NA ZUHURA JABIR
Katika jamii, mara nyingi mafanikio hupimwa kwa kiwango cha
elimu, mali au nafasi aliyonayo mtu. Hata hivyo, kuna watu ambao maisha yao
yanatufundisha kwamba mafanikio makubwa huanza pale mtu anapoamua kujiamini,
kupambana na changamoto na kutokubali mazingira yamzuie kufikia ndoto zake.
Hii ni simulizi ya Fatma Suleiman Mussa, mwanamke mwenye
ulemavu anayeishi Jumbi, Zanzibar, ambaye licha ya changamoto alizokutana nazo
tangu akiwa mtoto, ameamua kutumia uwezo alionao kujiajiri, kusaidia familia
yake na kuwa mfano kwa wanawake wengine wenye ulemavu. Safari yake imejaa
changamoto, lakini pia ni ushahidi kwamba “ulemavu si mwisho wa ndoto.”
SAFARI YA ELIMU NA MAISHA
Fatma ni mtoto wa pili katika familia ya watoto wanne, wote
wakiwa wa kike. Alianza elimu ya msingi katika Skuli ya Tunguu na baadaye
aliendelea hadi kidato cha pili mwaka 2015. Alipata nafasi ya kuendelea na
kidato cha tatu katika Skuli ya Kibele, lakini changamoto mbalimbali zilimfanya
ashindwe kuendelea na masomo.
Hata hivyo, mama yake hakukubali kuona ndoto ya mwanawe ya
kupata elimu ikizimika. Alimtafutia fursa nyingine ya masomo Mazizini, ambako
Fatma aliendelea na masomo katika Kiembe Samaki na hatimaye akafanikiwa
kuhitimu kidato cha nne.
Baada ya kumaliza masomo, Fatma alianza kujifunza
ujasiriamali, ikiwemo utengenezaji wa sabuni, dawa za chooni na Jiki.
Hakusimama hapo. Alijikita pia katika uwakala na baadaye akaanzisha duka pamoja
na mume wake. Kwa Fatma, mafanikio
hayakuwa jambo la kusubiri, bali safari ya kuendelea kujifunza na kujaribu
fursa mbalimbali.
Ulemavu wa Fatma ulitokea akiwa na umri wa miezi sita,
wakati bado akiwa kitandani. Hali hiyo ilimfanya kwa nyakati fulani ajione
hawezi kufikia baadhi ya malengo yake. Lakini
alipofikisha miaka 20, alianza kujitambua zaidi na kuelewa kwamba ulemavu
haupaswi kuwa sababu ya kukataa tamaa.
Katika safari hiyo, mama yake alikuwa nguzo muhimu. Fatma
anakumbuka maneno ya mama yake yaliyompa nguvu ya kuendelea kupambana:
“Hakuna
kukataa tamaa. Leo nipo, kesho sipo. Usiwe tegemezi kwa watu.”
Maneno hayo yameendelea kuwa sehemu ya msukumo wa maisha
yake. Badala ya kuangalia kile ambacho hawezi kufanya, Fatma aliamua kuangalia
kile anachoweza kufanya na kukiendeleza.
UFUMAJI NA BIASHARA ILIYOMPA MATUMAINI
Mwaka 2021, Fatma alianza kujifunza na kufanya ufumaji wa
mikoba kwa kutumia shanga. Ujuzi huo aliupata kutoka kwa dada yake na baadaye
akaendelea kuukuza kwa juhudi zake mwenyewe.
Leo anatengeneza mikoba ya shanga na bidhaa nyingine
mbalimbali. Aidha, anauza udi, haliud na mafuta ya pafyum. Baadhi ya bidhaa
hizo alianza kuzifanya takribani miezi mitatu iliyopita baada ya kujifunza
kupitia mitandao ya kijamii.
Kwa mujibu wa Fatma, sababu kubwa ya kuingia katika biashara
ni kutafuta kipato cha kujikimu, kuondokana na utegemezi na kujiepusha na
maisha ya kuomba msaada kila mara.
“Nilitaka
kujitegemea na kujiepusha kuwa ombaomba kwa watu. Nikaona nina uwezo wa kufanya
kazi na kujenga maisha yangu kupitia biashara.”
“Walisema
siwezi, lakini sikuacha”
Safari ya ujasiriamali haijawa rahisi kwake. Anakabiliwa na
changamoto za ukosefu wa mtaji, kupata wateja, mazingira yasiyokuwa rafiki kwa
mtu mwenye ulemavu na wakati mwingine kukutana na watu wanaomdharau au kumwona
hawezi kufanya biashara kutokana na hali yake.
