NA RAHEME MOHAMED, PEMBA
MOHAMMED bin Abrahman umaarufu "Mkamandume"
Ni mshirazi kutoka katika nchi ya Iran, mfalme ambae alifika
katika kisiwa cha Pemba mwishoni mwa karne ya 15, yaani miaka 600 iliyopita.
Alifikia mji wa Pujini, kijiji cha Kijito Kame ambapo
alikuwa pamoja na mke wake na mtoto wao mmoja.
Mtoto ambae alijulikana kwa jina la Haroun bin Mohammed bin
Abrahman, na hadi kufikia sasa jina halisi la mke ambae alifikanae kutoka Iran
halijafahamika.
Mfalme Mkamandume, walitoka nchi Iran kwa sababu kulikuwa na
vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuamua kuingia katika mwambao wa Afrika
Mashariki, kutafuta hifadhi.
Walifika hapo pamoja na familia yake kwa kutumia usafiri wa
majini na chombo, ambacho walitumia ilikuwa ni jahazi.
Huo ndio usafiri mashuhuri ulioukitumika katika enzi hizo,
kwani hakukuwa na mwingine zaidi ya jahazi.
Walifikia katika mji wa Pujini, kijiji cha Kijito Kame ambapo
alikaa hapo kwa mashirikiano na wenyeji alipwakitia na kumpa makaazi.
Alishirikiana nao katika mambo mbali mbali ikiwemo misiba na
harusi, muda wote alipoishi katika mji huo.
Kutokana na hadhi yake aliyokuwa nayo, hakupaswa kuishi
katika jamii na kuamua kujenga kasri lake, katika eneo ambalo linajulikana
maarufu kwa 'Mkama Ndume'.
Mfalme Mkama Ndume, alikuwa na uthubutu wa uongozi aliongoza
katika kisiwa cha Pemba, wakati huo huo aliongoza katika mji wa Mombasa Kenya.
Mfalme huyo, katika kipindi chake cha uongozi kisiwani Pemba
aliongoza katika diwani tano.
Moja ya diwani hizo ni Pujini ambapo yeye mwenyewe ilikuwa
ndipo alipoeka makaazi yake makuu na ndio, pakajulikana kwa jina la Mkama
Ndume.
Nyingine ni Wapokomo ipatikana kaskazini Mashariki mwa Pemba,
hapa palijulikana kuwa ni Micheweni.
Watu ambao asiliyao inasadikika kuwa ni jamii ya watu ambao
walitoka nchini Kenya.
Diwani nyingine ni Chwaka-Tumbe hii inapatikana maeneo ya kaskazini
maeneo ya Tumbe hadi Wingwi wilaya ya Micheweni.
Nyingine ni diwani ya utenzi ambayo ilijulikana kwa maeneo
ya Ziwani, Ole na Meli 5 na Pandani.
Diwani nyingine ni Kambaluu ambayo kwa sasa inaitwa rasi
Mkumbuu diwani hii inapatikana maeneo ya Mkumbuu, Ndagoni na Wesha.
Ukoma ni diwani nyingine, inayopatikana maeneo ya kusini
Mkoani, katika maeneo ya Fufuni, Mtambile na Chanjamjawiri.
SABABU YA KUITWA 'MKAMA NDUME'
Mohammed bin Abrahman alijulikana kwa jina la Mkama Ndume,
kutokana na kuwa, wakati wa utawala wake, alitunga sheria kwa wanajamii wa
Pujini.
Sheria ambazo ziliwabama wanawake watu wazima wanapofanya
makosa, kuchukuwa mawe kwa miguu kutoka Vitongoji hadi katika Ngome yake.
Mawe ambayo yalikuwa yakitumiwa kwa kuendeleza ujenzi wa
majengo yaliyojengea wakati huo.
Kwa wanaume watuwazima ambao walifanya makosa, wakati huo
walikamatwa uume wao na kukamuliwa kama Ng'ombe anavyo kamuliwa maziwa.
Hapo ndipo palipopatika jina la 'Mkama Ndume' yaani ‘mkamua
waume’.
Mfalme Mkama Ndume alikuwa na wake wawili, ambao walikuwa
wanaishi katika nyumba moja.
Nyumba hiyo iligawiwa sehemu mbili, ambazo hawakuwahi
kuonana muda wote walioishi hapo.
Katika ngome wa mfalme Mkama Ndume, mulikuwa na kisima,
kilichopachikwa jina la kisima wivu.
Kisima hicho kimo ndani ya ngome ya Mfalme Mkama Ndume, ambacho
kilikuwa kikitumiwa na wake zake hao.
Kiliitwa kisima cha wivu, kwa sababu walitumia wake hao
wawili, ambao waliolewa na mume mmoja kwa usiri bila ya kuonana.
Mfalme Mkama Ndume alihofia iwapo itatokea kukutana kisimani
na kujuwana kuwa ni wake wenza, inawezekana kutokea madhara kwao.
Aliamua kuwatenga na kutokujuwana au kukutana katika hali
yoyote ile, katika maisha.
Wakichota maji katika kisima hicho kwa njia tofauti bila ya
kuonana.
Upande mmoja wa kisima hicho, kulikuwa na ngazi ambayo mke
mmoja, alikuwa anashuka na kuchota maji kwa kutumia kata.
Upande mwingine kulikuwa na roda, ambayo ilifungwa na ndoo,
ndio ambayo akitumia katika kujipatia maji.
