NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANANCHI wa kijiji cha Kidutani
shehia ya Chumbageni wilaya ya Mkoani Pemba, wamepitisha kwa pamoja, kanuni
zitakazowaongoza wao na watoto wao, katika kufikia malezi na makuzi mema ya vijana
wao.
Akizisoma kanuni hizo mbele ya mkutano mkuu wa wanakijiji
hao, Katibu wa kamati ya maadili, taaluma na ushari Machano Ali Makame, alisema
moja ya kanuni hizo kati ya 19, walikubaliana kuwa, mwisho wa kutembea iwe ni saa
4:00 usiku.
Alisema kanuni hiyo, itawahusu watu wote, na ikitokezea
kuna kundi la watu au mtu mmoja ana dharura mfano ugonjwa, wavuvi, wafanyakazi
wataieleza kamati hiyo.
‘’Inawezekana ukamkamata mtu saa 5:00 usiku, lakini kama
ukitoa maelezo yenye ushahidi mbele ya kamati, unaweza kusameheka, maana lengo
sio kukomoana,’’alisema.
Katib huyo alisema kanuni nyingine ambayo wanakikiji hao
wamekubaliana ni, kupiga marfuku mikato ya nywele inayopongina na uislamu
pamoja na nguo za mbano.
Alifafanua kuwa, kanuni nyingine ambayo wanaamini wakiifuata
inaweza kuwa suluhisho la kwa vijana wao, ni kuwarejesha masomo waliokatisha.
‘’Wapo baadhi ya vijana wamekatisha masomo, iwe ni madrassa
au skuli, wapo wasiotaka kufanya ibada wote hawa wataitwa na kamati na kufanya
mazungumzo nao,’’alisema.
Katib huyo alisema kanuni nyingine walioipitisha ni kuwapa
fursa vijana, kuangalia nyenendo za wazazi, na pindi akitokezea mmoja wao,
anatabia hatarishi, wafikishe taarifa zake mbele ya kamati.
Mapema Mwenyekiti wa kamati hiyo, Saleh Abdalla Mohamed,
alisema kanuni hizo na nyingine, anaona zitakuwa msaada mkubwa kwa jamii ya
Kidutani.
Alieleza kuwa, ijapokuwa zipo kanuni zilizomo ndani ya
kitabu kitakatifu pamoja na hadithi za Bwana Mtume Muhammad (S.A.W), lakini
walizozipitisha hazipingani na amri hizo.
‘’Kwa mfano tunafuatilia nyenendo za watoto masomoni, uvaaji
wa nguo za stara, kupiga marufuku ngoma, ukataji wa nywele na kuacha wizi, yote
haya yamepitishwa kama kanuni, ingawa hata uislamu umekataza mwanzo,’’alifafanua.
Nae mwananchi Khamis Khatib Khamis, alishauri kuwa kamati
iwe madhubuti, katika kusimamia kanuni hizo, ili kuwa na vijana wenye maadili
mema.
Kwa upande wake mwananchi Time Pandu Makame, aliwasisitiza
wazazi na walezi wenzake, kuwa karibu na kamati hiyo, ili kufikia malengo husika.
Wananchi wa kijiji cha Kidutani, walifikia uamuzi wa kuwa
na kamati hiyo ya maadili, baada ya kuoenekana kujitokeza kwa vitendo viuvu ikiwemo
wizi hasa nyakati za usiku pamoja na kundi la watoto kukatisha masomo.
Wakati hayo yakifanyika, wizara ya Maendelezo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto, kwa mwaka wa fedha 2025/2026, imepanga kutumia
shilingi milioni 5,737,003,000, ili kuendesha programu mbali mbali, ikiwemo ya
kuratibu utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Kitaifa wa Kumaliza Vitendo vya
Ukatili na Udhalilishaji kwa wanawake na watoto.
Jingine lililokusudiwa kufanywa na wizara hiyo ni Mradi wa
Mapambano dhidi ya Vitendo vya Ukatili wa Kijinsia kwa Wanawake na Wasichana.
Mwisho
Comments
Post a Comment