NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
MTAALAMU wa Masuala la
Jinsia, kupitia Mradi wa ‘Pamoja’ wa kukuza usawa wa kijinsia Zanzibar, Nyezuma
Simai Issa, amesema Mradi huo, ni wa aina yake, na utapunguza wimbi la ukatili
na udhalilishaji, pindi utakapomalizika.
Mtaalamu huyo, aliyasema hayo leo Juni 11,
2026 ukumbi wa Samail Gombani Chakechake Pemba, wakati akielezea muhutasiri
ya utekelezaji wa mradi huo, kwa Kamati teule ya wilaya ya Chakechake, ya
utekelezaji wa mradi huo.
Alisema, jambo jipya ambalo limo ndani ya mradi
huo, ni ujenzi wa vituo vinane, vya makuzi na malezi ya awali ya mtoto, ambapo
kila wilaya kitajengwa kimoja.
Alisema, lengo la kituo hicho ni kuwapa nafasi
wazazi na walezi, kujiendeleza kiuchumi, wakiwa na uhakika wa malezi kwa watoto
wao.
‘’Kupitia mradi huu wa miaka mitano, jambo kubwa
ambalo limo pamoja na mingine mazuri, tutajenga vituo vinane, kwa wilaya zote
nane, zilizopotiwa na mradi huu,’’alifafanua.
Aidha Mtaalamu huyo, alisema jambo jingine
ambalo litafanyika, ni kuona kila wilaya mradi unalikarabati jengo moja,
chakavu na kwa ajili ya matumizi kama, hayo ya awali.
‘’Mradi huu, pamoja na kuanza kwa ujenzi wa
vituo hivyo vinane, lakini pia unapanga kukarabati majengo mingine machakavu kwa
wilaya zote, ili nayo yatowe huduma za makuzi na malezi ya awali ya watoto,’’alifafanua.
Hata hivyo alifafanua kuwa, ijapokuwa Mkoa wa Mjini
Magharibi, haumo kwenye mradi, lakini mradi utajenga kituo cha kitaifa cha
kutoa msaada wa kisaikolojia.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Mtaalamu wa masuala
ya kijamii, kupitia Mradi huo, Ali Wadi Makame, alisema ndani ya mradi, utawapa
mikopo wanawake, waliojikusanya kwenye vikundi vya ushirika.
Alieleza kuwa, hayo yatakuja baada ya kuwapa
mafunzo maalum, ya jinsi ya kujikwamua na umaskini na matumizi ya fedha hizo.
‘’Mradi huu, utawapa mikopo ya fedha moja kwa
moja wanawakwe walioanzisha vikundi vya ushirika na ambavy0 vimesajiliwa, ili
sasa iwe sababu ya kukuza pato lao,’’alifafanua.
Hata hivyo aliwataka wananchi wa Zanzibar, na
hasa ambao mradi huo unatekelezwa, kujenga ushirikiano na maafisa watakaopita
vijijini, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mradi huo.
Kuhusu kanuni za maadili, alisema mradi unataka
wajumbe hao kuheshimiana na kujengeana nidhamu wakati wote, wanapokua kwenye
shughuli zao.
‘’Ni jambo la kawaida kwa sisi watumishi, sasa kupitia
mradi huu zitakuwepo na kisha zitasainiwa na wajumbe wa kamati zote, ili
kulinda heshima wakati wote,’’alifafanua.
Katika hatua nyingine, alisema kwa sasa mradi
huo kwa kuanzia, unatekelezwa kwa majaribio katika wilaya za Kati kwa Unguja na
Chakechake kwa Pemba, na kisha wilaya nyingine za Kusini, Kaskazini ‘A’ na ‘B’
Mkoani, Wete na Micheweni zitafuata.
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo, walisema
mradi huo ni nzuri na umekuwa na mwelekeo wa aina ya pekee, katika kupunguza
wimbi la ukatili na udhalilishaji kwa wanawake na watoto.
Mmoja kati ya washiriki hao ambae pia ni Katibu
wa Kamati ya kupambana na udhalilishaji wilaya ya Chakechake Rashid Said
Nassor, alisema bado vitendo vya udhalilishaji vinaendelea kutokea.
Nae Salma Khamis Haji, alisema kilichobakia ni
kwa jamii, ni kutoa ushirikiano na watendaji walioteuliwa kupitia mradi huo.
Kwa sasa takwimu zilizokusanywa na Ofisi ya Mtakwimu
mkuu wa serikali Zanzibar, iliripoti matukio 1,809 ya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia, kwa mwaka 2024, ambapo waathirika walikuwa 1,809 na wengi walikuwa watoto, sawa na asilimia 84.3.
Wilaya ya Chake chake, ilishika nafasi ya nne, kwa kuripoti
matukio 113, kati ya wilaya 11 za Unguja na Pemba, huku wilaya ya Magharibi ‘B’
Unguja, ikiwa ya mwanzo kwa matukio 431.
Kwa mwaka jana, matukio hayo kwa Unguja
na Pemba, yalipungua 581, maana yalikua 1,228, kinyume na yale 1,809 ya mwaka
2024, jambo ambalo hata baadhi ya wilaya, ikiwemo ya Chake chake, yaliripotiwa
kushuka.
Wilaya iliyoongoza kwa mwaka jana ni
Magharibi ‘A’ kwa matukio 247, na wilaya ya Chake chake safari hii, ilipanda
nafsi moja, ingawa iliripoti matukio kiduchu 93, tofauti na matukio 113 ya
mwaka 2024.
Waathirika wakubwa kwa mwaka 2025, ni
watoto, waliokuwa 1,050 sawa na asilimia 85.4 kwa Unguja na Pemba, wakifuatiwa
na wanawake 162 asilimia 13.2 na wanaume 18, sawa na asilimia 1.5.
Mwisho
Comments
Post a Comment