NA
MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
KISIWANI
Pemba, kuna kijiji kimoja chenye historia ya pekee, kijuilikanacho kwa jina la
Jambangome.
Kijiji hicho kipo
katika maeneo ya karibu na Wambaa, wilaya ya Mkoani, mkoa wa kusini Pemba.
Kipo umbali wa kilometa 31 kutoka mji mkuu wa Pemba wa
kisasa Chake chake, ambapo ni umbali wa dakika 49 hadi saa moja, kwa usafiri wa gari ambayo si ya abiria.
Jambangome ina historia kubwa na yakuvutia inapoelezwa
kwa vizazi vya sasa na wageni wanaoingia na kutaka kuujuwa kiundani mji huo.
Kwani inaaminika mji huo, ndio wa kwanza kuhamiwa na
kukaliwa na watu katika kisiwa hicho cha Pemba.
Historia inatueleza kuwa, Jambangome ilikaliwa na
wahindi wa jamii ya Mabohora, ambao asili yao ni “Wagujurati” kutoka India.
Walihamia, baada ya kushauriwa na mababu zao kutafuta
fursa mpya za kibiashara, katika ukanda wa Afrika mashariki, baada ya kupatwa
na njaa kali huko katika jamii zao.
Neno hili “Bohora” linatokana na neno la kigujurati
lenye maana biashara, ambalo asili yake ni India, na ni neno la utambulisho wa
kihistoria kwa wafanyabiashara.
Inaaminika kuwa, Jambangome ulikuwa ni mji wa bandari
na kitovu kikubwa cha kibiashara kisiwani Pemba, hususani kwa mkoa wa kusini.
Na mji huo ulidumu
kuanzia karne ya 18 hadi 20, kuanzia mwaka 1911/12.
Mataifa mbali mbali ya Asia, Europe na hata Afrika
hasa Afrika ya Mashariki, walifika katika eneo hilo, kwa shughuli za kibiashara.
Ambazo zilifanya mji huo enzi hizo, kuwa ni miongoni
mwa miji mikubwa ya Afrika mashariki na kati, kwa shughuli za biashara.
Ilikuwa ni jambo rahisi sana kwa wafanyabiashara hao
kuingia katika mji huo kwa kutumia bahari ya Jambangome kutokana na jiografia
yake.
Huku ikielezwa usafiri wa karne hizo, ulikuwa ni
Mabedeni, Majahazi, na Mashua.
Wanahistoria wanaeleza, ingawa teknolojia ya
ujenzi haikuwepo enzi hizo, lakini majengo
mazuri na yenye thamani kwa wakati huo
yalijengwa, huku mingine yakibeba shughuli za utawala na uongozi.
Hii ikiwa na maana, kulikuwa na maofisi mbali mbali ya
kiutawala kama vile Polisi, Mahakama, Magereza na skuli ya mwanzo ilianzia hapo.
Na yote hayo yaliendeshwa na kusimamiwa na waarabu na wahindi,
huku yakifanya kijiji hicho kuingia katika machapisho ya historia.
Kwa mujibu wa historia, inayoelezwa na Afisa mambo ya Kale
Pemba Haji Seif Yussuf, anasema mnamo karne 19 mji huo, ulikaliwa na wahindi wa
jamii ya mabohora na miongoni mwa majengo waliojenga ni skuli.
Anaeleza kuwa, eneo hilo lilijengwa kwa ajili ya
watoto wao, ambayo ilibeba kumbukumbu ya kua skuli ya mwanzo, kujengwa katika
kisiwa hicho kwa mujibu wa historia.
Anasema inagawa wahindi hao, walifika katika eneo hilo
kwa ajili ya shughuli za biashara za bidhaa za viungo kama vile karafuu, lakini
walijiimarisha na kuufanya mji huo kua ni wenye kuwavutia wengi.
ILIVYOJENGWA SKULI YA KWANZA PEMBA
Akitoa historia ya ujenzi wa skuli hiyo, ofisa huyo
anasema hadi sasa, historia haijaweka wazi skuli hiyo ilikua na vyumba vingapi.
