Asha Khamis Hamad mkaazi
wa Wete anasema, yeye anapenda sana filamu anazoigiza Dongo, hasa za vichekesho
kwani anapoziangalia hata kama ana msongo wa mawazo, hunaondoka.
‘’Kwa kweli kipaji
chake ni kizuri, kwa sababu anaigiza kwenye vichekesho na kawaida, hivyo
inaoneshea anaweza kuigiza katika hali yeyote ile,’’ anasema.
Amina Makame wa Kiuyu
Minungwini anamsifia sana Dongo, katika uigizaji wake kwamba, anafurahisha hasa
pale anapovaa mavazi ambayo yanachekesha.
Bakar Hamad Juma
mkaazi wa Kambini anamtaja kuwa ni muigizaji mzuri, anaeweza kufika mbali kwenye
sanaa ya filamu, kwani kipaji chake ni cha kiwango cha juu.
‘’Tuna kipaji kizuri
pale, lakini kinachouwa vipaji vya wasanii Pemba, ni kukosa fedha za kufanyia sanaa
yao, maana, ili uwekeze fedha, badi uwe nazo,’’ anasema.
WIZARA INAFANYA NINI KUWASAIDIA WASANII
Mratibu wa Baraza la
Sanaa Pemba Seif Salim Mussa anasema, kuna fungu maalumu la kuwasaidia wasanii,
kwa kuwapatia elimu, vifaa na kuwatafitia fursa mbalimbali ikiwemo wadhamini.
‘’Wakifuata taratibu za
Baraza ketum kazi zao zinaonekana, kwa sababu ni lazima wawe na leseni, kwani vikundi
vya Sanaa, vinatakiwa vitambulike kwa kuwa na usajili pamoja na kuhakiki kazi
zao kwetu,’’ anafafanua.
Anasema, wanamipango
mingi, kuhakikisha wasanii hao wanaweza kujitegemea, hivyo wameandaa ‘ubunifu
wa kimkakati’ ambao unategemewa kuzinduliwa mwaka huu.
Katika ubunifu huo wa
kimkakati, wasanii wanatakiwa kutengeneza muongozo ‘script’ zao, na baada ya
kutoka tangazo la wizara, wanatakiwa waipeleke kwa ajili ya kufanyiwa kazi.
Anafafanua, lakini pia
walilishajiihisha ‘ZBC’ wachukue kazi za wasanii, angalau zioneshwe kwenye
kipindi maalumu cha sanaa, ili kukuza vipaji vyao.
‘’Ipo taasisi moja
inayohusika na kukuza vipaji Zanzibar, tulizungumza nayo na wakasema kuwa
watawasaidia na kuwachukua kwenye mashindano ya sanaa (ZIFF), na tumewaunganisha
wasanii,’’anafafanua.
MWISHO.





Comments
Post a Comment