KAMATI YA KUPAMBANA NA UDHALILISHAJI CHAKECHAKE YAWAJIA JUU WAZAZI WANAOWARUHUSU WATOTO KUTEMBEZA BIASHARA
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
KAMATI ya kupambana na udhalilishaji
kwa wanawake na watoto ya wilaya ya Chake chake, imepiga marufuku kwa wazazi na
walezi wilayani humo, kuwapa biashara za kutembeza watoto wao, kwani ni njia moja
wapo ya kufanyiwa vitendo viovu.
Kauli hiyo imetolewa leo Mei 25, 2026 na Kaimu
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Kassim Ali Omar, wakati akifungua kikao kazi, cha
wajumbe hao, kilichofanyika ukumbi wa zamani wa TASAF Chake chake.
Alisema lazima kamati, isimamie hilo maana wapo wazazi
wamekuwa wakiwatumia watoto wao, kutembeza biashara mitaani, na kisha huishia
kudhalilishwa.
Alieleza kuwa, hasa kuelekea kipindi hichi cha sikukuu na
skuli kufungwa, wazazi hutumia fursa hiyo, jambo ambalo sio sahihi.
‘’Niitake sana kamati hii, ihakikishe inasimamia sana,
maana wapo wazazi na walezi, wamekuwa wakiwatumia watoto wao, kutembeza
biashara majumbani, jambo ambalo ni hatari kwao,’’alifafanua.
‘’Sijajua kuwa, kuongezeka kwa matendo hayo ni jamii kupata
elimu, au vitendo vimezidi, hili ni jukumu la kamati, kuendelea kutoa elimu,’’alifafanua.
Aidha, aliwapongeza wajumbe wa kamati hiyo, kwa kazi wanayoifanya
ya kutoa elimu, katika maeneo kadhaa ya wilaya ya Chake chake.
Mapema Katibu wa kamati hiyo Rashid Said Nassor, alisema vyombo
vya habari, vimekuwa na mchango mkubwa, katika mapambano dhidi ya udhalilishaji.
‘’Na sisi kamati ya wilaya, tuliwafikia wananchi wa shehia
hizo, na tulifanya vikao na jamii, ambavyo vililenga kupambana na
udhalilishaji,’’alifafanua.
Mapema Moza Massoud Amour, kutoka wizara ya Kazi na Uwezeshaji,
alisema hivi karibuni, waliwarejesha skuli wanafunzi 13, kati ya 62 waliowagunda
wameacha masomo katika skuli mbalimbali.
Alisema, bado jamii inahitaji elimu kwa upana zaidi, kujua
viashiria ya vitendo vya udhalilishaji, kwa wanawake na watoto wilayani humo.
Akighairisha kikao hicho kazi, Kaimu Mwenyekiti huyo
Kassim Ali Omar, aliwasisitiza wajumbe hao, kuifikisha elimu waliyoipita, kwa
jamii.
Mwisho








Comments
Post a Comment