NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANAKIKUNDI cha ufugaji wa majongoo bahari, ‘tumuombe mola’ cha
Makangaale wilaya ya Micheweni Pemba, wanatarajia kujipatia shilingi milioni 20
mwishoni mwa mwaka huu, ikiwa watafanikiwa kuuza bidhaa hiyo, baada ya kuekeza
vifaranga vyenye thamani ya shilingi million 1.6 mwaka jana.
Fedha hizo, ni
uwekezaji wa vifaranga 3,300 vya majongoo habari, walivyovinunua kwa shilingi 1,650,000
wastani wa shilingi 500 kila kifaranga kimoja, chenye urefu kati ya nchi nne
hadi tano.
Wanakikundi hao
cha ‘tumuombe mola’ wamesema kati ya vifaranga hivyo,
wanatarajia kuvuna majongoo yaliokwisha pevuka 2,500 na kisha kila moja kuliuza
kwa bei ya shilingi 8,000 na kujipatia shilingi milioni 20.
Mwenyekiti wa
kikundi hicho Hator Hassan, alisema haiwezekani kuotesha vifaranga vya idadi 3,300
kisha kuvuna kama ilivyo.
‘’Zipo changamoto
kama za kufa na hasa wakati wa usafirishaji wa vifaranga kutoka eneo moja
kwenda kwenye bwawa lao, wizi na wingine kufa kabla ya kufikia kupevuka,’’alifafanua.
Aliongeza kuwa,
ingawa hawakula hasara, kama inavyoonekana, lakini hawakuvuuka lengo lao la
kujipatia fedha zaidi shilingi milioni 5.
‘’Kama sio
changamoto ya vifaranga kufa au kuibiwa wakiwa ndani ya bwawa letu, hata ule
mwaka 2021 wakati tunaanza, tungejipatia faida ya shilingi milioni 4,’’alifafanua.
Aidha Mwenyekti
huyo, aliongeza kuwa, hata mwaka 2023, walitarajia kujipatia faida ya shilingi
milioni 9, ingawa hatimae, walipata shilingi milioni 1.5.
Aliongeza kuwa, tayari wameshafuga mara mbili, tokea waanze kazi hiyo
mwaka 2021, na kutumia gharama ya shilingi milioni 3.1 kwa ununuzi wa vifaranga
4,000.
Hata hivyo, alisema kwa sasa wanasubiria hadi mwishoni mwa mwaka huu,
na ikiwa vifaranga walivyovitia ndani ya bwawa hilo, havitapitia changamoto ya
wizi na kufa, hawana wasiwasi wa kuvuna shilingi milioni 20.
Mmoja wa wanachama hao Hamad Omar Hamad, alisema wamekua wakibadilisha
maisha yao, kupitia kazi hiyo, ikiwemo kujihakikisha fedha za matumizi.
‘’Ni kweli kabla ya kuanza kazi hii ya ufugaji wa majongoo bahari,
sikuwa na uhakika wa wapi naweza kujipatia fedha za haraka, ingawa kwa sasa nnapo,’’alisema.
Hata hivyo, waliwaomba wafadhili kadhaa, kuzitatua changamoto zao,
ikiwemo kuwapatia boti dogo kwa ajili ya doria, viatu vya kuvulia, ili kuepusha
hasara za miguuni.
Afisa Ustawi wa mkoa wa kaskazini Pemba Nassra Massoud Sanani, alikiri
kukifahamu kikundi hicho, na kusema amekuwa akiwaunganisha na wadau mbali mbali
wakiwemo FAWE-Zanzibar.
Alisema, FAWE wamekuwa wakifanyakazi na taasisi kadhaa za kimataifa kama
vile UN-Women na wameshaanza kuwapatia mafunzo kadhaa.
Afisa miradi FAWE -ofisi ya Pemba Hija Hamad Issa, alisema hivi
karibuni, walikuwa na mafunzo ya siku nne ya mnyororo wa biashara, ambapo
mwakilishi wa kikundi hicho, alikuwa miongoni mwao.
‘’FAWE unao mradi wa pamoja, ambao unawaangalia wajasiriamali wanaojishughulisha
na kilimo cha mwani, majongoo bahari, migomba, ndizi na mihogo ili kuwa
wabunifu,’’alifafafanua.
Alisema, wamekuwa wakifanyakazi kwa karibu na UN-Women katika mradi huo, ambao wapo wajasiriamali 20 wa wilaya za Wete na Micheweni wameshanufaika.
Mapema Mwakilishi wa shirika la kimataifa la UN-Women Tanzania Emile
Kivugo Mwakafundu, alifafanua mradi huo, unawalenga wajasiriamali wa mazao ya
baharini na nchi kavu.
Alisema, mradi huo wa miaka mitatu, utamalizika mwakani, ambao lengo
ni kuona wajasiriamali hao, wanaziongezea thamani bidhaa zao.
Alieleza kuwa, kupitia wadau wao wa FAWE- Zanzibar wanawafundisha
namna ya kutoziuza bidhaa zao, kama walivyozivuna na badala yake, waweza kuzisarifu
ili wauze kwa mfumo wa bidhaa.
Kwa mwaka wa fedha 2024/2025 wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi
Zanzibar, katika
kuimarisha ufugaji wa majongoo bahari na upatikanaji wa vifaranga, Idara kwa
kushirikiana na Kampuni ya Zanzibar Marine Hatchery imezalisha vifaranga milioni
1.5.
Ambapo kati ya hivyo vifaranga 80,000 vimegawiwa kwa wafugaji wa Unguja
na Pemba na vyingine 70,000 kwa ajili ya biashara na uzalishaji.
Mwisho
Comments
Post a Comment