ZUHURA JUMA NA HAJI NASSOR, BEIJING@@@@
WAANDISHI wa habari wa nchi za Afrika, wametakiwa kuendelea kujifunza lugha mbali mbali, ili kusaidia kukuza uchumi katika mataifa yao.
Akifungua mafunzo ya siku 20 katika Ukumbi wa Hoteli ya RoyalLink ZiYu, Naibu Mkurugenzi wa Shirika la Kimataifa la Mawasiliano (CICG) Han Likiang alisema kuwa, kujua lugha mbali mbali ni muhimu katika kukuza uchumi wa nchi, hivyo kuna haja kwa wanahabari kujifuza zaidi.
Alisema kuwa, ili uchumi ukue unahitaji mambo mbali mbali ikiwemo waandishi wa habari kujifunza lugha ambazo zitawasaidia kuandaa makala, vipindi na habari zenye tija hususan zinazogusa viashiria vya ukuaji wa uchumi wa ndani.
‘’Watakapotumia lugha mbali bali itawasaidia kuwahabarisha watu wengi duniani ambao wanaweza kuvutia hata wawekezaji na wageni, ambayo ni miongoni mwa kukuza uchumi wa ndani,’’ alisema.
Akizungumzia umuhimu wa CICG kuandaa mafunzo hayo ni kuendeleza uhusiano wa kimataifa wa china na mataifa mengine ya Afrika kwa lengo kubadilishana uzoefu wa kisera za kiuchumi miongozi mwa mataifa hayo.
‘’Mafunzo haya yatasaida sana kuendelea kukuza ushurikiano kwa mataifa ya Afrika, kwani watatembelea sehemu mbali mbali ambazo zitawasaidia kutangaza fursa zilizopo katika nchi hii,’’ alisema.
Katika hatua nyingine Naibu Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa kabla ya kuanza kwa mafunzo hayo ya kuwaleta pamoja washiriki wa mataifa mbali mbali, CICG lilikuwa na utamaduni wa kuwafuata waandishi katika mataifa yao.
‘’Lengo la kuwaweka pamoja ni kuona kwamba tunakutana na kujuana, jambo ambalo litasaidia kufanya kazi zetu kwa ushirikiano, huku tukiamini kwamba ni sehemu ya juhudi ya kukuza uchumi katika nchi zetu,’’ alisema.
Mapema Mkurugenzi wa Idara ya Mafunzo ya kimataifa kutoka Shirika la CICG Feng Yin alieleza kuwa, mafunzo hayo ni fursa pekee kwa waandishi wa habari katika kukuza uchumi wa nchi yao, hivyo wanapaswa kuchukua juhudi za makusudi kuhakikisha nchi inapata maendeleo.
‘’Watakapoandika habari mbali mbali zitakazosaidia kukuza uchumi na nchi itapata maendeleo kwa sababu wananchi wanaamini sana vyombo vya habari,’’ alisema.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake, mwandishi wa habari kutoka nchini Zambia, Emeldah Libaga alisema, mafunzo hayo ni muhimu kwao katika kuongeza uhusiano wa kutambua sera za kiuchumi za China ambazo zitasaidia kutanua wigo katika mataifa yao.
‘’Tunalishukuru sana Shirika hili kwa kutuweka pamoja na kutupa mafunzo, hii itatusaidia sana kuongeza uelewa wa masuala mbali mbali ya kiuchumi,’’ alifafanua.
Katika mafunzo hayo yaliyoandaliwa na CICG kwa ufadhili wa Wizara ya Fedha ya China, ambalo limeanzishwa mwaka 1949 yamewashirikisha waandishi kutoka mataifa kadhaa ikiwemo Tanzania Zanzibar, Zambia, Gambia, Kenya, Gana na wenyeji wa China.
MWISHO.
Comments
Post a Comment