Lakini Fatma hakukubali maneno hayo yawe hukumu ya maisha
yake.
“Sikukubali
maneno yao yanivunje moyo. Niliendelea kujifunza kwa bidii na kuamini uwezo
wangu. Leo bidii yangu imeonyesha kwamba ulemavu si kikwazo cha kufikia malengo
yangu.”
Kauli hiyo inaonesha msimamo wake wa kutokuruhusu mtazamo wa
wengine uamue thamani au uwezo wake.
UONGOZI UNAANZIA KATIKA KUJISIMAMIA
Kwa Fatma, mwanamke anayejiajiri na kusimamia maisha yake
anaweza kuitwa kiongozi. Kwake, uongozi haupo kwenye cheo pekee, bali
unaonekana katika uwezo wa kufanya maamuzi, kuwajibika na kuwa mfano kwa
wengine. Biashara imemfundisha kuwa
kiongozi mzuri anatakiwa kuwa mvumilivu, kujiamini, kufanya maamuzi, kusikiliza
wengine na kutokata tamaa anapokutana na changamoto.
Amejifunza kufanya maamuzi kuhusu biashara yake mwenyewe,
kuanzia kuchagua bidhaa za kutengeneza, kupanga bei, kutafuta wateja hadi
kusimamia kipato chake.
“Nimejifunza
kujiamini katika maamuzi yangu na kutokata tamaa ninapokutana na changamoto.”
Kwa upande wake, misingi ya uongozi bora ni kujiamini, kuwa
na hekima na busara, uaminifu, uvumilivu, heshima na kuwajibika.
CHANGAMOTO ZA WANAWAKE WENYE ULEMAVU
Fatma anaamini kuwa bado kuna changamoto kubwa kwa wanawake
wenye ulemavu, hasa katika kupata mitaji, masoko, mafunzo na mazingira rafiki
ya kufanya shughuli za kiuchumi.
Anasema wakati mwingine jamii haiangalii uwezo wa mtu mwenye
ulemavu, bali huangalia ulemavu wake kwanza. Mtazamo huo, kwa mujibu wake,
unaweza kuwanyima wanawake wengi fursa ya kujiajiri na kuchangia maendeleo ya
familia na jamii.
“Tusiangalie
ulemavu wetu tu, bali watuangalie kwa uwezo na kazi tunazoweza kufanya.
Tunahitaji kupewa fursa, kuaminiwa na kusaidiwa ili tuweze kujitegemea na
kuchangia maendeleo ya jamii.”
Fatma anaomba wanawake wenye ulemavu wawezeshwe kwa mitaji,
mafunzo ya biashara na utengenezaji wa bidhaa, pamoja na kusaidiwa kupata
masoko.
Anaamini kuwa mazingira yakiboreshwa na fursa zikawa sawa,
wanawake wenye ulemavu wanaweza kukuza biashara zao, kuongeza kipato na
kuchangia katika maendeleo ya nchi.
USHUHUDA KUTOKA KWA WATU WALIOMZUNGUKA
Mume wa Fatma, Juma Shaaban, anasema anajivunia juhudi za
mke wake katika kupambana na changamoto na kujitahidi kuijenga familia.
“Fatma
ni mfano kwa watu wengine wenye ulemavu kwamba wanaweza kujiamini, kufanya kazi
na kujenga maisha yao. Namshukuru kwa kuwa mwanamke mwenye nguvu na
anayepambana kwa ajili ya familia yetu.”
Dada yake, Muzna Suleiman Mussa, anamuelezea Fatma kama
mwanamke mwenye juhudi, uvumilivu na bidii katika kujenga maisha yake na
familia yake.
“Najivunia
kuona anavyoendelea kupambana na changamoto na kutafuta njia ya kujitegemea.”
Naye dada yake mwingine, Khaitham Suleiman Mussa, anasema
Fatma hajawahi kuruhusu changamoto zimfanye akate tamaa.
“Pamoja
na changamoto anazopitia, kamwe hakuwahi kukataa tamaa. Anaendelea kupambana
kufikia malengo yake. Kama mdogo wake, najivunia kuwa na dada kama yeye.”
Kwa upande wa wateja, Mauwa Aliy Khamis anasema amemfahamu
Fatma kupitia biashara yake na amemuona akifanya kazi kwa juhudi, akiwahudumia
watu vizuri na kwa uaminifu.
Mteja mwingine, Ali Kombo Maalim, anasema Fatma ni mwanamke
anayestahili kuwa mfano kwa wengine kutokana na bidii, ujasiri na moyo wake wa
kujitegemea.
