‘…….SEA Cucumbers’ ama matango bahari…...
Na wingine huliita jongoo la pwani, ama
kiazi bahari.
Ni aina ya wanyama ama kiumbe, kinachoendesha
maisha yake baharini.
Kitango bahari, kina ngozi ngumu
kiasi na mwili mrefu ambapo muonekano na maumbile yake ni sawa na kitango
kinacholiwa nchi kavu.
Kitango bahari, kinaendelea kufafanuliwa
kwenye vitabu na mitandao kuwa, kina mwili mrefu wenye via vya uzazi, moja
iliyo na matawi.
Wanyama hawa, wanapatikana kwenye
sakafu za bahari duniani kote, wakiwa wamegawanyika kwenye spishi zaidi ya 1,717.
Ingawa nyingi zao, zinapatikana eneo la
Asia-Pasifiki, ambapo kwa Zanzibar utafiti umeonesha zipo zaidi ya aina 35.
Vitango
bahari, huishi kwa kutambaa kwenye sakafu ya bahari, na kuweka hifadhi na
kujisitiri kwenye matumbawe.
Maisha
ya viumbve hawa, waliokua hawakuwa na thamani kwa zaidi ya karne moja Zanzibar,
maisha yao yana mchango mkubwa katika ikolojia ya bahari, hasa katika kuisafisha.
Tena
imeonekana kuwa, na hili hutokea kipindi wanapokula mchanga, wenye mchanganyiko
wa bakteria, mwani na viumbe vidogo vidogo na hatimaye kusafisha.
Vina mchango muhimu kwenye mfumo wa ekolojia
wa bahari, kwa kusaidia kuzungusha virutubishi na kuvunja vunja mabaki na
uchafu wa kioganiki, wa baharini.
KIPI
CHAKULA KIKUU CHA VITANGO BAHARI?
Wataalamu mbali mbali wa ndani na wale wanaoandika tatifi, wanakubali
kuwa, moja ya chakula kikuu cha vitango bahari, ni mabaki ya viumbe vidogo.
Aina nyingine
ni viumbe vidogo vya baharini, kama planktoni na bakteria,
ingawa hata chembe chembe za kikaboni, zilizochanganyika
na mchanga wa baharini nazo hula.
AINA
ZAKE
Tafiti
zinaonesha duniani kuna aina nyingi za vitango bahari, ingawa kwa
sasa, wanasayansi wamegundua na kuelezea zaidi ya aina 1,250
tofauti.
Kwa mfano vipo aina ya ‘dendrochirotida’
nyenye umbo la miti, hutumia kukusanya chembe ndogo za chakula, ambao hupatikana
katika kina kirefu cha bahari.
Aina ya ‘holothuriida’ ambapo huwa ni
kundi kubwa lenye spishi nyingi, zinazojulikana kibiashara, ambapo hutambuliwa
kwa mikia mirefu,
Kwa Zanzibar,
wanasayansi na watafiti wamebaini kuwa kuna aina kadhaa za vitango bahari
zinazopatikana, hasa katika maeneo ya pwani yenye miamba na mchanga.
Ingawa idadi kamili ya spishi zote, bado
inachunguzwa, tafiti zinaonyesha kuwepo aina 30 hadi 40 zinazojulikana.
Na kati ya hizo, aina nane hadi 10, ndizo
zinazovunwa au kufugwa hasa kwa soko la Asia.
ZANZIBAR NA MARUFUKU UVUVI WA VITANGO
BAHARI
Marufuku
ya uvunaji wa majongoo bahari Zanzibar ilianza kutekelezwa rasmi mwanzoni mwa
miaka ya 2000, baada ya tafiti kuonyesha kupungua kwa kasi kwa spishi baharini,
kutokana na uvunaji kupita kiasi.
Kwa
wakati huo, serikali iliweka vizuizi vya uvunaji na biashara ya vitango bahari,
ili kulinda rasilimali na kuhamasisha ufugaji, badala ya kuvua moja kwa moja.
