NA FATMA HAMAD, PEMBA@@@@
MJANE mwenye watoto saba amewaomba wahisani na
watu wenye uwezo, kumpa msaada wa bati na miti, kwa ajili ya kuezekea nyumba
yake, ili apate kustirika na watoto wake.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi
nyumbani kwake kijiji cha Madenjani Wilaya ya Wete Pemba, leo Juni 12, 2025 mama huyo Rehema Salum, alisema nyumba anayokaa imeshakua mbovu, mvua yote inamnyeshea ndani
mwake.
Alisema anapatashida kwani mvua inaponyesha
husimama barazani hata kama ni usiku mkubwa,kwa vile ndani hujaa maji na kukosa
sehemu salama.
‘’Ndani hujaa maji, vitanda vyangu vyote
vimeshaharibika sina hata pakulala na watoto wangu saba, naomba binadamu
wezangu munisaidie nateseka,’’alilalamika.
Alieleza tayari alishajenga vyumba viwili vya
matufali, ingawa ameshindwa kuezeka, hivyo ameomba asaidiwe bati pamoja na miti
kwa ajili ya kuezekea, ili apate kuishi sehemu anapostahiki binadamu.
Alifahamisha kuwa mume wake amemuacha na
watoto saba, na kumuachia mzigo wa malezi, na kwa sasa hamuulizi huduma ya aina
yoyote kwa watoto wao.
Alisema amesharipoti maeneo mbalimbali ikiwemo
ustawi wa jamii wilaya ya Wete pamoja wizara ya Maendeleo ya Jamii, ingawa
hakuna hatua aliyochukuliwa.
Katika hatua nyingine, alimuomba sheha wa shehia kumuingiza katika miradi ya maendelo ambayo
inakuja, ili iweze kuwasaidia kumoa uhakika wa chakula.
Mtoto wa mjane huyo, Bilali Mohamed Rashid (16) anaesoma darasa la kumi, anasema ndoto zake
za baadae ni kuwa waziri wa Fedha.
Alifahamisha kuwa, kitendo cha kukosa huduma
kutoka kwa baba yao kinamuathiri, kwani wanashindwa kupata huduma wanazotakiwa,
kutoka kwa wazazi wao, ndio maana anasoma kwa bidii.
‘’Tunakwenda skuli hatuna viatu mvua kama
hizi, hatuli chochote, na tukirudi tunakuta hamna kitu, kwakweli hilo
linaniathiri na linaweza kupelekea kushindwa kutimiza ndoto zangu,’’alifafanua.
Nae Nasra Mohamed Rashid ambae anasoma darasa
la pili amesema ipo haja serikali,
kuweka adhabu kali kwa wazazi pindi wakizitekeleza familia zao.
Baba mzazi huyo ambae ni mstaafu wa JWTZ,
Mohamed Rashid alipopigiwa simu na mwandishi wa habari alisema, sio kwasababu
hataki kuwahudumia watoto wake, bali ni kutokana na halingumu ya maisha yake.
‘’Ni kweli mstaafu, ingawa ninachokipata,
hakitoshelizi kukigawa nyumba mbili, inafaa kama hawa watoto atanirejeshea
nipate kuwahudumia kwa chungu kimoja,’’alisema.
Mwana harakati wa kulinda na kutetea haki za
watoto Pemba Tatu Abdalla Msellem alisema kuvunjika kwa ndoa isiwe sababu ya
kila mzazi kufumbia macho wajibu wake wa malezi na huduma kwa watoto.
Sheikh Said Ahmed
Mohamed kutoka Ofisi ya Mufti Pemba, anasema kisheria mwanamme ndie mwenye jukumu la kutoa matunzo kwa familia yake, hata baada ya kuvunjika kwa ndoa.
Kiongozi wa Kanisa Katoliki lililopo Mkungu Malofa Chakechake Robert
Miguwa Ndalami, anasema dini
imeelekeza wanaume watoe huduma stahiki kwa familia zao akiwemo mama na watoto.
Ripoti ya Wizara ya Kazi, Uezeshaji, Wazee na
Watoto, kwa sasa wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto ya mwaka
2017/2018, imeeleza kua, kesi 534 za
utelekezaji watoto zimeripotiwa Zanzibar.
Ambapo kesi 412 ni kwa upande wa Unguja na 122
kwa Upande wa Pemba, hata hivyo ripoti hiyo haijaweka wazi sababu rasmi za utelekezaji huo.
MWISHO.
Comments
Post a Comment