Skip to main content

MADIWANI WANAWAKE WANAVYOSIMAMIA VYEMA UWONGOZI

 


NA  AMRAT KOMBO, ZANZIBAR@@@@

SIKU zote baadhi ya watu wanaimani ya kuwa, mwanamke bado ni mama wa nyumbani pekee.

Ambae anatakiwa kuchunga familia yake tu peke yake, lakini bila ya kufikiri kuwa mwanamke anaweza kufanya mambo makubwa ya kuwasaidia jamii na kuleta maendeleo katika nchi.

Ushahidi wa hili, sasa usiangalia tena Marekani na kwengineko, njoo kwa Rais wa Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania, alivokuwa jasiri na mchapa kazi, katika nafasi yake ya uwongozi.

Hivyo inaonesha kuwa, mwanamke sio mdhaifu kama watu wanavoona, hebu tuangalie baadhi ya viongozi mwanamke wanavyowajibika katika nafasi zao.

Fatma Rashid Juma ni diwani wa  Chukwani Unguja, anasema kabla ya kushika nafasi hiyo, alikuwa mfanya biashara  mjasiria mali mdogo, huku akiwa mwanancha wa chama cha mapinduzi CCM.

Anasema katika mwaka 2020, alijishirikisha katika kugombea udiwani wakiwa na wagombea wenzake 11, wakiwa wanawake watatu na wanaume nane, na kubahatika kutokea mshindi kwenye kinyanganyiro hicho kwa kupata kura 49 katika watu 100.



Sababu iliyopelekea kuingia katika siasa, anasema zipo nyingi ingawa moja ni kutetea haki za wanyonge, kuweza kupaza sauti zao.

Licha ya hayo anasema uongozi  hauna umri kila mtu anahaki ya kusimamia na kutetea, na hasa akishafikia ule umri wa kuanza kupiga kura.

Diwani Fatma amefanya mambo mbali mbali ambayo yameweza kuwasaidia wananchi wake, ikiwemo kutengeneza barabara ya kijiji cha Shakani na ya Chukwani, kutengenezea banda la wajasiria mali 20 katika skuli ya Chukwani, lenye gharama ya shiling 5,700,000  na kwasasa anapambana kutengeneza kituo cha daladala cha Chukwani.

Sambamba na hayo anatarajia kutengeneza kisima katika wadi ya Chukwani na Buyu, ili kuona wananchi wake wanaendelea kuugawa muda wao katika kazi nyingine.

Vikwanzo ambavyo amepitia wakati alipopata nafasi ya uwongozi ikiwemo baadhi ya wagombea wenzake kuwepo kwa matabaka, lakini alifanikiwa kukabiliana na vikwazo hivyo kwa kuamua kujishusha chini na kuanza kuwasikiliza maoni yao.





" Wakati nilipopata hii nafasi, nikapelekea kupata changamoto ya wagombea wenzangu, kuweka matabaka pamoja na maneno yasio kwisha, ingawa niliamua kupambana na changamoto hiyo na kufanikiwa,’’anasema.

 WANAOMFAHAMU DIWANI FATMA

Sheha wa  Chukwani Suleiman Mohamed Mwinyi, anasema kuna umuhimu wa kuwepo viongozi wanawake kama Diwani Fatma, kwani wanakuwa na ushawishi mkubwa katika uwongozi wao.

" Haswa wanapopewa mafunzo, huwa mstari wa mbele katika kufahamu mambo mengi, wanakuwa waaminifu katika uwongozi wao kama alivyo Diwani wetu,’’anaeleza.

Anaona viongozi walio wengi wanawake, wamekuwa watetezi wakubwa katika shughuli mbali mbali, ikiwemo katika sekta ya   kupiga vita vitendo vya ukali na udhalilishaji.

Sambamba na hayo alisema katika shehia yao wametoa viongozi mbalimbali wanawake kwa lengo la kuwajengea uwezo na kusimamia maendeleo ya shehia hiyo.

"Katika shehia yetu, tunao viongozi wanawake, kwa mfano tumewahi kuwa na mbunge mwanamke, diwani mwanamke hadi kufikia mwenyekiti wa halimashauri wa wilaya, na akanzisha vikundi tofauti vya maendeleo,’’anasifia.

 "Kwasasa tuna mkuu wa wilaya mwanamke ambae  ni mchakarikaji, mshumpavu, na mwenye  kuvumilia kero za wananchi, pamoja na kutatua changamoto zetu, akishirikiana na Diwani Fatma,’’analeza.

