KUCHELEWA KUHAMIA KWA WAJASIRIAMALI KITUO CHA MICHAKAINI, MANISPAA CHAKE CHAKE ILIKOSA 'BUNDA' LA MAPATO
MWENYEWE Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi kwenye hutuba
yake ya ufunguzi wa Kituo cha wajasiriamali Chake chake, alielezea kufarajika.
Mbele ya
umati wa wajasiriamali na wananchi wa mkoa wa kusini Pemba, ameelezea kuwa,
sasa atapa usingizi baada ya kumalizika kwa kituo hicho.
‘’Leo nimefarajika
kuona sasa kituo hichi kipya na cha kisasa, nakifungua rasmi, sasa wajasiriamali
wa mji wa Chake chake, waliokuwa wakihangaika huku na kule wamepata utulivu,’’akasisitiza.
Eneo jingine
Dk. Mwinyi wakati wa hafla ya uzinduzi wa
kituo hicho, mwezi Oktoba 2023, akatoa rai kama sio maagizo kwa Baraza la Manispaa
Chake chake.
Moja,
akaanza kusisitiza kwa watendaji, kuhakikisha usafi unafanyika kwa udhati, ili
wananchi watakaofika hapo, wasishuhudie uchafu kuzagaa.
‘’Haiwezekani
hata kidogo, kuwa wapo wingine wameweka bidhaa zo nje, hapo ni dhahiri wale
waliomo ndani watakosa wateja,’’alifafanua.
Kwenye
hafla hiyo ya ufunguzi wa kituo hicho, Dk. Mwinyi ambae sio muumini wa kodi
kubwa, akasema ni lazima miezi mitatu ya mwanzo, wajasiriamali wasilipe kodi.
‘’Ingawa
niwaombe wenzetu wa Baraza la Manispaa Chake chake, kuwatoza fedha ndogo kwa ajili
ya usafi, kwani ndio kwanza wanaanza sasa biashara,’’anasema.
Kwa
kule kuona kwake mbali, alisema kwa wakati huo, ilikuwa ni kuwavutia wajasiriamali
hao, kuhama katikati ya mji na kuingia ndani ya kituo hicho.
Akitaja
kuwa, hapo baadae Baraza la Manispaa litakwenda kutunisha mfuko wake wa mapato,
kupitia vikuta na fremu za milango zilizomo.
Maana alisisitiza
kuwa, ujenzi wa vituo hivyo vya wajasiriamali vya Unguja na Pemba, vipo kwa
ajili ya kuwawekea mazingira mazuri, wajasiriamali.
‘’Kama
mlivyosikia kuwa, ujenzi wa Kituo cha wajasiriamali hichi cha Michakaini, fedha
nyingi zimetumika, sasa lazima wajasiriamali wahamie, ili wafanye kazi zao kwa
ufanisi,’’alisisitiza.
Kwa wakati
huo, alitumia nafasi hiyo kuwahakikishia, wajasiriamali wote wa Unguja na Pemba,
kila anayeomba mkopo, atapatiwa na serikali.
‘’Huku
tunaendelea kutoa mikopo, na wakati huo huo tunawaondoa wajasiriamali
kufanyabiashara zao, pembezoni mwa barabara,’’anasisitiza.
Na ndio
maana, baadhi ya wajasriamali wakasema kituo hicho cha kisasa, ni msaada mkubwa
kwao, kwa ajili ya kupata utulivu wa biashara zao.
HALI HALISI BAADA YA MIAKA MIWILI YA UFUNGUZI
Ilitarajiwa
mno, kuwa shilingi milioni 107,190,000 zikusanywe na Baraza la Manispaa Chake chake
Pemba, kuanzia mwezi Novemba, 2023 hadi Januari mwaka huu, baada ya ufunguzi wa
kituo hicho.
Ingawa,
imebainika kuwa hazikupatikana, baada ya wajasiriamali kugoma kukitumia kituo chao
cha Michakaini Chake chake Pemba kwa wakati, uliokusudiwa.
Maana kituo hicho kipya kilichojengwa kwa ajili yao,
kina milango 63 ya maduka, ambapo kila mmoja Baraza lilikusudia kuukodisha kwa
shilingi 50,000.
Hapo, Baraza hilo lilikusudia, kujipa wastani wa
shilingi milioni 3,150,000 kwa kila mwezi mmoja, na hasa kuanzia mwezi Novemba
mwaka 2023.
Ingawa imebainika, baada ya wajasiriamali hao kukataa
kuingia kituoni humo, Baraza hilo, kuanzia mwezi Novemba, 2023 hadi Januari mwaka
huu, limeshapoteza shilingi milioni 85,050,000.
Aidha mapato ya shilingi ya milioni 22,140,000 nayo hayakukusanywa
na Baraza hilo kwa kipindi hicho, yaliokuwa yatokane na vizimba ‘vikuta’
82.
Ambapo kwa mujibu taarifa za uongozi wa Baraza hilo, kila
kimoja, kilitarajiwa kukukodishwa kwa shilingi 10,000 kwa wajasiriamali.
Ikafahamika kuwa, vikuta hivyo kama vyengepata wajasiriamali,
kwa mwezi mmoja Baraza lingekusanya shilingi 820,000, sawa na jumla shilingi
milioni 3,970,000 ijumuisha na kodi ya milango 63.