Na hii ni kutokana na kutofanyiwa utafiti wa kitaalamu,
unaolenga kugundua mabaki ya vitu mbali mbali vya zamani yaani (Excavation).
“Kihistoria inaaminika skuli ya mwanzo kujengwa
kisiwani Pemba, ilikua ni katika kijiji cha Jambangome wilaya ya Mkoani, ila
bado hakujafanyika utafiti wa kitaalamu wa kugundua mabaki ya vitu vya zamani.
Kwa mujibu wa historia inayoelezwa na Afisa huyo jengo hilo lilijengwa kwa zana za asili kama,
mawe na chokaa, ambavyo kwa wakati huo, ndio vifaaa maarufu vya kujengea.
Ingawa vifaa vyake havikua vya kisasa, ila jengo hilo lilikua na umadhubuti wa hali ya juu, uliosababishwa
na utaalamu waliokua nao wajenzi wa jengo hilo, ambao ni wahindi wenyewe.
“Jengo la skuli ya mwanzo Pemba, lilojengwa Jambangome
kwa kutumia mawe na chokaa, vifaa hivi sio vya kisasa, ila kwa wakati huo
lilikua imara kuliko yanayojengwa sasa,’’anasema.
Wakati wa ujenzi wake, kazi zenye hadhi na thamani
kama za usimamizi, zilikua zikifanywa na wenyewe wahindi, na wazawa walitumiwa
kufanya kazi za nguvu ambazo hazikuhitaji ujuzi kama kubeba mawe na chokaa.
Jengo hilo halikuchukua muda mrefu kukamilika,
kutokana na ufanisi na utayari waliokua nao wahindi, ambao ndio wajenzi wakuu
wa skuli hiyo.
ELIMU
ILIOSOMESHWA
Kwa mujibu wa ufafanuzi uliotolewa na Ofisa huyo, ni
kwamba elimu iliotolewa ilikuwa ni hesabu ili kuwaandaa wanafunzi kua na uwezo
wa kudhibiti mali za mabwana (watawala)
wa enzi hizo.
Soma la lugha ya kiengereza ilitolewa, ili watoto wao
wapate fursa za kujumuika kibiashara kutoka kwa wafanyabiasha wa kiengereza,
amabo walionekana kua na nguvu kubwa za kibiashara.
Mbali na lugha, inaaminika kwamba elimu ya maadili na utawala ilitolewa, ili iweze
kuwasaidia kuimarisha mahusiano ya kibiashara baina yao, pamoja na kujua mbinu
za kiutawala na kuandaana katika uongozi.
“Skuli hii wanafunzi walisomeshwa masomo kama hesabu,
ili waweze kusimamia biashara, maadili na lugha ili kuimarisha mawasiliano na
mahusiano ya kibiashara, pamoja na utawala,’’anafafanua.
Kumbe wazawa wa Jambangome, hawakupata fursa za kusoma
kwa wakati huo na walibaki kuwa ni wakulima ama wachukuzi (wapagazi),
wavuvi au wafanyakazi wa majumbani pekee.
NJIA,
VIFAA VILIVYOTUMIKA KUSOMESHEA
Kwani mnamo karne ya 19 na 20, njia za kufundishia na
kujifunzia zilikua si rasmi na muda mwingi, waalimu walitumia vifaa vya asili
kulingana na mazingira yao.
Inasadikika waalimu waliosomesha skuli hiyo, walitumia
vitabu na baadae kuhifadhisha wanafunzi kama ni njia yao kuu ya kufundishia.
Kwa njia hii, wanafunzi walilazimika kuhifadhi elimu
waliopewa na waalimu wao, ili waweze kujibia mitihani pamoja na kuitumia katika
maisha yao ya kila siku.
“Hapakua na njia rasmi ya kufundishia na kujifunza, hivyo
waalimu walitumia njia za asili za kujifunzia, na walitumia vitabu kufundishia,
wanafunzi walihifadhi kichwani elimu waliopewa”, anaeleza.
