NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
WANAWAKE wanaofanya biashara katika masoko ya Mjini Wete
na Kifumbikai Wilaya ya Wete Kaskazini Pemba, wameshauriwa kuripoti vitendo vya ukatili na udhalilishaji kwa
viongozi wao wa masoko, ili kuchukua hatua zaidi katika kukabiliana navyo.
Ushauri huo umetolewa na Msimamizi wa masoko na mazingira
Wilaya ya Wete Sadri Mussa Said, wakati
akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake Wete Kaskazini Pemba.
Alise katika masoko yote kuna viongozi waliochaguliwa kwa
ajili ya kusimamia wafanyabiashara na kuwatatulia changamoto zao mbali mbali za
kimazingira na kinidhamu, hivyo ni vizuri kuwatumia ili kupata msaada wa
changamoto hizo wanapokua katika shughuli zao za kibiashara.
"Masoko yote kuna viongozi waliochaguliwa kwa ajili ya
kusimamia wafanyabiashara na kuwatatulia changamoto zao mbali mbali za
kimazingira na kinidhamu, hivyo
tunawashauri wanawake kuwatumia kuripoti matukio ya udhalilishaji yanapotokezea,
ili kupata msaada zaidi" alieleza.
Alisema kufanya hivyo kutawawezesha wanawake kufanya kazi
zao vizuri, kwa kua na uhakika wa Ulinzi na usalama wao wanpokua katika maeneo
ya soko, ambayo ndio matakwa ya serikali na sheria za nchi kwa ujumla.
Alisema uongozi wa soko umekua ukiwashajihisha
wafanyabiashara hao kuripoti changamoto zao mbali mbali ikiwemo ya
udhalilishaji, lakini bado muitikio ni mdogo jambo linalopelekea kuendelea kwa
vitendo hivyo.
Aidha alitoa wito kwa wanawake kua na tahadhari juu ya
viashiria vitakavyopeleka udhalilishaji, kwa uepuka michanganyiko pamoja na majibizano yasio ya lazima ya wao
kwa wao na wateja wao.
Kwa upande wake Mfanyabiashara Tahiya Said Abeid wa soko la
Mjini Wete alisema, katika ufanyajikazi
wao sokoni hapo wamekua wakikabiliwa na udhalilishaji wa kihisia utokanao na
maneno machafu na udhalilishaji wa kimwili, ambao huwakatisha tamaa katika
utafutaji.
Alisema changamoto hizo mara nyingi husabishwa na hali duni za kiuchumi na uhaba wa mitaji ,
unaopelekea kua wategemezi kwa watu wengine, hali inayotoa fursa ya
kudhalilishwa.
Hivyo aliiomba serikali na wadau wengine wa maendeleo
kuungamkono harakati za kuwainua wanawake
kiuchumi, ili kuimarisha vipato vyao na kupunguza matendo hayo.
Nae mfanyabiashara Maryam Muhammed Mgeni wa soko la
Kifumbikai Wete Pemba alisema, wanawake wengi sokoni hapo hawana muamko wa
kuripoti vitendo hivyo kutokana na kushindwa kuelewa pakuanzia na wakati
mwengine kuoana vitendo hivyo ni vya kawaida kutokea hasa katika mazingira yao.
Hivyo ameomba mamlaka husika kuendelea kutoa elimu zaidi juu
ya viashiria na athari za udhalilishaji na ukatili, namna ya kujikinga na hatua
za kuchukua pale vinapotokezea, ili kudumisha usalama wa wanawake katika shughuli zao za kiuchumi.
Nae Afisa Ustawi wa Jamii wilaya ya Wete Kaskazini
Pemba Salma Saleh Hamad alisema,
kunauwekano mkubwa wa wanawake kufanya biashara zao masoko bila kudhalilishwa,
iwapo wataelewa haki zao na kuweza kujipambania, huku akisisitiza umuhimu wa
kuripoti vitendo hivyo vinapotokezea.
MWISHO


Comments
Post a Comment