NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
KADHI wa wilaya ya Micheweni sheikh Mansab Khamis Omar, amewakumbusha waumini wa dini ya kiislam wa wilaya hiyo, kuzisajili ndoa zao, ili kupata cheti kinachotambulika.
Kadhi huyo, aliyasema hayo leo Juni 3, 2025 kwa nyakati tofauti, wakati akizungumza na wananachi hao, kwenye muendelezo wa mikutano ya kampeni ya kitaifa ya msaada wa sheria ya Mama Samia, iliyofanyika Tumbe na Chimba.
Alisema, unaposajili ndoa, kisha unakabidhiwa cheti ambacho kinaweza kusaidia pindi ikitokezea siuntafahamu katika maisha ya ndoa hapo baadae.
Alieleza kuwa, cheti hicho pia husaidia kupatikana kwa uhakika wa maandishi, iwapo mmoja kati ya wanandoa hao amefariki.
‘’Cheti cha ndoa ni muhimu mno, maana kinaweza kukusaidia hata, unapoomba vyeti vyingine mfano cheti cha kuzaliwa kwa watoto watakaopatikana,’’ aliwakumbusha.
Katika hatua nyingine, Kadhi huyo wa wilaya ya Micheweni, aliwataka wazazi na walezi kusimamia kwa karibu ndoa za watoto wao, na wasiwe chanzo cha kuzivunja.
‘’Pale mahakamani tunapokea kesi na kisha ndoa kuvunjika, ingawa ukikaa na wanandoa, wanaeleza kuwa wazazi na wamekuwa sehemu ya kuzivunja ndoa za watoto wao,’’alieleza.
Mapema Afisa sheria kutoka Kamisheni ya wakfu Pemba Massoud Ali Massoud, aliwakumbusha waumini hao wa dini ya kiislamu, kuitumia ofisi yao wanapotaka kurithi mali za marehemu wao.
‘’Moja ya faida kubwa ya kufika ofisini kwetu na kurithishwa, ni kupewa nyaraka halisi za umiliki, ambazo zinaweza kuongeza thamani ya ardhi, shamba ama nyumba iliyorithiwa,’’alisisitiza.
Kwa upande wake Mratibu wa kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya Mama Samia wilaya ya Ali Salim, alisema ujio wa kampeni hiyo ni maono ya Mama Samia, katika kuhakikisha wananchi wasiokuwa na uwezo na wanawake, wanapata msaada na ushauri wa kisheria.
Alisema, tayari kampeni kama hiyo imeshazinduliwa kwa mkoa wa kusini Pemba, na kuwepo kwa kambi maalum pamoja na wataalamu wa masuala ya sheria, kuwafikia wananchi walipo.
‘’Hapa ambacho alikusudia Mama Samia, ni kuona hakuna mwananchi analalamikia kukosa haki yake na akidai kukosa gharama za kumtafuta mwanasheria au wakili,’’alisisitiza.
Mwalimu mkuu wa skuli ya sekondari ya Shumba Vyamboni Baraka Seif Hamad, alisema kampeni imekuja wakati mwafaka katika skuli yake, kwa vile wanafunzi wake, hawana uwelewa wa mausala ya kisheria.
Mwananchi wa Chimba wilaya ya Micheweni Hamida Haji Said, alisema kwa sasa amepata uwelewa wa masuala la mirathi na kujua faida ya kurithishwa serikalini.
Nassor Haji Hamdani wa shehia ya Mihogoni, alishauri kuwa, ujio kama huo ufanyike kila baada ya miezi sita, ili wananchi wapate kutoa malalamiko yao.
Timu ya wataalamu wa masuala ya sheria kutoka Jeshi la Polisi, Ofisi ya Mkurugenzi wa mashataka, ofisi ya mwanasheria mkuu, Halmashauri, ustawi wa jamii, wakala wa matukio ya kijamii na ofisi ya kadhi, itaendelea kesho kwa shehia za Konde na skuli zake.
Mwisho
Comments
Post a Comment