 Licha ya yote hayo alisema diwani Fatma amefanya jitihada mbalimbali za kimaendeleo, ikiwemo kuhamasisha masuala ya afya, kiuchumi pamoja na kufanya ubunifu wa kueka banda la ujasiria mali kwa lengo la kuweza  kujikwamua na umaskini.

Mwananchi Aziza Ali, anasema wamepata kiongozi imara mwenye utu, ambae anasidia kutatua changamoto zinazowakabili kwenye wadi yao.

Nae Hamadi Makame, anasema wamepata kiongozi anaewajibika katika majukumu yake, na ataendelea kumuunga mkono, ili aweze kufanya kazi kwa wepesi.

Asha Hassan Juma ambae ni Diwani ya Jitimai Mwanakwerekwe, anasema kabla ya kugombea nafasi ya udiwani, alikuwa anafasi mbalimbali, ikiwemo mjumbe wa sheha, Mwenyekiti wa  umoja wa wanawake tanzania (UWT) katika tawi na kuamua kugombea nafasi ya diwani tangu 2015 .

"Nimegombea udiwani katika awamu mbili, tangu mwaka 2015 hadi 2020, na nikagombea tena 2020, hivyo uwongozi huu natumikia hadi 2025," anasema.

Wengi wao wanasema msemo unaosema mwanamke bila ya kuwezeshwa anaweza, ni sahihi kutokana na mapambano na jitihada wanazozifanya mwanamke katika kuhakikisha analeta maendeleo katika uwongozi wake.

Mkurugezi wa Jumuiya ya wanasheria wanawake (ZAFELA) Jamila Mahmoud, anasema wanatoa elimu ya kuhamasisha wanawake katika kugombea nafasi mbali mbali za uongozi.

Anasema, kwani wanawake ilionekana wapo kidogo mno, kwenye nafasi kuanzia udiwani, uwakilishi, ubunge, na hata kwenye nafasi za uteuzi kama za uwaziri, katibu mkuu, mkuu wa wilaya, usheha pamoja na wakurugenzi.

Sambamba hayo anasema kuna umuhimu wa kuwepo sheria ambazo zinatoa nafasi, mfano watu walivopendekeza kuwepo kwa 50 kwa 50 kwa hiyo itasaidia wanawake kupata nafasi nyingi za uongozi.

"Mwanamke anapotaka kusimama katika  kugombea jimboni, anaweza kupata vitisho, kutengenezewa kashfa, pamoja na  kuamini tamaduni kuwa mwanamke hafai kuwa kiongozi, hizi huwavunja moyo,’’anaeleza.

Mratibu wa kuinua wanawake katika uongozi kutoka chama cha wandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA Zanzibar), Maryam Ame, anasema wanatoa elimu mbalimbali, kwa wanawake ambao wanahitaji kuwa kiongozi, ili wajitambue na kutatua changamoto za kiuongozi.

"Na hii inawapa hamasa na kuweza kutambua haki zao za kidemokrasia, siasa, mil ana utamaduni ikiwemo haki ya kupata elimu, afya pamoja na miundombinu,’’anasema.

Maryam anasema hadi sasa zaidi ya wanawake 172 wamepatiwa mafunzo ya uwongozi kutoka Unguja na Pemba, pamoja na kutambua vikwazo na namna ya kukabiliana navyo.


Aidha aliwanasihi wanawake wanaotaka kuingia kwenye uongozi kutokuwa na hofu, kama Katiba inavyosema katika serikali zote mbili inavyoelezea pamoja na mikataba mbalimbali ya kitaifa na kikanda.

Mkurugezi wa Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Thabit Idarous Faina, anasema hali halisi ya viongozi wanawake Zanzibar, kupitia nafasi ya uwakilishi kwenye majimbo 50, ya Zanzibar wanawake ni wanane  pekee.

Anasema wabunge wanaowakilisha Zanzibar wanawake ni wanne tu sawa na asilimia nane, huku mawaziri wakiwa sita sawa na asilimia 33 na makatibu wakuu ni saba sawa na asilimia 39.

Kwa upande wa wakuu wa mikoa, mwanamke ni moja tu sawa na asilimia 20,wakuu wa wilaya ni wanane sawa na asilimia 36 na masheha wanawake ni 68 sawa na asilimia 17 kwa masheha wote ambao ni 389.

Sambamba na hayo anasema miongoni mwa vikwanzo vya wanawake kutoingia kwenye uwongozi, ikiwemo majukwaa ya kisiasa yanatajwa kuwa ni moja wapo ya vikwanzo vinavyosababisha wanawake wasifikie malengo yao.

 Mwisho

 

 

 

Comments