NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANAFUNZI wa vyuo, skuli za msingi na sekondari za wilaya ya Micheweni, wametakiwa kujiepusha na kupokea zawadi ovyo ovyo zikiwemo chips kuku, kwani huwa ni chanzo za kudhalilishwa na baadhi ya watu.
Hayo yameelezwa leo Juni 2, 2025 na maafisa sheria kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, Jeshi la Polisi, Maafisa ustawi na wanasheria wingine, kwenye kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya Mama Samia Suluhu Hassaan inayoendelea.
Afisa Ustawi wa Jamii wilaya ya Micheweni Bizume Haji Zume, alisema wapo baadhi ya wadhalilishaji, huanza kuwapa zawadi watoto ikiwemo chakula cha chips na fedha, hivyo ni vyema wakajiepusha navyo.
Alieleza kuwa, wapo wengi ambao wameshadhalilishwa kwa kuwa rahisi kupokea zawadi ambazo mwisho wake, hudhalilishwa na kufanyiwa ukatili.
‘’Wanafunzi, mhakikishe hampendi kupokea zawadi za ovyo ovyo, kama chips na fedha na hata msaada wa usafiri ‘lift’ kwa watu wasiowafahamu, maana athari yake ni mbaya,’’alifafanua.
Kwa upande wake, Wakili wa serikali Zubeir Awamu Zubeir, aliwakumbusha wanafunzi kuwa, kwa sasa jukumu lao ni kusoma na sio kujiingiza katika vitendo vya uasharati.
‘’Kwa muda huu, wanafunzi nyinyi jukumu lenu ni kusoma na sio jingine lolote, maana maisha yenu yanaanzia hapa katika skuli na vyuo,’’alifafanua.
Mapema Inspekta wa Polisi kutoka kituo cha Polisi Chake chake Saleh Ame Makame, amewataka wanafunzi kuhakikisha wanawaripoti wale wote wanaoonesha nia ya kutaka kuwaharibia maisha yao.
Akizungumzia lengo la kampeni hiyio, Afisa sheria kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria Pemba, Ali Salim Hamad, alisema inataka kuwafikia wananchi hasa wa kundi la wanawake, watoto, watu wenye ulemavu na wasiojiweza.
Alieleza kuwa, Mama Samia katika ziara zake, aliposhuhudia wapo wananchi kadhaa, wanalilia haki zao na hawajuai wapi wazifuatilie.
‘’Baada ya kuona hivyo, ndio maana aliamua kuanzisha kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria, ili wananchi wajue haki na wajibu wao, na kuhakikisha wanapata haki zao,’’alifafanua.
Mwanasheri wa Halmashauri ya wilaya ya Micheweni Rukia Khamis Said, aliwakumbusha wanafunzi hao, kuwahimiza wananchi kulipa ada na matozo mbali mbali, ili serikali ipate kujiendesha.
Mwalimu mkuu wa skuli ya sekondari ya Mtemani Hamad Bur-han Daudi, alisema ujio wa kampeni hiyo, imesaidia kupata taaluma, ambayo yengepaswa kulipiwa.
‘’Leo kupitia kampeni hii, tumejua haki na wajibu wa watoto, haki za binaadamu na hata malengo ya kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya Mama Samia,’’alieleza.
Nae Mkuu wa Chuo cha Ualimu cha Singida kilichopo Wingwi Salim Khamis Bakari, ameiomba timu hiyo kurejea tena katika chuo hicho, ili kutoa elimu zaidi.
Wanafunzi wa skuli hizo, walisema ujio wa kampeni hiyo, imewapa fursa ya kuuliza maswali yao kadhaa ya kisheria, ambayo yalikuwa yakiwakwaza.
Mwanafunzi Aisha Haji Machano wa skuli ya Mtemani, alitaka kujua ikiwa mtoto aliyedhalilishwa anaweza kumsaidiaje, ili asiathirike kiakili.
Mwanafunzi anayesomea ualimu chuo cha ualimu cha Singida, Jokha Mohamed Said, alitaka kujua ikiwa kwa mtoto aliyebakwa anaweza kumfanyia vipi ikiwa wazazi wamepanga kuimaliza kesi kienyeji.
Mwisho
Comments
Post a Comment