Kwa
sasa, juhudi kubwa zimeelekezwa kwenye ufugaji wa vitango bahari, hasa aina ya ‘holothuria scabra’
kupitia vituo vya kuzalisha vifaranga Unguja na Pemba.
Aina hiyo ni maarufu kwa sababu ya thamani
yake, kwenye soko la kimataifa, hasa bara la Asia, ambako hutumika kama chakula,
na kwa madhumuni ya tiba.
MAZINGIRA YA UFUGAJI WA VITANGO
BAHARI
Kunahitaji mazingira maalum ya
baharini, ili kukua vizuri na kwa haraka, ambapo kwa kawaida, wanakua kwenye
maeneo yenye mchanga, miamba, au matumbawe kwenye kina kifupi cha maji.
Hivyo wataalam wanaekeleza mambo
kadhaa ya kuzingatia, ikiwemo kiwango cha maji ya bahari, kwani hupenda kuishi
kwenye kina kisichozidi mita 20, ingawa hukua vuzuri kina cha mita1 hadi 5.
Wanashauri kuwa, hali joto ya maji, hupendelea
yenye halijoto kati ya nyuzi 25°C hadi 30°C, kwani chini ya hapo, inaweza
kuathiri ukuaji wao au hata kifo.
Lakini hata suala la uchafu wa maji,
hupendelea yalio safi na yasiyo na uchafu mwingi, ambapo wakulima husisitizwa
kusafisa, shamba zao.
WANAKIKUNDI CHA UFUGAJI
‘Tumuombe mola’
ni wanakikundi cha wanawake na wanaume, kipo Makangaale wilaya ya
Micheweni Pemba, wanatarajia kujipatia shilingi milioni 20 mwishoni mwa mwaka
huu.
Wananchi hawa, sasa wamechangamkia
ufugaji wa vitango bahari, na fedha hizo wataziingiza ikiwa watafanikiwa kuuza.
Hii ni baada ya kuekeza vifaranga vyenye
thamani ya shilingi million 1.6 mwaka jana, wakisubiri muda mfupi sasa kuvuna.
Fedha hizo, ni uwekezaji wa
vifaranga 3,300, walivyovinunua kwa shilingi milioni 1,650,000 wastani wa
shilingi 500 kila kimoja.
Wanasema kati ya vifaranga hivyo,
wanatarajia kuvuna vitango yaliokwisha komaa 2,500 na kisha kila moja kukiuza
kwa bei ya shilingi 8,000 na kujipatia shilingi milioni 20.
Mwenyekiti wa kikundi hicho Hator
Hassan, anasema haiwezekani kuotesha vifaranga vya 3,300 kisha kuvuna kama vilivyo.
‘’Zipo changamoto kama za kufa na
hasa wakati wa usafirishaji wa vifaranga kutoka eneo moja kwenda bwawani, wizi
na wingine kufa kabla ya kufikia kukomaa,’’anafafanua.
Kumbe mara ya kwanza, wakati
wanaanza kazi hiyo, walitumia shilingi milioni 1,000,000 kwa ununuzi wa vifaranga
1,000.
Ingawa hatimae, walivuna vitango 340
na kujipatia shilingi milioni 1.7, baada ya kuviuza vikiwa vibichi.
Hawakula hasara, ingawa hawakuvuuka
lengo lao la kujipatia zaidi ya shilingi milioni 5, kama sio kujitokeza
changamoto hizo.
‘’Kama sio changamoto ya vifaranga
kufa au kuibiwa wakiwa ndani ya bwawa letu, hata ule mwaka 2021 wakati
tunaanza, tungejipatia faida ya shilingi milioni 4,’’anafafanua.
Hata mwaka 2023, walitarajia kujipatia
faida ya shilingi milioni 9, ingawa hatimae, walipata shilingi milioni 1.5.
