NA SAIDA ALI, PEMBA@@@@
KAIMU Ofisa Mdhamini Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Pemba, Sharifa
Hamad Shapandu, amezitaka kamati za kufanikisha tamasha la 31 la utamaduni wa mzanzibari,
kuhakikisha zinafanyakazi kwa kushirikiana, ili kufanikisha tamasha hilo.
Ameyasema hayo August 18, 2026,
ofisini kwake Gombani Chakechake Pemba, mara baada ya kuzizindua kamati hizo
tano, kuelekea uzinduzi wa tamasha hilo mwishoni mwa mwezi ujao, kisiwani humo.
Alisema kuwa,
kuwepo kwa kamati hizo anataka iwe ni njia rahisi ya kufanikiwa kwa tamasha
hilo, ambalo kwa awamu hii, linatarajiwa kuwa la aina yake.
Alieleza kuwa, njia ya kuzigawa kwa kamati hizo, ni namna ya kuwa na na urahisi
wa ufuatuliaji, ingawa isiwe chanzo cha kukosa kushirikiana.
‘’Najua kuwa zipo
kamati tano, zinawajumbe wenye uwezo na maarifa yasiofanana, lakini hili sasa
muwe na ushirikiano kwa pamoja, ili kulifanikisha hili,’’alifafanua.
Aidha Kaimu Ofisa
Mdhamini huyo, amewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika tamasha hilo,
tangu kuanza kwa uzinduzi wake wilaya ya Micheweni, ili kujionea mambo
mbalimbali ikiwemo, utamaduni wa kizanzibar, michezo, maigizo na ngoma za
asili.
"Wananchi wote nawaomba mushiriki kikamilifu, katika tamasha hili la utamaduni
wa mzanzibari, ikiwa ni njia moja wapo ya kujionea utamaduni wetu na wingine
kujikumbusha,’’alieleza.
Mapema Mkuu wa
Divisheni na Utamaduni Pemba Hamad Ali Haji, alisema tamasha hilo litakuwa la
aina yake kwa mwaka huu, kwa kuvishirikisha zaidi ya vikundi 10 vya ngoma asili,
kutoka Unguja na Pemba.
Alisema, tangu
kuanzishwa kwa tamasha hilo, kwa mwaka huu, ambalo ni 31, kwa wanachi
watakaojitokeza wataniufaika na mambo makubwa, ikiwemo resi za ngalawa, Punda,
msewe wa zamani na sasa, taarab asilia na mbio za baiskeli.
‘’Kwa mwaka huu
wizara yetu ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, chini Waziri Riziki Pembe
Juma Khamis na Katibu Mkuu Matar, tamasha hili, litakuwa la kuvutia na si la
kukosa,’’alisisitiza.
Katika hatua nyingine,
alisema tamasha hilo kwa kuanzia, litazinduliwa Septemba 19 hadi 23 mwaka huu
kisiwani Pemba, wilaya ya Micheweni na mgeni rasmi akitarajiwa kuwa, Makamu wa
Pili wa Rais Zanzibar Hemed Suleiman Abdulla.
Alifafanua kuwa,
kwenye uzinduzi wa tamasha hilo, utafuatiwa na matembezi ya wajasiriamali, wasanii
wa ngoma za asili, utenzi na shamra shamra nyingine za kulipamba.
Siku ya pili,
tamasha litahamia wilaya ya Wete, litanogeshwa na maulidi ya home, nasheed,
dufu na maigizo yanayohusiana na tamaduni wa kiislam na kizanzibari.
‘’Wananchi wa
wilaya ya Wete, wanakaribishwa siku hiyo, ukumbi wa zamani wa baraza la Wawakilishi,
ambapo hakutakuwa na kiingilio,’’alisema.
Aidha Mkuu huyo wa Divisheni ya Utamaduni Pemba, alisema Septemba 21, kutakuwa
na mashindano ya ngalawa, yatakayoambatana na sarakasi na ngoma za asili Mkoani,
na siku inayofuata ni mchezo Ng'ombe uwanja Pujini.
‘’Niwaarifu wananchi wa Pemba, tamasha hili litahitimishwa
Septemba 23, kwa usiku wa sanaa, pamoja na wajasriliamali, wakionesha shughuli mbalimbali,
zikipambwa na kwa taarabu, uwanja wa Gombani, kabla ya kilele Septemba 25 Unguja,’’alieleza.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati ya Habari na Burudani Adam Ramadhani
Kombo, ameipongeza wizara, kwa kuendeleza tamasha hilo na kuahidi kamati yake,
itafanyakazi kwa karibu na wizara, ili kufanikisha shughuli hiyo.
Aidha aliwataka
wajumbe wa kamati hiyo, kuhakikisha, kazi na majukumu waliyopewa wanayafanya
kwa ufanisi, ili kuhakikisha wananchi wote wanapata taarifa.
Hili ni tamasha la
31, la utamaduni wa mzanzibari, kufanyika Unguja na Pemba, ambapo kwa mwaka huu,
uzinduzi wake unatarajiwa kufanyika Micheweni Septemba 19 mwaka huu.
MWISHO.

Comments
Post a Comment