NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
“NIWEKEE kisongo pawa 2000, supu weka nyingi na
pili pili kwa mbali na kiungwa”, lugha za kuagizia supu ya Mwata.
Sio lugha ngeni kwa wafanya biashara na watu wanaouza supu
hiyo ya Mwata hususan katika maeneo ya Kangani na vitongoji vyake.
Wenyewe hutumia jina la “kisongopawa”kama umaarufu lakini jina
halisi ni Mwata, ndilo watu wengi kutoka maeneo mbali mbali hufahamu kwa
haraka.
Na jina la kisongopawa si rasmi na si lenye kufahamika
isipokua kwa wenyeji wa maeneo ya Kangani na jirani ambako ndio mwata huvuliwa na kuliwa .
Mwata ni aina ya viumbe vipatikanavyo pwani, ambacho
hutumiwa kwa ajili ya chakula au kitoweo kama ilivyo viumbe vingi vya baharini,
ingawa umetofautiana navyo kwa kiasi kikubwa hata uvuvi wake.
Mwata kisiwani Pemba hupatikana zaidi na kuhesabiwa kama ni
kitoweo adhimu katika Pwani ya Jemele iliopo shehia ya Kangani wilaya ya Mkoani
mkoa wa kusini Pemba.
Ingawa baadhi ya watu hueleza yapo maeneo mingine
yanayopatikana Mwata, lakini watu wa maeneo hayo hawauchukulii kama ni chakula.
Badala yake hutumia kama chambo cha kuvulia samaki au viumbe wingine
wa baharini, huku baadhi ya watu wakisema huo ni tofauti na ule unaovuliwa
Kangani na kuliwa.
Ila kuzingatiwa kwake kama kitoweleo muhimu tena cha enzi na
enzi kwa wakaazi wa Kangani kumeipa kijiji hicho na maeneo jirani ya Mjimbini
na Kukuu umaarufu mkubwa.
Na hadi sasa ukitaja Kangani, Mjimbini na Kukuu kwa anaekujua
au kukusikia hutanguliza swali kama mwata upo? ni sawa na kusema Pemba na
karafuu.
Na umaarufu huu umekaa vichwani kwa watu miaka na miaka hadi
sasa, ambapo unazingatiwa na vizazi kwa vizazi.
HUPATIKANA KATIKA
ENEO GANI?
Aina hii ya kiumbe cha baharini, hupatikana katika sehemu za
pwani zenye mchanga mweupe ambapo panafikiwa na maji, yaani sehemu ambazo maji yanaingia na kutoka (kupwa na kujaa).
Fumu Haji ni miongoni mwa wavuvi maarufu wa Mwata anasema, viumbe
hao huonekana zaidi sehemu zenye usafi wa mazingira na mchanga mwingi
uliotulia.
“Kila sehemu ikiwa safi zaidi na mchanga mwingi na unaofikiwa
na maji na kutoka, ndipo viumbe hawa huonekana zaidi kuliko sehemu nyingine”,
anafahamisha.
Anasema si rahisi kuonekana na kila mtu pale anapofika pwani
kwa lengo la kuwatafuta, kwani si watu wengi ambao wanaweza kutambua uwepo wa
Mwata katika eneo fulani.
Wakati Makame Ali Makame nae ni mvuvi wa mwata anaeleza, ‘’sio
kila mvuvi anaweza kuvua Mwata kwani
unaweza kuwa mvuvi wa samaki na usiweze kuvua Mwata’’.
Maana sehemu unapopatikana kunahitaji uzoefu wa hali ya juu,
kwakuwa hata ishara zinazo ashiria uwepo wa kiumbe hicho zinamuhitaji mzoefu.
Anasema ishara kama kishimo ndio inayoonesha kuwepo kwa mwata katika
eneo, ila pia kishimo hicho si chakueleweka kwa kila mmoja.
Anaeleza wakati ambao maji hukauka ndio wakati unaopatikana
mwata na bamvua likiisha yaani maji yakijaa ni vigumu Mwata kupatikana.
