NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WIZARA ya Ujenzi na Uchukuzi kisiwani
Pemba, imewataka wananchi watakaodaiwa nauli mpya iwe kwenye dalala, bajaji au
bodaboda kwa kisingizio cha kupanda bei ya mafuta, kuripoti katika vyombo vya
sheria, kwani serikali haijatangaaza nauli mpya.
Kauli hiyo, imetolewa na Ofisa Mdhamini wa wizara
hiyo, Ibrahim Saleh Juma, wakati akizungumza na mwandishi wa habari hizi,
kufuatia malalamiko ya wananchi, kulipishiwa nauli mpya hivi sasa.
Alisema, serikali inaelewa vyema juu ya changamoto
ya kupanda kwa nishati hiyo ya mafuta duniani, ingawa bado, tamko la kupandishwa
nauli halijatolewa.
Alieleza kuwa, serikali imekuwa na utaratibu wa
kupokea mapendekezo ya upandishwaji wa nauli hiyo kutoka kwa madereva hao, na
kisha kukaa pamoja, ili kuangalia uwezekono wa kupandisha ama laa.
Ibrahimu alieleza kuwa, hadi sasa na tokea kupanda
kwa nishati hiyo, serikali haijatangaaza nauli mpya, hivyo ni marufuku kwa
dereva yeyote, kupandisha nauli hiyo.
Alifafanua kuwa, ni vyema wananchi watakaokumbana na
changamoto hiyo, kuchukua nambari ya chombo hicho, na kukilalamikia katika
vyombo ya sheria, kwa hatua zaidi.
‘’Tunaelewa kuwa nishati ya mafuta imeshapanda bei,
lakini serikali na wamiliki wa gari hizo na vyombo vyingine, hatujakaa
tukakubaliana bei mpya, hivyo kwa sasa ziendelee bei za zamani,’’alifafanua.
Hivyo, amerejea wito wake kwa wananchi, kwanza
wasikubali kulipishwa nauli mpya na wakitenzwa nguvu, wakimbilie kwenye vyombo
vya sheria kuripoti taarifa hiyo.
Aliendelea kusisitiza kuwa, dereva atakejichukulia
sheria mikononi mwake, kwa kuwaongezea nauli abiria, hatua kali za kisheria zitachukuliwa
dhidi yake.
Katika hatua nyingine, Ofisa Mdhamini huyo,
aliwataka madereva na makondakta, kuendelea kuwatoza abiria nauli za zamani, na
serikali inaendelea kulitafutia ufumbuzi jambo hilo.
‘’Ni kweli madereva wanahaki ya kulalamikia upandaji
wa bei ya mafuta, lakini hawana mamlaka ya kupandisha nauli, maana hata mafuta
yakishuka bei, wao hawashushi,’’alifafanua.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Jumuiya ya wenye
dalala na gari za mizigo mkoa wa kusini Pemba ‘PESTA’ Hafidh Mbarka Salum,
alisema tayari wameshapeleka mapendekezo ya nauli mpya serikalini.
Alisema, baada ya kuona kuna changamoto ya kupanda
kwa bei ya nishati ya mafuta, waliamua haraka mno, kuiarifu serikali na
kuwaandikia mapendekezo yao, ili kupunguza ukali wa bei hiyo.
‘’Sasa imeshafika karibu wiki, tokea tupeleke
mapendekezo hayo, ingawa siwezi kukutajia aina ya nauli tulizopendekeza, kwa
mujibu wa masafa,’’alieleza.
Hata hivyo Katibu mkuu huyo wa ‘PESTA’, amesema
Jumuiya yao, haitambui nauli mpya wanazotoleshwa abiria, katika gari za abiria,
kwani hadi sasa, mapendekezo yao ya nauli mpya hayajajibiwa serikalini.
‘’Inaumiza na kuuma mno, kuona nishati ya mafuta na
gharama nyingine zimeshapanda, lakini nauli bado zinatumika za zamani, niwaombe
waendelee na ustahamilivu,’’alisisitiza.
Baadhi ya madereva wa gari za abiria, akiwemo Hassan
Ali Mohamed alisema, kwa sasa wanafanyakazi hiyo, kwa hasara kubwa.
Nae Ibrahim Haji Machano, alisema kukosekana kwa
nauli mpya, na nishati ya mafuta kupanda, imekuwa kama wanawachumia fedha wenye
vituo vya mafuta pekee.
Kwa upande wake Issa Khatib Issa, alisema amekuwa
akienda miendo miwili tu kwa siku na kulaza gari, ili kupunguza hasara.
‘’Nikibahatika siku za kuwepo kwa meli, huwa ndio
safari yangu moja tu, kisha naenda kuilaza gari, maana mafuta yamepanda na
nauli bado ni kongwe,’’alifafanua.
Mwananchi Asha Haji Kombo alisema, juzi alitoleshwa
shilingi 1,500 badala ya shilingi 1,000 bei ya zamani, kutoka mjini Chake chake
hadi Ngwachwani.
Kwa upande wake Hawa Othman Azizi, alisema alipanda
dalala kutoka Mtambile hadi Mkoani, kondakta alimtolesha nauli ya shilingi 1,000
badala ya shilingi 600 ya zamani.
Imebaini kuwa, baadhi makondakta wanaofanyakazi barabara
ya Mkoani- Chake chake badala ya nauli ya shilingi 1,800 ya zamani, huwakata abiria
kati ya shilingi 2,000 hadi shilingi 2,500.
Ilifahamika kuwa, kwa mara ya mwisho serikali
ilitangaaza nauli mpya miaka mitano iliyopita, kufuatia wakati huo, kupanda kwa
nishati ya mafuta.
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati
Zanzibar ‘ZURA’ April mwaka huu, ilitangaaza kupanda kwa bei ya mafuta,
yakiwemo ya Petroli kutoka shilingi 2,942 kwa mwezi Machi hadi shilingi 3,500.
Mafuta mingine yaliopanda ni ya Dizeli, kutoka
shilingi 2,952 hadi shilingi 3,500 huku mafuta ya taa nayo yakichupa hadi
shilingi 3,500 kutoka shilingi 2,900 wakati mafuta ya ndege pekee, yakishuka
bei kutoka shilingi 2,368 hadi shilingi 2,365.
Nauli za zamani ambazo hadi sasa zinaendelea
kutumika kwa baadhi ya maeneo ni shilingi 1,800 Chake chake- Mkoani, shilingi
900 Chake chake- Mizingani, shilingi 1,300 Chake chake hadi Mtambile.
Mwisho
Comments
Post a Comment