“Ulemavu
haumzui mtu kufanya kazi. Fatma anauwezo wa kufanya biashara na kutoa bidhaa
zenye ubora. Najivunia kununua bidhaa kwake.”
NDOTO YA KUWAWEZESHA WANAWAKE WENGINE
Pamoja na mafanikio aliyoyapata, Fatma bado ana ndoto kubwa.
Anatamani kukuza biashara yake, kupata wateja wengi zaidi na kuongeza aina na
kiwango cha bidhaa anazotengeneza.
Ndoto yake kubwa zaidi ni kuona biashara yake inakuwa na
uwezo wa kuwapa wanawake wengine, hasa wanawake wenye ulemavu, nafasi ya
kujifunza na kujiajiri.
Kwa mtazamo wake, mafanikio si kupata pesa pekee. Ni uwezo
wa kujitegemea, kufanya kazi unayoipenda, kushinda changamoto na kuwa mfano kwa
wengine. Anasema mafanikio anayojivunia
zaidi ni kujifunza ufumaji, kuanzisha biashara yake mwenyewe na kufikia hatua
ya kujitegemea licha ya changamoto anazokutana nazo.
UJUMBE KWA WANAWAKE WENYE ULEMAVU
Fatma anatoa wito kwa wanawake wengine wenye ulemavu
kutokata tamaa wala kujiona hawawezi.
“Kila
mtu ana uwezo wake. Changamoto hazimaanishi huwezi kufanikiwa. Jiamini, anza
pale ulipo na endelea kujifunza. Mungu akipenda, juhudi na uvumilivu vinaweza
kukufikisha kwenye mafanikio.”
Anaamini kwamba mtu hapaswi kusubiri mpaka apate kila kitu
ndipo aanze. Anachohitaji ni kujiamini, kuanza na kile alichonacho na kuendelea
kuongeza ujuzi.
WITO KWA JAMII NA VIONGOZI
Fatma pia anaiomba jamii ibadili mtazamo kuhusu wanawake
wenye ulemavu na kutambua kuwa wao ni sehemu muhimu ya maendeleo. Kwa viongozi, anaomba kuwepo kwa mazingira
wezeshi zaidi, ikiwa ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa mitaji, mafunzo ya
ujasiriamali na masoko ya bidhaa zinazotengenezwa na wanawake wenye ulemavu.
Pia anataka wanawake wenye ulemavu wasikilizwe na
kushirikishwa katika mipango ya maendeleo kwa sababu wana uwezo wa kufanya
maamuzi, kuwajibika na kutoa mchango katika jamii kama watu wengine.
SHERIA INASEMAJE
1.
Kifungu cha 4 — Kanuni za msingi
Sheria
Na. 9 ya 2010, Kifungu cha 4 kinaweka misingi ambayo Serikali na jamii
wanapaswa kuzingatia kuhusu watu wenye ulemavu.
Misingi
hiyo inajumuisha:
●kuheshimu
utu wa mtu mwenye ulemavu;
●kutokubagua
mtu kwa sababu ya ulemavu;
●ushiriki
kamili wa watu wenye ulemavu katika jamii;
usawa
wa fursa;
●upatikanaji
wa huduma na mazingira;
●usawa
kati ya wanaume na wanawake wenye ulemavu; na
kiwango
cha msingi cha maisha na ulinzi wa kijamii.
Maana
yake kwenye biashara: mtu mwenye ulemavu hapaswi kunyimwa fursa ya kushiriki
katika shughuli za kiuchumi kwa sababu tu ana ulemavu.
HITIMISHO
Hadithi ya Fatma Suleiman Mussa si hadithi ya ulemavu pekee;
ni hadithi ya moyo wa kupambana, kujiamini na kukataa kuruhusu changamoto
kuamua mwisho wa maisha. Kutoka kwenye kukata tamaa akiwa mdogo hadi kujifunza
ufumaji, kuanzisha biashara na kujitahidi kujitegemea, Fatma ameonyesha kuwa
uwezo wa mtu haupaswi kupimwa kwa hali yake ya mwili. Safari yake inatoa somo kwa jamii kwamba
fursa inapopewa mtu, inaweza kubadilisha maisha yake; lakini fursa inaponyimwa
kwa sababu ya ulemavu, jamii nzima hupoteza mchango wa mtu huyo.
Fatma anaendelea kuamini katika uwezo wake, kumtegemea Allah
na kufanya kazi kwa bidii. Ndoto yake si kujikwamua yeye mwenyewe pekee, bali
pia siku moja kuwawezesha wanawake wengine wenye ulemavu kujifunza, kujiajiri
na kujitegemea.
Comments
Post a Comment