UVUVI
WAKE
Mchakato wa uvuvi wa mwata unatofautiana kidogo na uvuvi wa
viumbe kama samaki, Pweza na hata viumbe vyingine wa baharini ingawa wote kwa
pamoja wanaishi katika mazingira yanayofanana.
Abass Haji Mkaazi wa Kangani anasema, nilazima mvuvi awe na
ujiti maalum wenye urefu kutoka ncha
ya kidole cha kati cha mkono hadi kwenye
“mirfaki” yaani futi moja.
Anaeleza ujiti huo unaweza kuwa wa mti kama Mkoko michanga,
Mbungo na miti mingine yenye ncha kali na kupinda pinda.
Anaongeza sio kila mti wenye ncha unaweza kutumika kuvulia
Mwata, akitolea mfano mti wa mpenda pendapo ingawa unancha ila hauwezi kutumika
kuvulia Mwata.
“Kuvua Mwata tunatumia ujiti maalumu wenye urefu wa futi moja
ambao una ncha kali, na mara nyingi tunatumia miti kama Mikoko michanga, ila si
kila mti unaweza kutumia” anafahamisha.
MUONEKANO
WA MWATA
Muonekano wa mwata baada ya kuvuliwa ni mithili ya uchango wa
kuku ama bata, kwa upana kama huo kwa wale wachanga na wapevu wakiwa ni wenye
kuongezeka kidogo.
Urefu wake unaweza kufikia hadi sentimita 30 kwa waliopea na
sentimita 20 hadi 25 kwa ambao hawajapea vizuri.
Mwata ukivuliwa unakua ni wenye kujifumba ambapo ndani yake
huonekana kuwa na mchanga mweupe wa pwani na muda mwingine hua na chango ambazo
ni kidogo sana.
Mara nyingi muonekano wake huwapa mashaka walaji hasa wale
wanaouona kwa mara ya kwanza, kwani huufananisha na uchango wa kuku na wengi
hushindwa kuula hasa wale ambao hawauoni sana.
Mwata huwa ni warangi nyeupe kwa ule mchanga au mpevu kiasi,
na rangi manjano kwa ule mpevu zaidi ambao wengi wakiuona kwa mara ya kwanza
hushtuka.
Aina hii ya mwata mkubwa hupatikana kwa kuzamia na ni madrassa
sana kupatikana na umepewa jina la “mwata koko”.
UPISHI WAKE
Mwata hupikwa kwa namna tofauti, kulingana na matakwa ya mlaji
ambapo hutofautiana ladha kulingana na namna ya upishi.
Kuna wanaopika kwa mchemsho wa kawaida wa mwata maji na
chumvi, huku wataalamu wa upishi huo wakisema ladha huwa nzuri zaidi ukipikiwa
maji ya chumvi “yabaharini”.
Mara chache hutiwa pilipili, na aina hii ya mchemsho ndio
ambao hupendwa na watu wengi hasa wanaojizowesha kuula.
Na wingine hupikwa mchemsho kwa kuongeza baadhi ya vifaa kama
kitunguu swaumu, uzile na bizari ambapo aina hii ya mchemsho wa mwata hutumiwa
na wafanyabiashara wingi, kwani ni yenye kuwavutia wateja, na hupendelewa zaidi
na wazoefu wa ulaji huu.
Mwata hupikwa kwa kukaangwa, na aina hii ya upishi hupendelewa
zaidi na watu ambao si wazoefu wa ulaji wa mwata.
WALAJI
WAKE/WATEJA WAKE
Mwata ni aina ya kitoweo ambacho hupendelewa zaidi na wakaazi
wa maeneo ya karibu na bahari au ambao washawahi kuishi katika maeneo hayo.
Anasema mmoja kati ya wavuvi wa Mwata Khadija Mcha Amour wa
Kangani kwa miaka ya nyuma, haukuwa na wateja wengi wala bei inayoridhisha.
Anaeleza mwata ulichukuliwa kama ni kitoweleo cha waliokosa
pesa au waliokosa samaki na kuufanya kuwa ni chaguo lao la mwisho.
