Skip to main content

UGONJWA WA ‘RED EYES’ WAKWAMISHA KESI DAWA ZA KULEVYA PEMBA

 

 NA MARYAM NASSOR, PEMBA@@@@   

 KESI ya kupatikana na dawa zinazoaminika kuwa ni za kulevya, iliyopo mahakama kuu Zanzibar, kanda ya Pemba, imeshindwa kuendelea, baada ya shahidi nambari moja, ambae ni Mkemia kushindwa kufika  mahakamani hapo, kwa  udhuru wa  ugonjwa wa ‘RED EYES’.

 Awali, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, mtuhumiwa katika shauri hilo, Omar Khatibu Juma, alikutwa na misokoto 700 yanayosadikiwa kuwa ni dawa za kulevya  aina ya bangi, yenye uzito wa gramu 2836.75, eneo la Machomane wilaya ya Chake chake.

Mara baada ya kufika mahakamani hapo, mtuhumiwa akiwakilishwa na wakili wake Zahran Mohamed Yussuf aliambiwa  na upande wa mashtaka ulioongozwa na Mwendesha mashtaka kutoka Afisi ya Mkurugenzi wa mashtaka, Mohamed  Ali Juma, kuwa walikuwa wanategemea kupokea mashahid watatu.

 

Alidai kuwa, kesi hiyo ipo kwa ajili ya kusikilizwa,  na wamepokea mashahidi wawili, kati ya watatu waliyoitwa, ingawa shahidi nambari moja ambae ni Mkemia, hajafika mahakamani hapo kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa macho mekundu.

Aliendelea kudai kuwa, kutokana na aina ya kesi hiyo wanahitaji mtiririko mzuri wa mashahidi, hivyo hawawezi kusikiliza shahidi wengine kabla ya kuanza na Mkemia.

‘’Mheshimiwa leo (jana) kesi ipo kwa ajili ya kusikilizwa, ingawa shahidi nambari moja hajafika mahakamani, hivyo tunaomba utupangie tarehe nyingine, kwa ajili ya kusikiliza mashahidi,’’alidai.

Mara baada ya kuusikiliza upande wa mashtaka, Jaji wa mahakama kuu Pemba, Ibrahim Mzee Ibrahim, aliuliza upande wa utetezi kuwa wanasemaje kuhusu ombi la upande wa mashtaka.

Nao, upande wa utetezi ulikuwa ukiongozwa na mawakili Zahran Mohamed Yussuf na Massoud Juma walidai kuwa, hawakubaliani na ombi hilo kutokana na kuwa, mteja wao ameshakaa ndani muda mrefu na kuomna kusikilizwa kwa mashahidi waliofika mahakamani.

“Mheshimiwa Jaji, kama ikikupendeza, basi tunaomba usikilize hao mashahidi wawili waliofika, kutokana na kuwa mteja wangu yuko ndani mudaa mrefu,”alidai.

Alidai kuwa, shauri hilo tokea lifunguliwe mahakamani hapo, linafika miezi sita na mtuhumiwa yuko ndani, kama ikiwezekana basi wasikilizwe hao mashahidi waliyofika na isiwe vyenginevyo.

Nae Jaji wa mahakama hiyo, alimuliza wakili wa upande wa utetezi kuwa mteja wake, ana shutumiwa na makosa mangapi, kwa sababu kama kosa ni kukutwa na bangi basi shahidi nambari moja ni Mkemia.

Aidha alisema, Mkemia ndie atakae thibitisha kuwa kile alichokiona ni bangi au laa na hapo, ushahidi utakaofuata utakuwa unasaidia.

“Hatuwezi kusikiliza shahidi wengine kabla ya Mkemia, kwa sababu ndie atakae thibitisha hizi tuhuma ni za kweli au laa,”alisema.

Nao upande wa utetezi kisha, ulikubaliana na hoja za Jaji huyo, na kisha kesi hiyo kughairishwa hadi Machi 7 mwaka huu, ili kuendelea na ushahidi.



Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, Julai 28, jana majira ya saa 4:00 za usiku eneo la Mkoroshoni, katika wilaya ya Chake chake, bila ya halali  alipatikana na misokoto 700, ya dawa zinazodhaniwa kuwa ni za kulevya aina ya bhangi, yenye uzito wa gramu 2836.75.

Hilo ni kosa kinyume na kifungu cha 21 (1) (d) cha sheria za Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana  na dawa za kulevya Zanzibar, sheria namba 8 ya mwaka 2021 sheria za Zanzibar.

                                         MWISHO

 

 

 

Comments