NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
KIONGOZI wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa
Ismail Ali Ussi amesema, ameridhishwa kwa asilimia 100, na utekelezwaji wa
mradi wa upandaji wa migomba uliotekelezwa na kikundi cha ‘tusitupane
Cooparative’ kilichopo shehia ya Kukuu wilaya ya Mkoani Pemba.
Alisema, mradi huo ni miongoni mwa jitihada za serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar, za kuunga mkono wananchi wake, katika kuhakikisha wanatumia
fursa za kiuchumi zinazowazunguka katika maeneo yao.
Aliyasema hayo jana, wakati alipotembelea shamba la
migomba la kikundi hicho, shehiani humo, ikiwa ni shamra shamra za mwenge huo,
kwa mwaka huu.
Alieleza kua, mradi huo ni utekelezaji wa ahadi
alizoziweka Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi baada ya kuingia
madarakani, za kuwawezesha wananchi kuzitumia fursa za kiuchumi zilizopo nchini.
Alifafanua kua, kilimo hicho kinaonyesha dhahiri kwamba,
vijana wa kikundi hicho wamefanya jitihada nzuri, katika kutimiza azma na maono
ya Dk. Mwinyi.
"Vijana wa kikundi hichi, wamefanya jitihada kubwa
katika kutimiza azma ya serikali, kwani wameonesha wazi mafanikio ya jihudi zinazofanywa
na serikali, za kuwawezesha wananchi wake katika kutumia fursa za kiuchumi,"
alisema.
Alieleza kwamba, kikundi hicho kimefanya kazi kubwa
ambayo, ni hatua muhimu katika kujikwamua kimaisha na kujiimarisha kiuchumi,
kutokana na mchango wa kilimo kuwa mkubwa.
Aidha kiongozi huyo wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa
Ismail Ali Ussi, alitoa wito kwa wananchi kushiriki uchaguzi mkuu, kwa amani na
utulivu, huku akiwataka kuwaunga mkono viongozi
waliopo madarakani.
"Kama ilivyo kaulimbiu ya mwenge wa uhuru mwaka huu
ya "jitokeze kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu"
naombeni Oktoba tuwaunge mkono viongozi wetu waliopo,"alisisitiza.
Awali akisoma risala ya kikundi, Katibu wa kikundi hicho
Habibu Ali alisema, kikundi hicho kilianzishwa 2019 na kupata usajili mwaka 2023,
kina wanachama 24, wanaume 16 na wanawake wanane, hadi sasa kimepokea mkopo wa shilingi
milioni 5, kutoka serikalini na shilingi milioni 10 kutoka kwa taasisi ya
Uwezeshaji wananchi Kiuchumi (ZEEA).
Alieleza kua, hadi sasa kikundi kimeshapanda migomba 380 ya
aina tofauti, ambapo kati ya hiyo 145, imeshaanza kuzaa na kuvuna ndizi 46,
ambapo zimeuzwa na kujipatia shilingi 490,000.
Aliongeza kua, shamba lao lenye ekari 1.25, limefanikiwa
kutoa ajira kwa vijana, limesaidia kuongeza lishe na uhakika, uhifadhi wa
mazingira na matumizi bora ya ardhi kwa kutumia mbolea za samadi.
Katika ukaguzi wa mradi huo, kiongozi wa mbio za mwenge
kitaifa, alishiriki katika zoezi la upandaji wa migomba shambani hapo.
Wakati huo huo, kiongozi huyo wa mbio za mwenge wa uhuru
kitaifa, alitembelea mradi wa lishe bora, ambapo alifungua klabu ya uhamasishaji wa lishe bora
kwa afya imara, iliopo skuli ya msingi Kukuu.
Katika ufunguzi huo alisema, klabu hiyo itasaidia kutoa
elimu ya matumizi ya lishe bora kwa jamii, ambapo kauli mbiu yake ni "mtaji
ni afya yako zingatia unachokula".
Wilaya ya Mkoani mwenge huo na ujumbe wake, ulitembelea
jengo la kuhifadhia mwani Mtuhaliwa, diko na soko la samaki Mbuyuni, uwekaji wa
sanduku la maoni bandarini na ujenzi wa dakhalia Kiwani na kufanyika mkesha
eneo la Tasini jimbo la Kiwani.
MWISHO
Comments
Post a Comment