NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANANCHI kisiwani Pemba, waetakiwa kuipiga
nambari 119, ambayo ni bure, wanapoona kuna viashiria au mtumiaji, muuzaji, msambaazaji
na muingizaji wa dawa za kulevya nchini.
Ushauri huo umetolewa leo Juni 13, 2026 na
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maryam Juma Abdalla ‘MABODI’,
wakati akizungumza na wananchi hao, uwanja wa Gombani Chakechake, kwenye
uzinduzi wa siku ya kimataifa ya kupinga dawa za kulevya.
Alisema, kwa upande wake serikali imeshaweka mikakati
kadhaa, ikiwemo kuanzisha nambari hiyo bure kwa ajili ya kupokea taarifa, za
dawa za kulevya.
Alieleza kuwa, nambari hiyo iko wazi saa 24, na wananchi
watakaoipiga watapokelewa na kupewa ushirikiano, ikiwa ni sehemu ya mapambano
dhidi ya dawa za kulevya.
‘’Tukiwa ndani ya uzinduzi wa kampeni ya kupinga matumizi,
usambaazaji, uingizaji, uuzaji wa dawa za kulevya, leo itumie nambari hiyo bure,
ili kuwaokoa vijana wetu,’’alisisitiza.
Aidha Katibu Mkuu huyo, alisema kwa sasa hali inatisha kwa
Zanzibar, ambapo mwaka 2015, kulikuwa na vijana watano (5) tu, walioanzishwa
dawa maalum za ‘methadone’, ingawa kuanzia mwaka 2016, waliongezeka
na kufikia 1,838.
‘’Tiba hii ipo na inapatikana na kutolewa na wizara ya
Afya, ili kuhakikisha vijana wanapona, waliotumia dawa za kulevya na kuamua
kuacha matumizi hayo,’’alifafanua.
Katika hatua nyingine Katibu Mkuu huyo, alisema ni dhahiri
kuwa, vijana wanaendelea kutumia dawa za kulevya, bila ya kujua kuwa wanahitajika
kulijenga taifa lao.
Mapema Kaimu Waziri, Ofisi hiyo, Hamza Hassan Juma,
alisema serikali inaelewa kuwa waingizaji, wasambaazaji na hata wanaozitengeneza
dawa za kulevya ni watu wakubwa, na wenye fedha zao.
Alieleza kuwa, hata hivyo serikali haijalala imeanzisha
mipango na mikakati endelevu, ili kupambana na wanaojiita wakubwa wa dawa za kulevya.
Alifahamisha, hakuna hata mtu mmoja, ambae ameitia serikali
mfukoni mwake, na watahakikisha wanaoingiza wanahama Zanzibar ndani ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania.
Katika hatua nyingine, Kaimu huyo Waziri ofisi ya Makamu
wa Kwanza, alimtaka Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti, na Kupambana na dawa za
Kulevya Zanzibar, asimuonea yeyote aibu, pindi wakimkuta na dawa za kulevya.
‘’Hata nikiwa mimi Waziri, au Katibu mkuu, Mwakilishi,
sheha na mwingine yeyote, mkamateni na sheria ichukua nafasi yake,’’alifafanua.
Hata hivyo alisema, wale wanaokimbilia kwa viongozi wa juu
na kupiga simu ili kupata msamaha wasahau, kwani kila kiongozi kwa sasa, hayuko
tayari na hilo.
Aliwakumbusha masheha na kamati zao, kuendelea kufuatilia
wanaouza, kutumia, kuingiza, kusambaaza dawa za kulevya, kwenye maeneo yao.
Akizungumzia mbinu za wafanyabiashara hao haramu za dawa
za kulevya, aliwatahadharisha wananchi, kuwa sasa dawa hizo, huchanganywa na
vyakula kama biskuti.
‘’Tumeshabaini kuwa, sasa dawa za kulevya huchanganywa
kwenye ubuyu, peremendi na biskuti, hivyo wananchi wawe makini na hili,’’alifafanua.
Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kupambana na Kudhibiti
dawa za kulevya Zanzibar, Kanali: Bur-han Zubier Nassor, alisema serikali
inayodhamira ya dhati, ili kuondoa kabisa dawa za kulevya.
Alieleza kuwa, moja ya athari za dawa hizo, ni kudhoofisha
afya ya mtumiaji, vifo, kuongezeka kwa uhalifu na kudumaza uchumi wa taifa.
Baadhi ya wananchi waliohudhuria, walisema bado adhabu sio
kali, kwa wanaokatwa na kutiwa hatiani kwa dawa za kulevya.
Mohamed Issa Haji wa Gombani, alisema kama wanaokamatwa na dawa hizo, wanapewa adhabu ya kunyongwa kama ilivyo mataifa mingine, jambo hilo lingekoma.
Mayasa Hassan Kassim wa Wawi, alisema bado hajaona
kupungua kwa watumiaji wa dawa za kulevya, ndani ya jamii.
Kwenye hutuba ya bajeti
ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza mwaka 2023/2024, kuliripotiwa kesi 312 na
kufanyiwa kazi, zikiwemo 25 zilizopo kwa Mkurugenzi wa Mashtaka, 31 kwa Mkemia
Mkuu, 215 zilifunguliwa mahakamani na kesi 41 ziliendelea na upelelezi.
Kesi hizo zinajumuisha
watuhumiwa 316, wakiwemo 306 wanaume na 10 wanawake kwa Unguja na Pemba, kwa
kipindi hicho pekee.
Kuhusu utoaji wa huduma
za upataji nafuu, zimeendelea kuimarishwa katika kituo cha tiba na marekebisho
ya tabia, cha Kidimni Unguja, na waraibu 186 walipokelewa, kati yao 40 waliruhusiwa
baada ya kukamilisha tiba, 35 waliondolewa, 60 wametoroka na 51 wanaendelea
kupata huduma.
Hata hivyo, ikaelezwa kuwa, kwa muda wa miaka
minne, kutoka 2020/2024, Ofisi imefanikiwa kuwamata watuhumiwa 1,220, wakiwemo wanaume
1,169 na wanawake 51, wakihusishwa na dawa za kulevya zikiwemo bangi kesi 757,
heroin kesi 463.
Ambapo kati ya hizo, 1,198
zilifunguliwa, 755 zimefikishwa mahakamani, na wakifanikiwa kuteketeza vielelezo
vya dawa za kulevya, vyenye uzito wa kilogramu 1,619.86 kwa kipindi hicho.
Kubwa zaidi,
wamefanikiwa kukamilisha ujenzi wa kituo cha tiba na marekebisho ya tabia kwa
waraibu wa dawa za kulevya, kilichopo Kidimni Unguja.
Ambapo kauli mbiu ya mwaka huu, inaeleza kuwa, ‘ushahidi
uko wazi, ekeza katika kinga’
Mwisho
Comments
Post a Comment