Wanawake wameombwa kuvitumia vyombo vya habari ipasavyo kwa lengo la kutangaza kazi wanazozifanya katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Akifungua mafunzo ya siku moja ya kuwajengea uwezo wanawake viongozi kupitia mradi wa ZanzAdapt Mkurugenzi wa TAMWA ZNZ Dkt Mzuri Issa Ali amesema wanawake wanafanya mambo mengi katika jamii ila bado mchango wao haujatambulika kama ilivyo kwa wanaume hivyo kuvitumia vyombo vya habari kutawezesha kutambulika na kujitangaza kwa haraka hasa kupitia mitandao ya kijamii.
Amesema historia ya Tanzania na Zanzibar kwa ujumla haioneshi mchango ama juhudi za wanawake kwa sababu wanawake bado hawajawa na ujasiri na uthubutu wa kutumia vyombo vya habari kwa usahihi.
“Wanawake wanafanya mambo mengi katika jamii na kujitoa zaidi, sasa wakati umefika kueleza changamoto na mambo yanayowahusu kupitia vyombo vya habari ili kupatiwa ufumbuzi,” Dkt Mzuri.
Mkufunzi katika mafunzo hayo Sophia Ngalapi amesema vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kutatua changamoto za kijamii zinazowakabili kwa mamlaka husika kuzitafutia ufumbuzi ikiwa jamii itapaza sauti zao.
‘’Kupitia vyombo vya habari nyinyi nimashahidi tuanaona hatua zinazochukuliwa kwa wahusika endapo kutatokezea tatizo,” Ngalapi.
Akizungumzia mada inayohusu jinsia amesema wazazi/walezi kuwalea watoto wao katika muktadha wa kijinsia kuhakikisha kila mtoto anapata fursa na haki sawa kama zilivyoeleza katiba zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bila kujali jinsia zao.
Nae Afisa Mawasiliano kutoa Jumuiya ya Misitu Pemba (CFP) Munira Iddi Kaoneka amesema wanawake hawana budi kujiamini na kutumia vyombo vya habari kutangaza kazi wanazofanya ikiwemo mitandao ya kijamii kwani ujumbe wao hufikia watu wengi na kwa wakati mmoja.
“Mukilima na kuvuna mazao yenu halafu mukanyamaza kimya nani atajuwa kama muna bidhaa, ila chukuwa video ukivuna mazao kisha rusha Tiktok weka nambari za simu, soko litakuja na watu watakutafuta,” Munira.
Wanawake viongozi waliopata mafunzo ya kuwajengea uwezo na kuwainuwa kiuchumi kwa kulima kilimo msitu chini ya mradi wa ZanzAdapt wamesema watayatumia vyema mafunzo hayo kwa kuwa mabalozi bora wa kuwafunza wengine il kukabiliana na mbadiliko ya tabianchi.
Mradi wa Wanawake na Uongozi katika kukabiliana na mabadilio ya tabianchi (ZanzAdapt) unatekelezwa kwa pamoja na Chama cha Waandishi Wahabari Wanawake Tanzania TAMWA ZNZ, Jumuiya ya Misitu Pemba (CFP) na Jumuiya ya Misitu Kimataifa (CFI) kwa kushirikiana na ubalozi wa Canada.
Comments
Post a Comment