Anaeleza mwata haukua na thamani kama ilivyo sasa, na haukua
na wateja wa uhakika wala soko la uhakika na walikua wanavua kama bahati
nasibu, na mvuvi hakuwa anapata mteja akaridhika.
Anafahamisha walikuwa wakiuza kwa kupitisha mitaani ambapo
mwata ulipangwa siniani na kupewa watoto kuutembeza na muda mwingi huenda nao
masafa marefu bila kupata wateja.
“Kwa miaka ya nyuma mwata haukuwa na wateja wengi wala bei inayoridhisha, na haukuwa na wateja wa uhakika wala soko la uhakika
tulikuwa tunavua kama bahati nasibu, na
mara nyingi tulikua tuna kula wenyewe”, anaeleza.
Khadija anasema mbali na kukosa wateja pia thamani yake ilikua
ndogo sana, kwani fungu lenye Mwata 10 hadi 15 lilikuwa likiuzwa kwa shillingi 500
bei ambayo haikuendana na juhudi za
mvuvi.
Time Kebu Ali, pia ni mvuvi wa mwata anasema wateja wao
wengine maarufu ni wafanyabiashara, anasema kutokana na umaarufu wa mwata siku
hizi pia kuna kundi la wafanyabiasha ambao hununua mbichi na kupika supu na
kuuza.
Anaeleza hili pia limeongeza thamani kwa wavuvi kwani
limefanya mwata kuwa wa thamani na wenye kumfaidisha mvuvi, kwani kwa sasa
fungu la jumla ya mwata 6 au 8 huuzwa kwa shilling 1000, bei yenye manufaa kwa
mvuvi.
Anafafanua pamoja na kuongezeka thamani Mwata haupatikani kwa
wingi kama ulivyokua zamani, hii ni kutokana na mabadiliko ya tabia ya nchi
yanayopelekea kujaa kwa maji chumvi katika sehemu zinazotegemewa kutoka maji
ili mwata uishi.
Ali Mohamed Makame ni mfanyabiashara wa supu ya mwata ambayo
imempa jina la umaarufu (kisongo pawa) anaeleza, wateja wake wengi hukimbilia
supu ya mwata kuliko aina nyengine ya supu.
Anafahamisha ingawa kiingilio ni shillingi 500 ila wapo watu
wanakunywa hata ya 5000 kitako kimoja kutokana na upenzi walionao kwa supu
hiyo.
Bikombo Khamis ni muuza supu ya mwata anafafanua, wanaume ndio
huvutiwa zaidi na supu ya Mwata kuliko wanawake na wateja wake, wengi ni watu
wazima kuliko vijana.
“Supu ya mwata ni supu inayopendwa zaidi kuliko aina nyingine
ya supu kwa hizi nnazouza mimi, na wateja wangu wengi ni wanaume kuliko
wanawake”, anaeleza.
FAIDA ZA KIAFYA
Kama ilivyo kwa vitoweo vya baharini kuwa na umuhimu mkubwa
kwa ujenzi wa afya ya binaadamu mwata pia una umuhimu mkubwa kiafya.
Mwata unamadini ya Iodini na Amaino asidi yanayotengeneza
homoni za kudhibiti uvimbe katika mwili.
Huzalisha kabohaidreti inayosaidia kuimarisha mfumo wa
mmeng’enyo wa chakula, mwata pia
huimarisha afya ya mifupa.
Mmoja ya wakaazi wa Kangani Jamila Khatibu Faki anasema, wao
hula mwata kama sio kitoweo rasmi, bali ni kama kiburudisho au nyongeza tu,
kama ilivyo kachumbari kwa baadhi ya watu.
Nae Far-hat Mohamed wa Kangani anasema, umaarufu wa mwata
ni miongoni mwa vitu wanavyojivunia,
kwani umebeba utambulisho wao katika
maeneo mbali mbali, kama ilivyo vyakula vyingine.
MWISHO.


.jpg)

Comments
Post a Comment