NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANANCHI wa shehia za Wambaa na Chumbageni wilaya ya Mkoani Pemba, wamesema sasa wanaelekea kuondokana na changamoto ya muda mrefu ya usafiri, kufuatia kuanza kwa ujenzi wa barabara yao, kwa kiwango cha lami.
Walisema,
walidumu zaidi ya miaka minane, wakiwa napita kwenye barabara iliyojaa
changamoto, kwa kuwepo mashimo yenye kina kirefu, misingi isiyotarajiwa, jambo
lililokuwa likiwapa usumbufu.
Wakizungumza
na mwandishi wa habari hizi shehiani humo, walisema kwa sasa, wanaelekea
kusahau machofu na dhiki ya barabara chakavu, kufuatia kuanza kwa ujenzi wa
kiwango cha lami.
Walieleza
kuwa, walikuwa wakiahidiwa na wizara husika kwamba, iko siku ujenzi wa barabara
yao kwa kiwango cha lami utafanyika, ingawa hawakuamini, kutokana na kukaa kwa
siku nyingi.
Mmoja kati
ya wananchi hao Asha Khamis Juma, alisema sasa wanaanza kuona nyota njema,
kufuatia serikali kuanza kutimiza ahadi ya ujenzi wa barabara yao.
‘’Tumeshayashuhudia
magari ya kampuni ya Iris Constriction, yakianza kusafisha barabara
hiyo, na tulipoitwa tuliarifiwa na wajenzi kuwa, ni kwa kiwango cha
lami,’’alieleza.
Nae Mayasa
Haji Mohamed, alisema kwa sasa wanahamu kubwa, kuona siku moja barabara yao
inamalizika kwa kiwango cha lamu, ili wasahau machungu.
‘’Kwa siku
za karibuni, baada ya kumalizika nguvu ile lami baridi iliyotengenezwa kwa
zaidi ya miaka 14 sasa kuharibika, ilitulazimu tunapokwenda Mkoani,
kuzungurikia Mgelema, ili kuyakimbia mashimo,’’alisema.
Nae
mfanyabishara Khamis Omar Khamis, alisema wamekuwa wakipata dhiki ya
kusafirishia bidhaa zao, kutokana na barabara yao, kuzidiwa na uchakavu.
Dereva mwenye
gari ya abiria ya Wambaa-Chake chake Khamis Haji Mohamed, alisema walilazimika
kupitia barabara ya shehia ya Mgelema- Kipapo, ili kukimbia mashimo ya barabara
yao ya Mizingani- Wambaa.
‘’Ukiitumia
barabara hiyo kwenda mjini, ukifika uanzie gereji aidha kuna msumari umetoka au
skuruu imekatika, kutokana na uwepo wa mashimo makubwa,’’alilalamika.
Mapema Ofisa
Mdhamini, wizara ya Ujenzi na Uchukuzi Pemba Ibrahim Saleh Juma, alikiri kuwa
tayari ujenzi wa barabara ya Mizingani-Wambaa, umeshaanza kwa hatua za awali.
Alisema,
waliokabidhiwa ujenzi huo ni kampuni ya Iris Construction, ambayo imeshaanza
kwa hatua za usafishaji wa barabara hiyo.
Alieleza
kuwa, ujenzi huo, pia utajumuisha barabara ya Sisimizini- Andikoni ambako kuna
umabali wa kilomita 2, ambazo zitajumuisha kwa kiwango cha lami.
‘’Ni kweli
baada ya majadiliano makubwa, wizara sasa imeamua kuhakikisha barabara zote,
zilizojengwa kwa kiwango cha lami baridi na mfumo wa ‘labor base’
sasa kuzijenga kwa kiwango cha lami,’’alifafanua.
Aidha Ofisa
Mdhamini huyo, alisema ujenzi huo utakwenda moja kwa moja hadi kwenye uwekezaji
wa hoteli, ili kuhakikisha inarahisisha usafiri kwa watu mbali mbali.
Akizungumzia
kuhusu utaratibu wa ulipwaji wa fidia, alisema baada ya kumalizika kwa sikukuu
za krismas na mwaka mpya, wathamini watapita kila nyumba, iliyokando na bara
bara, ili kuanza harakati za kulipwa.
‘’Kuanzia
mwezi ujao, wenzetu wanaohusika watapita na kuchukua taarifa za kila mmiliki wa
nyumba, ili kuhakikisha analipwa na kupisha ujenzi wa barabara
hiyo,’’alifafanua.
Hivi
karibuni Mkuu wa mkoa wa kusini Pemba, Rashid Hadid Rashid, aliwaambia waandishi
wa habari, kuwa ujenzi wa barabara hiyo na nyingine, utafanyika ndani ya mwaka
huu wa fedha.
Barabara
nyingine ambazo zitaingia kwenye ujenzi wa kiwango cha lami ni Mtambile-
Kangani, Kenya- Chambani na Mtambile- Mwambe, ambazo barabara hizo zilifunguliwa
miaka 14 sasa.
Ambapo
ujenzi wa barabara hizo, ulifanywa kwa mfumo wa lami baridi, na kuwashirikisha
wananchi mwanzo hadi mwisho, ilijengwa kwa ushirikiano kati ya serikali ya
mapinduzi na shirika la misaasa la Norway (NORAD).
MWISHO



Comments
Post a Comment