NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@@
KAMPENI ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluh Hassan, imetangaazwa kwa wanafunzi wa skuli ya skondari ya Maziwang’ombe na wale wa Chuo cha kiislamu Micheweni.
Wataalamu wa masuala ya kisheria kutoka ofisi za Mkurugenzi wa Mashtaka, Jeshi la Polisi, Mawakili wa kujitegemea, Maafisa ustawi wa jamii na wanasheria wa halmashauri, walifika leo Juni 1, 2025 kwenye kampeni maalum inayoendelea.
Wakizungumza kwenye mikutano hiyo ya wazi, walisema kampeni hiyo inakuja kuwaelezea wananchi na hasa wanawake, watu wenye ulemavu, waliomo kwenye makundi maalum na wasiokuwa na uwezo, kujua haki na wajibu wao kisheria.
Inspekta Saleh Ame Makame kutoka kituo cha Polisi Chake chake, aliwataka wanafunzi hao, kuripoti wanapoona viashiria vya udhalilishaji dhidi yao na wasivifumbie macho.
Alisema, kama lengo la kampeni hiyo ni kuwaelezea haki na wajibu wao, hivyo wahakikisha wanawaripoti wanaowanyemelea kutaka kuwadhalilishaji.
‘’Leo kampeni ya msaada wa kisheria imefika kwenu, sasa ni wakati wenu kuzijua haki hizi na kuyajua maeneo ya kuripoti matukio mbali mbali,’’alisema.
Nae Mratibu wa kampeni hiyo kwa wilaya ya Micheweni kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, Khamis Bakar Amani, alisema matokeo ya kampeni hiyo ni maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alisema, wakati anafanya ziara katika maeneo kadhaa ya Tanzania, alishuhudia wananchi mbali mbali, wakilalamikia kukosa uwezo wa kufuatilia haki zao kwa wanasheria, kwa kukosa gharama.
‘’Leo kampeni hii, sasa iko kwa wananchi mbali mbali, na lengo lake ni kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo,’’alifafanua.
Mapema Wakili wa serikali kutoka Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Pemba Zubeir Awamu Zuebir, akizungumza na wanafunzi cha Chuo cha Kiislamu Micheweni, alisema moja wapo ya haki za mtoto, ni kupatiwa cheti cha kuzaliwa.
‘’Kwa ambae hana cheti cha kuzaliwa, sheria ziko wazi kuwa anatakiwa afuate taratibu ikiwemo kwenda kwa shehe wake na kisha anaweza kulipa ada kidogo, kwa ajili ya kupatiwa,’’alifafanua.
Hata hivyo, Mwanasheria kutoka Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Pemba Massoud Ali Massoud, amewakumbusha wananchi wa wilaya ya Micheweni, kuzitumia siku tisa za kampeni hiyo, maalum kupata ufafanuzi wa masuala yao ya kisheria.
‘’Mabanda yetu yapo Wete eneo la Jamhuri holi, sasa mnaweza kufika na malalamiko yenu ya kisheria, iwe migogoro ya ndoa, ardhi, mipaka, vyeti vya kuzaliwa wanaweza kupewa ufafanuzi bila ya malipo,’’alieleza.
Awali Msaidizi Mkuu wa Chuo cha Kiislam Micheweni CCK, Maryam Hemed Said, aliwataka wanafunzi wanaoyemelewa na waalimu kwa matendo ya udhalilishaji, kuwaripoti katika vyombo mbali mbali.
‘’Hata kama anayekutaka kimapenzi ni mwalimu wako wa darasa ama mwalimu mkuu, kwa vile ana nia ya kutaka kukuharibia, toa taarifa hapa Polisi, au ustawi wa jamii, ili hatua zichukuliwe,’’alieleza.
Awali kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa mkoa wa kaskazini Pemba, ilizinduliwa Oktoba 17, 2024 wilaya ya Micheweni, na kitaifa itamalizika Febuari mwakani.
Mwisho
Comments
Post a Comment