Said Omar Said, ambae ni Ofisa Muhifadhi katika eneo hilo la
kihistoria Mkama Ndume, anaeleza kuwa moja miongoni mwa siku, wake wa Mfalme wakiwa
katika eneo la kisimani kuchota maji vyombo vyao vilikutana.
Mke mkubwa akashtushwa na hili ile, na kuamua kumuhadithia
mume wake kuwa ameona kata imegongana na chombo chake, wakati akichota maji.
Hapo ndipo Mkama Ndume alipomtuliza kwa kumfahamisha kuwa,
huenda ikawa ni mzimu uliopo katika kisima hicho.
Mfalme Mkama Ndume, alimshauri mke wake kukwepa uwo muda
aliokwenda, kwa lengo la kuuachia mzimu kutumia na kupanga muda mwingine, ili
asije akamletea madhara.
Mke mkubwa akafahamu hivyo bila ya kujuwa siri ambayo,
ilifichwa na Mkama Ndume.
Mtandao wa wikipedia.org unatufahamisha kuwa, kisima hicho,
kilikuwa na pande mbili zilizogawiwa kwa kuekwa ukuta katikati.
Ukuta ambao, uliwazuwiya wake hao wawili wa Mfalme, bila ya
kuonana katika mazingira hayo.
Upande mmoja, alikuwa anatumia mke mkubwa kwa kuchota maji
kwa kutumia roda.
Upande mwingine alitumia mke mdogo kwa kushuka kwa ngazi na
kuchota maji kwa kutumia kata.
Katika muda wote walioishi hapo haikutokea siku wakakutana
katika hali yoyote ile.
Kwa mara ya kwanza walikutana wakati walipokuwa wanaondoka
pamoja na mume wao.
Aidha historia inatueleza kuwa, kisima hicho kinatumika kwa
masuala ya kiibada mbali mbali za kijadi.
Ibada ambazo watu hufika katika eneo hilo na kuomba maombi
yao, kwa wale walio na matatizo ya kimapenzi.
Mara baada ya mafanikio hufika tena kwa kutoa sadaka kama ni
zawadi kwao, kutokana na mafanikio waliyoyapata.
Zawadi hizo hutumiwa na watu wa jamii iliyozunguka katika
eneo hilo.
NJIA WALIYOPITIA WAKATI WANAONDOKA
Historia inatueleza kuwa, kulikuwa na chumba ambacho
kilikuwepo chini ya bahari, huko ndiko ambako alifikilia Mfalme Mkama Ndume
yeye na wake zake.
Kuna sehemu ambayo walioingia na kupita chini kwa chini hadi
kufika katika chumba hicho.
Kwa mujibu wa utafiti ambae alijulikana kwa jina la Adria
Laviolete aliefika miaka ya 1987 aligundua chumba hicho.
Chumba ambacho kipo chini ya bahari, ambapo alikuwa kuna
ngazi 14, kufika katika chumba hicho.
Hadi kufika sasa haikujulikana tena kuwa ni sehemu gani
ambayo walielekea Mfalme Mkama Ndume, pamoja na wake zake hao.
Mfalme Mohammed bin Abrahman 'Mkama Ndume' alibahatika kuzaa
watoto wanne, ambao wote alizaa na mke mkubwa.
Mtoto wake mmoja, aliitwa Haroun bin Mohammed bin Abrahman
ambae alitawala katika eneo la Chwaka- Tumbe.
Mwingine aliitwa Mjawiri, ambae alikuwepo maeneo ya Chanja
mjawiri, kama jina lilivyo maarufu kwa sasa.
Huyu inasemekana kuwa, mara baada ya kuondoka baba yake,
aliomba kupasuka ardhi na kuingia na hakujilikana alikokwenda.
Mwingine alijulikana kwa jina la Mwana mtoto ambae, akiishi
katika kijiji cha mwana mtoto, kilichopo hapo hapo Pujini.
Na mwingine hakuwahi kupatikana jina lake kutokana na kuwa
alifariki akiwa hajapatiwa jina.
Said Omar Said kutoka eneo la hifadhi ya Mkama Ndume,
anafahamisha kuwa, kiwango cha watalii ambao hufika katika ngome hiyo ni ndogo
sana na hairidhishi.
Kwani kwa mwaka, hupata ugeni wa wanafunzi wanaokuja
kujifunza wasiozidi 800 na wageni wa ndani ya nchi au wakaazi wa kisiwa hichi
cha Pemba, wasiozidi 100.
Wkati ambapo watalii wa nje hali ikiwa imezidi kupunguza wao
ni wastani wa wageni 50, jambo ambalo kwa idadi hiyo ni ndogo.
Said amefahamisha kuwa, iwapo jamii itapata mwamko wa kufika
katika sehemu za kihistoria, kuona uhalisia wa maeneo waliyoishi watawala wa
zamani.
Wanaweza kujijengea uelewa zaidi kuliko kutosheka na masomo
wanayosoma wanapokuwa madarasani, au hadithi na wazazi nyumbani.
Kwa upande wake Saleh Omar Juma Mkuu wa divisheni wa Makumbusho
na Mambo ya Kale Pemba anasema, taasisi mbalimbali zinazohusiana na Mambo ya
utalii, kuwaelekeza watalii wanapofika Unguja kufika Pemba.
Anasema kuwa, watakapofika Pemba, wanaweza kusaidia kuingiza
mapato ya serikali na kuongeza kuenea kwa historia ya visiwa hivi.
Amesema iwapo watafanya hivyo wanaweza kuwasaidia wao kwa kuongeza
idadi ya wageni.
MWISHO.


Comments
Post a Comment