Skip to main content

KIDUTANI CHUMBAGENI PEMBA WAPITISHA KANUNI ZA KUWALINDA

 


 

NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WANANCHI wa kijiji cha Kidutani shehia ya Chumbageni wilaya ya Mkoani Pemba, wamepitisha kwa pamoja, kanuni zitakazowaongoza wao na watoto wao, katika kufikia malezi na makuzi mema ya vijana wao.

Akizisoma kanuni hizo mbele ya mkutano mkuu wa wanakijiji hao, Katibu wa kamati ya maadili, taaluma na ushari Machano Ali Makame, alisema moja ya kanuni hizo kati ya 19, walikubaliana kuwa, mwisho wa kutembea iwe ni saa 4:00 usiku.

Alisema kanuni hiyo, itawahusu watu wote, na ikitokezea kuna kundi la watu au mtu mmoja ana dharura mfano ugonjwa, wavuvi, wafanyakazi wataieleza kamati hiyo.

‘’Inawezekana ukamkamata mtu saa 5:00 usiku, lakini kama ukitoa maelezo yenye ushahidi mbele ya kamati, unaweza kusameheka, maana lengo sio kukomoana,’’alisema.

Katib huyo alisema kanuni nyingine ambayo wanakikiji hao wamekubaliana ni, kupiga marfuku mikato ya nywele inayopongina na uislamu pamoja na nguo za mbano.

Alifafanua kuwa, kanuni nyingine ambayo wanaamini wakiifuata inaweza kuwa suluhisho la kwa vijana wao, ni kuwarejesha masomo waliokatisha.

‘’Wapo baadhi ya vijana wamekatisha masomo, iwe ni madrassa au skuli, wapo wasiotaka kufanya ibada wote hawa wataitwa na kamati na kufanya mazungumzo nao,’’alisema.

Katib huyo alisema kanuni nyingine walioipitisha ni kuwapa fursa vijana, kuangalia nyenendo za wazazi, na pindi akitokezea mmoja wao, anatabia hatarishi, wafikishe taarifa zake mbele ya kamati.

Mapema Mwenyekiti wa kamati hiyo, Saleh Abdalla Mohamed, alisema kanuni hizo na nyingine, anaona zitakuwa msaada mkubwa kwa jamii ya Kidutani.

Alieleza kuwa, ijapokuwa zipo kanuni zilizomo ndani ya kitabu kitakatifu pamoja na hadithi za Bwana Mtume Muhammad (S.A.W), lakini walizozipitisha hazipingani na amri hizo.

‘’Kwa mfano tunafuatilia nyenendo za watoto masomoni, uvaaji wa nguo za stara, kupiga marufuku ngoma, ukataji wa nywele na kuacha wizi, yote haya yamepitishwa kama kanuni, ingawa hata uislamu umekataza mwanzo,’’alifafanua.

Msaidizi Katibu wa kamati hiyo Mariyama Mussa Khamis, alisema kamati inatarajia kuanzisha madarasa kadhaa, kwa ajili ya wananchi kujiendeleza.



Nae mwananchi Khamis Khatib Khamis, alishauri kuwa kamati iwe madhubuti, katika kusimamia kanuni hizo, ili kuwa na vijana wenye maadili mema.

Kwa upande wake mwananchi Time Pandu Makame, aliwasisitiza wazazi na walezi wenzake, kuwa karibu na kamati hiyo, ili kufikia malengo husika.

Wananchi wa kijiji cha Kidutani, walifikia uamuzi wa kuwa na kamati hiyo ya maadili, baada ya kuoenekana kujitokeza kwa vitendo viuvu ikiwemo wizi hasa nyakati za usiku pamoja na kundi la watoto kukatisha masomo.

Wakati hayo yakifanyika, wizara ya Maendelezo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, kwa mwaka wa fedha 2025/2026, imepanga kutumia shilingi milioni 5,737,003,000, ili kuendesha programu mbali mbali, ikiwemo ya kuratibu utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Kitaifa wa Kumaliza Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji kwa wanawake na watoto.

Jingine lililokusudiwa kufanywa na wizara hiyo ni Mradi wa Mapambano dhidi ya Vitendo vya Ukatili wa Kijinsia kwa Wanawake na Wasichana.

                 Mwisho

Comments