Historia inatuambia kabla ya Zanzibar, kupata uhuru
wake hakukua na usawa katika upatikanaji wa elimu.
Hivyo elimu ilitolewa kwa kuangalia rangi, tofauti za
kitabaka na kwa gharama kubwa, jambo lililowanyima wazawa fursa za elimu.
Maana Ofisa Mambo ya Kale Pemba, Haji Seif anasema
skuli ya mwanzo Pemba waalimu wake walikua ni miongoni mwa wahindi, ambao ndio
watawala na wajenzi wa skuli hiyo.
Kwani hawakuwapa fursa wazawa wa Jambangome kujifunza
wala kusomesha wingine, hivyo walikosa sifa ya kua waalimu.
Kwani wanafunzi walikua ni watoto wa watawala wa eneo
hilo, ambao walipewa kipaumbele zaidi, kutokana na aina ya elimu inayotolewa.
Kwani ililenga kuwaandaa kibiashara na kiutawala
watoto wao na gharama za elimu iliyotolewa, hawakuimudu wazawa.
Mwishoni mwa mwaka 1911, (wazungu, wamishini–Missionaries)
walifika Jambangome, kwa matembezi lakini baadae walifanya makaazi yao katika
mji huo.
Hatimae walivamia na kudhibiti mianya yote ya mapato
ikiwemo biashara, hali iliosababisha wahindi wa jamii ya mabohora kusambaratika.
Ambapo walienea katika miji mbali mbali ya Pemba ikiwa
ni miji ya Chake chake, Kengeja na Mkoani
ambayo kwa sasa, ndio miji yenye mvuto kwa kisiwa cha Pemba.
Baada ya muda kupita, ndipo skuli hiyo ilipo hamia
katika mji wa Mkoani, na sasa inajuilikana kama skuli ya Uweleni.
Ilikua mwaka 1932, ambapo kwanza ilijuilikana kwa jina
la Mkoani Government School, chini ya uongozi wa Abdallah Sadalla, akiwa ni
mwalimu mkuu wa mwanzo.
skuli ya Uweleni Mkoani Pemba
Mwaka 1959 skuli hio, ilifanywa kuwa ni ya wanaume pekee na hivyo kubadilishwa jina na kuitwa ‘Mkoani
Boys School’.
Mwaka 1969, ilifanywa tena kuwa skuli ya mchanganyiko
wa wanafunzi wanaume na wanawake na kubadilishwa jina na kuitwa skuli Uweleni.
Mwaka huo huo wa 1969, skuli hiyo ilipandishwa daraja
na hivyo kufunguliwa sekondari ya mwanzo.
Baadae mwaka1988, ilipandishwa daraja na kuwa skuli ya
sekondari tu, baada ya kufunguliwa darasa la 12 kubadilishwa jina na kuitwa skuli ya sekondari Uweleni.
Mwaka 2005, skuli hii ilipandishwa tena daraja na hadi
sasa inatoa elimu ya juu ya kidato cha tano na sita.
Ambapo ikiwa ni skuli pekee ya kiwango hicho kwa
wilaya ya Mkoani, hadi mwaka 2018 ilipofunguliwa rasmi skuli ya MOHAMMED JUMA
PINDUA.
HALI
ILIVYO KWA SASA
Katika eneo hilo la kihistoria la Jambangome, kwasasa
kumebakiwa na magofu na vijumba vidogo vidogo vya wazawa.
Ambapo mabaki ya skuli hiyo ya mwanzo kujengwa Pemba,
yamezomgwa na majani na miti mikubwa ya Mlandege.
Waswahili wanasema, chakale ni dhahabu, wakimaanisha
chochote cha zamani kina thamani zaidi.
Hivyo ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha analinda
anapigania na kutunza historia ya Zanzibar kwa manufaa ya kizazi chote cha kizanzibari.
Kwani mabaki hayo ya skuli na mji wa Jambangome yatakapoachwa bila matunzo, tutawaachia nini
watoto wetu na vijukuu vyetu juu ya mji huo wa mwanzoni mwa karne ya 18.
MWISHO


Comments
Post a Comment