IMEANDIKWA NA SAIDA ALI, PEMBA@@@@
MAAFISA Utumishi kwenye taasisi za Serikali na binafsi
wametakiwa kutokuchelewesha mafaili ya watumishi wanaohitaji stahiki zao za
mafao ZSSF, ili kuondosha usumbufu unaojitokeza wakati wa utekelezaji wa kazi
hiyo.
Akizungumza na maafisa hao katika Ukumbi wa kiwanja cha
kufurahishia watoto Tibirinzi Chake Chake Pemba, Mkurugenzi wa Mfuko wa Hifadhi
ya Jamii (ZSSF) Pemba, Msabah Massoud Msabah alisema, kuna haja ya kuwa na
Ofisa maalumu ambae atashughulikia mafaili hayo na sio kubadilishwa.
Alisema kuwa, kumekuwa na ucheleweshwaji mkubwa wa mafaili
ya watumishi ambao wanastahiki kupatiwa mafao yao kwa namna moja ama nyengine,
jambo ambalo linaweza kuchukua muda mrefu kupatikana kwa haki, na wakati
mwengene wanaweza kuikosesha kabisa, kwani kuna muda maalumu uliopangwa kwa
ajili ya kuwasilisha vielelezo.
“Tushirikiane pamoja katika hili kuhakikisha wanapatikana
watendaji maalumu, ambao hata kwenye mafunzo watakuwa wanakuja hao hao kwa
ajili ya kuwajenga zaidi kiufanisi katika kazi zetu, hii itaondosha usumbufu,”
alisema Mkurugenzi huyo.
Alisema kuwa, lengo la mkutano huo ni kuimarisha utendaji
kazi wa maofisa hao, kwani ZSSF ndio kwenye maisha ya baadae ya watumishi.
Akielezea Dhana ya Hifadhi ya Jamii, Mkuu wa Kitengo cha
Sheria ZSSF, Ramadhan Juma Suleiman alisema, ni utoaji wa hifadhi ya jamii
kupitia mifumo ya bima ya jamii au mifumo ya lazima ya akiba na Pensheni,
ambapo wafanyakazi na waajiri wao hutoa michango ya lazima kwa mfuko wa hifadhi
ya jamii, kwa mujibu wa sheria ambayo hutumika kutoa mafao kwa wanachama
wanapokabiliwa na hatari za kijamii.
Alieleza kuwa inaaminika kidunia kwamba, kila mmoja
anatabiriwa changamoto, na ndio maana ZSSF inahakikisha mwanachama wao anapata
kinga kwa kupatiwa mafao yake, kwa ajili ya kuendeleza kipato chake hata akiwa
amepatwa na majanga.
“Tumeweka utaratibu huu maalumu, ili kumsaidia mtumishi
kupata kipato cha kujiendeleza kimaisha, ikiwa amepatwa na ugonjwa, ajali,
upotevu wa ajira, uzee na uzazi, hivyo maofisa mnatakiwa kulijua hili na
kuwaelimisha watumishi, ili wasikose haki zao hizi,” alisema.
Kwa upande wake muwasilishaji mada ya Mafao ya upotevu wa
ajira, Rashid Shoka Salim alieleza kuwa, ni kiwango maalumu cha fedha kinachotolewa
kwa mwanachama aliepoteza ajira kutokana na sababu zilizoainishwa kwenye Sheria
na kanuni za mafao hayo.
Alisema ili mwanachama aweze kupata fao hilo, ni lazima awe
ameachishwa kazi kuanzia Oktoba mwaka 2022, awe amechagia kwa kipindi kisichopungua
miezi 18, awe amekosa kazi kwa kipindi cha miezi sita, awe mtanzania na pia awe
ameachishwa kazi na muajiri wa mwisho.
“Lakini hawezi kupata fao hili mtumishi ambae ameacha kazi mwenyewe, au alieachishwa kazi kwa kosa la nidhamu,
rushwa, wizi, ubadhirifu au ameacha kazi kwa shughuli za kisiasa,” alisema
Shoka.
Nae Muwasilishaji wa Fao la kuumia kazini, Meneja Mafao ya
Muda Mfupi ZSSF Zainab Rajab Baraka, alitaja changamoto zinazowakabili ni,
kuchelewa kuwasilisha taarifa za ajali kwa wakati, wanachama kuripoti kwa
madaktari kwa ajili ya kupatiwa siku za mapumziko na utambuzi wa maradhi
yatokanayo na kazi kwa wafanyakazi.
“Mfanyakazi anaestahiki kulipwa mafao ya kuumia kazini ni,
yule ambae ni mwanachama wa ZSSF, michango yake ya asilimia moja inawasilishwa
kwetu, amepatwa na majeraha, maradhi au kifo kutokana na kazi bila kukusudia,
na ameshindwa kufanya kazi kuanzia siku tatu,” alifahamisha.
Mshiriki wa mkutano huo kutoka hoteli ya Mantarif, Suleiman
Kombo Ali alisema, elimu waliyoipata ni faida kwao kwani yamewajengea uwezo
mkubwa wa kuelewa haki zao kwenye Mfuko huo, kwa sababu sekta binafi ajira sio
za kudumu, hivyo wengi hupoteza haki zao.
“Awali ilikuwa hatujui kuhusu fao la upotevu wa ajira, hivyo
kupitia elimu hii tutawafundisha wengine, ili waelewe na kupata haki zao za
msingi, tunaewapongeza ZSSF kwa kutuelewesha, tumefurahi sana,” alisema
mwakilishi wa hoteli ya Fundolagon Kessi Shehe.
MWISHO.
Comments
Post a Comment