IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA "SIKATI tamaa ipo siku nitafanikiwa lengo langu nililolikusudia kwa sababu kila kitu kimepangwa kwa muda maalumu, hivyo naamini bado wangu haujafika" Sio maneno ya mtu mwengine bali ni Awena Salim Kombo mwenye umri wa miaka 50 mkaazi wa shehia ya Kangagani Wadi ya Kiuyu, Jimbo la Kojani Wilaya ya Wete Pemba. Awena ni mwanamke shupavu mwenye ndoto ya kuwa kiongozi tangu akiwa kijana mdogo, na ndipo mwaka 1990 alipoamua kujiunga kwenye chama cha Mapinduzi CCM, ili kusudi apate nafasi ya kuwa kiongozi. Lengo lake la kusaka uongozi ni kutaka kusaidia jamii kwenye mambo mbalimbali ikiwemo kutatua changamoto zinazowakabili. "Hivi sasa baadhi ya wanajamii wenye matatizo hunifuata kutaka msaada, hivyo wakati mwengine nashindwa kutokana na hali yangu kutomudu" anaeleza. Mwaka 2017 Awena alianza kupata nafasi za uongozi katika chama chake, ambapo alijiona tayari anaenda kutimiza ndoto zake ...