Tayari wanakikundi
hao, wameshafuga mara mbili, tokea waanze kazi hiyo mwaka 2021, na kutumia
gharama ya shilingi milioni 3.1 kwa ununuzi wa vifaranga 4,000.
Kwa kwa sasa wanasubiria
hadi mwishoni mwa mwaka huu, na ikiwa vifaranga walivyovitia ndani ya bwawa hilo,
havitapata changamoto ya wizi na kufa, hawana wasiwasi wa kuvuna shilingi
milioni 20.
Mwanachama Hamad Omar
Hamad, anasema wamekua wakibadilisha maisha yao, kupitia kazi hiyo, ikiwemo
kujihakikisha fedha za matumizi.
‘’Ni kweli kabla ya
kuanza kazi hii ya ufugaji wa vitango bahari, sikuwa na uhakika wa wapi naweza
kujipatia fedha za haraka, ingawa kwa sasa nnapo,’’anasema.
Akawageukia wafadhili,
kuzitatua changamoto zao, ikiwemo kuwapatia boti dogo kwa ajili ya doria, viatu
vya kuvulia, ili kuepusha hasara za miguuni.
Afisa Ustawi mkoa wa
kaskazini Pemba Nassra Massoud Sanani, anakifahamu kikundi hicho, na amekuwa
akiwaunganisha na wadau mbali mbali wakiwemo FAWE- Zanzibar.
FAWE wamekuwa
wakifanyakazi na taasisi kadhaa za kimataifa kama UN-Women na wameshaanza kuwapatia
mafunzo.
Afisa Miradi FAWE -ofisi
ya Pemba Hija Hamad Issa, anasema hivi karibuni, walikuwa na mafunzo ya siku
nne ya mnyororo wa biashara, ambapo mwakilishi wa kikundi hicho, alishiriki.
‘’FAWE unao mradi wa pamoja,
ambao unawaangalia wajasiriamali wanaojishughulisha na kilimo cha mwani,
majongoo bahari, migomba, ndizi na mihogo ili kuwa wabunifu,’’anafafanua.
Wamekuwa wakifanyakazi
kwa karibu na UN-Women katika mradi huo, ambao wapo wajasiriamali 20 wa wilaya za
Wete na Micheweni, wameshanufaika.
Mwakilishi wa shirika
la kimataifa la UN-Women Tanzania Emile Kivugo Mwakafundu, anafafanua kua mradi
huo, unawalenga wajasiriamali wa mazao ya baharini na nchi kavu.
Mradi huo wa miaka
mitatu, utamalizika mwakani, ambao lengo ni kuona wajasiriamali hao, wanaziongezea
thamani bidhaa zao.
Tena kupitia wadau wao
FAWE- Zanzibar wanawafundisha namna ya kutoziuza bidhaa zao, kama walivyozivuna
na badala yake, wazisarifu.
Kwa mwaka wa fedha
2024/2025 wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar, katika kuimarisha
ufugaji wa zao hilo, kwa kushirikiana na Kampuni ya Zanzibar Marine Hatchery, ilizalisha
vifaranga milioni 1.5.
Kati ya hivyo 80,000
vimegawiwa kwa wafugaji wa Unguja na Pemba na vyingine 70,000 kwa ajili ya
biashara na uzalishaji.
Eneo jingine, sekta ya uvuvi imechangia katika pato la taifa,
umeongezeka kutoka asilimia 4.1 mwaka 2023 hadi kufikia asilimia 5.7 mwaka 2024,
ambapo sekta hiyo imekua kwa asilimia 14.2 kwa mwaka 2024 kutoka asilimia 8.1
mwaka 2023.
Ambapo taarifa za wizara hiyo zinaeleza kuwa, ongezeko
hilo linatokana na hatua mbalimbali za serikali katika kuimarisha sekta ya uvuvi,
kwa kuwawezesha wavuvi, wakulima wa mazao ya baharini, kwa kupatiwa zana za
kisasa.
Mwisho

Comments
Post a Comment