NA MWANDISHI WETU, PEMBA
MKUU wa wilaya ya Mkoani Dk.
Hamad Omar Bakari, ameuhakikishia, uongozi wa mbio za mwenge kitaifa wa mwaka
2025, kwamba watayafanyia kazi maagizo, maelekezo na ushauri waliutoa, hasa suala
la kutunza amani na utulivu, kuelekea uchaguzi mkuu.
Mkuu huyo wa wilaya aliysema
hayo jana, eneo la skuli ya Ngwachani wilayani humo, kwenye hafla ya kumkabidhi
mwenge huo, mwenzake wa wilaya ya Chake chake Mgeni Khatib Yahya.
Alisema ujumbe wa mwenge
kiujumla, umekuja kuwazindua wananchi wa wilaya yake, juu ya umuhimu wa kutunza
amani, kwa maslahi mapana ya taifa na watu wake.
Alieleza kuwa, wakati mwenge
huo unakimbizwa wilayani mwake na kukutana na wananchi, ulisisitiza utunzaji wa
amani, na hasa kuelekea mwezi Oktoba mwaka huu, kwenye uchaguzi mkuu wa vyama
vingi.
Dk. Hamad alifahamisha kuwa,
jingine ambalo mwenge huo wa uhuru chini ya kiongozi wake Ismail Ali Ussi,
ulisisitiza, ni kupiga vita dawa za kulevya nchini.
‘’Na hili suala la kupiga vita
dawa za kulevya, na sisi wilayani tunaliunga mkono, maana vijana wamekuwa
wakiathirika siku hadi siku na kupoteza nguvu kazi ya taifa letu,’’alifafanua.
Katika hatua nyingine, Mkuu
huyo wa wilaya ya Mkoani, aliwapongeza wakimbizwa hao, kwa umoja na mshikamano
waliouonesha, katika kipindi chote ndani ya wilaya hiyo.
Akimkabidhi mkuu wa wilaya ya
Chake chake mwenge huo na wakimbiza mwenge wake, alimtaka kuutunza, kuenzi, ili
nae kuukabidhi wilaya nyingine ukiwa salama.
Akisoma taarifa ya mwenge huo
kwa wilaya ya Mkoani, Katib tawala wa wilaya hiyo, Miza Hassan Faki, alisema
miradi sita ilitembelewa na mwenge huo, yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni
15.8.
Alieleza kuwa, awali
walifanikiwa kukusanya michango yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 52.1,
ambapo kati ya fedha hizo, shilingi milioni 13.5 zilitumika kwa usafiri na
shilingi milioni 23 kwa ajili ya kuchangia miradi ya mwenge.
Mapema, kiongozi wa mbio za
mwenge wa uhuru kitaifa kwa mwaka 2025, Ismail Ali Ussi, aliwakumbusha wananchi
wa wilaya Mkoani, kuwachagua viongozi wenye hamu ya maendeleo.
‘’Naelewa kuwa, mwishoni mwa
mwaka huu, Tanzania itaingia kwenye uchaguzi mkuu wa vyama vingi, niwaombe
mkawachague viongozi, wanaowajali,’’alisema.
Aidha, kiongozi huyo wa mbio
za mwenge, alisifu usihirikiano aliouona kwa watendaji wa wilaya ya Mkoani, jambo
lililompa faraja.
Mara baada ya kuupokea mwenge
huo, Mkuu wa wilaya ya Chake chake Mgeni Khatib Yahya, aliwahakikisha watembeza
mwenge hao, kuwa watakuwa salama na afya njema.
Alieleza kuwa, wilaya imeshajipanga
kuutembeza mwenge huo kwa umbali wa kilomita 53.5, katika miradi minne, yenye
thamani ya zaidi ya shilingi biloni 19.
Baadhi ya wananchi wa wilaya
ya Chake chake, waliahidi kuunga mkono mwenge huo, ili kuhakikisha unafungua miradi
na kuiwekea mawe ya msingi iliyokusudiwa.
Khadija Omar Hassan wa
Madungu na mwenzake Aisha Hassan Kassim wa Chanjaani, walisema ujio wa chombo
hicho, ni kuwaunganisha watanzania kuwa kitu kimoja.
‘’Mwenge hauna chama wala
dini, na haipendezi kuutenga, maana lengo lake ni kuchochea maendeleo kwa
wananchi wote,’’walifafanua.
Mwenge huo wa uhuru ukiwa
wilaya ya Chake chake, utayatembelea miradi minne, ukiwemo ujenzi wa hospital
Chonga, mradi wa vijana Wesha, hospital ya huduma za wazazi Gombani na kufanyika
mkesha wake Madungu, ambapo asubuhi utaaelekea mko wa kaskazini Pemba.
Mwisho
Comments
Post a Comment