Ndani
ya kituo hicho kilichofunguliwa mwezi Novemba mwaka 2023, Baraza la Manispaa
lilitarajia wajasiriamali wa nguo za mtumba na wauza viatu, wakitumie na kuanza
kulipia vikuta 82 na milango 63.
Na ndio
maana baada ya wajasiriamali hao wa mji wa Chake chake kugoma kikutimia kituo
hicho, walilisababishia Baraza la Manispaa hilo, kupoteza mapato ya zaidi ya shilingi
milioni 107.190 kwa fremu 63 za milango na vizimba 82 kukosa wateja.
Uchunguzi
ulibaibi kuwa, baada ya kufunguliwa kwa kituo hicho mwezi Oktoba mwaka 2023,
mwezi uliofuata Baraza hilo la Manispaa, lilianza kuwahamisha wajasirimali,
hasa wauza mitumba na viatu, kuhamia kituoni hapo.
Kwa wakati
huo Askari na uongozi mzima wa Baraza la Manispaa, ulihamia ndani ya mji wa
Chake chake, ili kuwasaka wajasiriamali, wanaopanga bidhaa zao chini na
kuwaomba kuingia kituoni hapo, bila ya mafanikio.
Msaidizi
Ofisa Mapato wa Baraza hilo, Said Mabrouk Juma, alikiri kuwa, kulikuwa na ugumu
kwa wajasiriamali wa nguo za mtumba, viatu na urembo kukitumi kituo hicho.
‘’Pamoja na kuwatumia
hata askari wa jiji na wakati mwingine na Mkurugenzi kuwapitia, lakini walikataa
na sisi kuendelea kupoteza mapato,’’anafafanua.
Ikafahamika
kuwa, baada ya kugoma kuingia kituoni hapo, waliwaomba kwa mara nyingine, kwa
sharti la kuwaondolea kodi, na kuwaomba kuchangia fedha ya umeme tu shilingi
20,000 na kukubali.
‘’Wapo
waliokubali kuingia kituoni hapo, ingawa walituomba na kukubaliana nao, kwamba
wasitozwe kodi na badala yake, wachangie huduma ya umeme, na hadi sasa hilo linaendelea,’’anaeleza.
Mkurugenzi
wa Baraza hilo Shida Kombo Mohamed, akabainisha kuwa, kuanzia mwezi Januari
mwaka 2025, rasmi walipokubaliana na wajasiriamali hao, kuchangia gharama za
umeme, kituoni hapo.
‘’Ni
kweli wakati wanahamia kituoni hapo, hata biashara ilikuwa ngumu kwa kukosa
wateja, na ndio maana tuliwaomba kuchangia huduma umeme, kwa shilingi 20,000 kwa
mwezi,’’anasema.
Wenyewe
sasa, wanampango kuanzia mwezi Machi mwaka huu, kila mlango mmoja, kuuwekea
mita yake ya umeme, ili kuondoa changamoto ya matumizi, kama yaliyopo sasa.
‘’Kwa
sasa mchango wa umeme uko sawa kwa kila mjasiriamali, ingawa baada ya kushauriwa
kuhusu kila mmoja awe na yake mita, tumelikubali na harakati zimeshaanza,’’anabainisha.
Baadhi
ya wajasiriamali waliopo kituoni hapo, walikiri kuwa walikosa uwelewa na
kuchelewa kuhamia ndani ya kituo hicho, jambo lililochelewa kupanua biashara
zao.
Hija
Omar Khamis, anasema kwa sasa biashara eneo hilo imetononoka, baada ya wateja
kuzoea, tokea walipohamia mwezi Januari, mwaka jana.
Khadija
Sultan, anasema umaarufu wa bidhaa za nguo za mtumba kituoni hapo, kinaendelea
kukua, kadiri siku zinavyosonga.
‘’Ni
kweli pale mwanzo, tulipokuwa tukiondolewa ndani ya mji wa Chake chake, tuliona
kama tunaonewa, ingawa sasa biashara imechangamka kiasi,’’anasema.
Mtama
Mwalimu Haji, anasema eneo hilo sasa limekuwa lulu kwa wenzao, kuja kuwaomba
wachanganye biashara, baada ya kuona soko limekuwa.
MAKUSANYO YA WIZARA NA BARAZA LA MANISPAA CHAKE CHAKE
Aliyekuwa Waziri Ofisi ya
Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Massoud Ali Mohamed,
wakati akisoma bajeti ya mwaka wa fedha 2024/2025, alisema wizara hiyo iliidhinishiwa
kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 5.109.
Ambapo ni kupitia mafungu
yake ya bajeti, kwa ajili ya kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali, ingawa hadi
mwezi Machi 2025, ilifanikiwa kukusanya zaidi zaidi ya shilingi bilioni 3.126 sawa
na asilimia 61.
Kwa Baraza la Manispaa
Chake chake, kwa mwaka huo wa fedha, lilikadiria kukusanya shilingi milioni 880,
788, ingawa nalo lilikusanya wastani wa shilingi milioni 459. 385.
Aidha mwaka huo pia, lilifanikiwa
kutoa mchango wa fedha kwenye mfuko wa pamoja wa kuwawezesha wananchi wa shilingi
milioni 43.814.
Mapungufu hayo ya makusanyo
ya wizara, yanaweza kuchangiwa kwa kiasi kikubwa, kwa Baraza la Manispaa Chake chake
kutokusanya zaidi ya shilingi shilingi milioni 107 kwenye kianzio kipya cha
mapato.
mwisho


Comments
Post a Comment